Friday 24 November 2017

Zimbabwe: Shamba la Grace Mugabe lavamiwa na wanakijiji




Mamia ya wanakijiji katika shamba la Arnold katika kijiji cha Mazowe nchini Zimbabwe walivamia shamba la Grace Mugabe ili kusheherekea kung'atuliwa mamlakani kwa kiongozi huyo waliyedai amekuwa akiwanyanyasa na kuwafanya kuwa masikini kwa lengo la kuimarisha mali ya familia yao.

Aliyekuwa rais wa Zimbabwe Robert Mugabe alijiuzulu siku ya Jumanne hatua iliozua sherehe kubwa miongoni mwa raia wa taifa hilo.

Wanakijiji cha Mazowe ambao kwa miaka mingi wamekuwa wakizozana na familia hiyo ya Mugabe kuhusu shamba hilo la Arnold wamesema kuwa wanataka kuonyesha ahsante yao kwa wale wote waliofanikiwa kumng'oa madarakani Mugabe.

Kwa saa kadhaa wanakijiji hao waliobeba mabango waliimba na kucheza densi kwa nyimbo za uhuru huku wengine wakikashifu tamaa ya bwana Mugabe na kuandamana nje ya lango la nyumba ya mayatima la Mazowe wakitaka haki kabla ya kuandamana katika kituo cha maduka pamoja na wenzao wanaosherehekea kuanguka kwa Mugabe.

Wengine hususan wazee walikionyesha chombo cha habari cha Newsday majeraha waliopata baada ya kupigwa na maafisa wa polisi.

Waliionya familia ya Mugabe kutoingia katika shamba lao.

''Kwa sababu ya Grace na Mumewe tulilazimika kuishi katika shamba la Arnold kama wafungwa.Walibomoa nyumba zetu kila mara tulipojaribu kujenga.Walifurahia tulipolala nje na wajukuu zetu'', alisema Stella Nikisi mwenye umri wa miaka 65 akionyesha jeraha alilopata katika mguu baada ya kushambuliwa na maafisa wa polisi.

No comments:

Post a Comment