Friday 24 November 2017

Viongozi Simba wataka Okwi aangaliwe zaidi


KUFUATIA kinara wa mabao Ligi Kuu Bara, Emmanuel Okwi kuwa majeruhi wa enka, uongozi wa klabu hiyo, umetoa rai kuhakikisha mchezaji huyo anapewa uangalizi wa hali ya juu kuona anafanikiwa kupona haraka kutokana na umuhimu wake katika kikosi hicho.

Okwi ndiye anayeongoza kwa kufunga mabao kwenye ligi kuu kwa sasa kutokana na kuwa na mabao nane akifuatiwa na Obrey Chirwa wa Yanga na Mohamed Rashid wa Tanzania Prisons ambao wote wana mabao sita.

Okwi alipata majeraha ya enka kabla ya mechi dhidi ya Prisons ya Mbeya ambapo kwa sasa anaendelea na matibabu.

 Taarifa kutoka Simba zinaeleza kwamba uongozi wa timu hiyo umemkabidhi jukumu Dk Yasin Gembe kuhakikisha anakuwa na uangalizi wa hali ya juu kwa mchezaji huyo kutokana na majeraha aliyonayo.

 “Uongozi umetaka Okwi awe chini ya uangalizi wa dokta kutokana na majeraha aliyonayo, kwa kuwa ndiye kinara wa mabao, hivyo ni vyema akaangaliwa ili aweze kupona kwa haraka na kurejea mzigoni,” alisema mtoa taarifa huyo.

 Simba inaongoza msimamo wa ligi kwa kuwa na pointi 22 huku Yanga ikiwa nafasi ya tatu kwa kuwa na pointi 20 ambapo timu zote zimeshuka dimbani mara 10, hali ambayo inaonyesha ni jinsi gani ligi imekuwa ngumu.

No comments:

Post a Comment