Saturday 25 November 2017

IGP Sirro awaasa wananchi kufanya uchaguzi kwa amani


MKUU wa Jeshi la Polisi Tanzania, Simon Sirro amewatahadharisha wananchi kote nchini kutokuvuruga uchaguzi wa marudio wa udiwani unaotarajiwa kufanyika Novemba 26, mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Sirro amesema kuwa, jeshi lake limejipanga vilivyo kuhakikisha kuwa zoezi hilo la uchaguzi litafanyika kwa amani na utulivu na kwamba ulinzi umeimarishwa katika maeneo yote ya uchaguzi ili kuzuia aina yoyote ya uvunjifu wa amani utakaojitokeza.

“Natoa rai kwa wananchi walioko kwenye maeneo hayo kushiriki zoezi hili la uchaguzi kwa amani na utulivu na wakishapiga kura warejee kwenye maeneo yao na kuendelea na shughuli za ujenzi wa taifa huku wakisubiri kutangazwa kwa matokeo,” alisema Sirro.

Kamanda Sirro vilevile amezungumzia hali ilivyo kwa sasa katika maeneo ya kibiti na Rufiji kuwa hali ni shwari na wananchi waendelee kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi.

“Kuhusiana na uharifu wa kutumia silaha katika Wilaya za Mkuranga, Kibiti na Rufiji tumefanikiwa kuwakamata waharifu waliokuwa wakijihusisha na matukio haya ambao wamekiri kufanya matukio mbalimbali ya mauaji na baadhi yao wamekimbilia nchi za jirani ikiwemo Msumbiji na Jamhuri ya Kidemokrasia ya CONGO lakini hata hivyo kutokana na ushirikiano mzuri uliopo kati ya nchi hizi. Lakini tutaendelea kuwashughulikia hata huko walikokimbilia.

No comments:

Post a Comment