Friday 24 November 2017

Mtoto wa Mfalme Saudia asema Hayatollah ni 'Hitler' mpya



Mwanamfalme wa Saudia amemtaja kiongozi wa kidini wa Iran kuwa 'Hitler' mpya wa eneo la mashariki ya kati huku kukiwa na wasiwasi kati ya mataifa hayo mawili.

Akitaja kuongezeka kwa ubabe wa Iran katika eneo hilo, Mohammed Bin Salman amesema kuwa ni vyema kuzuia yaliotokea barani Ulaya katika eneo la mashariki ya kati.

Saudia na Iran ni wapinzani na wamekuwa wakishutumiana kwa kuchochea ukosefu wa uthabiti katika eneo la mashariki ya kati.

Hatahivyo hakuna tamko lolote liliotolewa na Iran kufuatia matamshi hayo ya hivi karibuni.

Akizungumza na gazeti la The New York Times , Mohammed bin Salman alisema kuwa Iran haiwezi kuruhusiwa kusambaza ushawishi wake.

''Tulijifunza kutoka Ulaya kwamba kujionyesha kwamba wewe ni mtu mzuri hakufanikiwi''.
''Hatutaki Hitler mpya wa Iran kurudia yaliotokea barani Ulaya katika eneo la mashariki ya kati'', alisema akimtaja kiongozi wa kidini wa Iran Ayatollah Ali Khamenei.

Mohammed bin Salman, ambaye ndio mtawala mkuu wa ufalme huo amekuwa na msimamo mkali dhidi ya Iran tangu alipochukua mamlaka katika kipindi cha miaka miwili iliopita.

Mapema mwezi huu ,aliishutumu Iran kwa kile alichosema ni uchokozi wa kivita akiilaumu kwa shambuio la kombora lililolenga mji mkuu wa Saudia, Riyadh, na waasi katika taifa jirani la Yemen.
Iran imekana kwamba ilihusika.

No comments:

Post a Comment