Saturday 25 November 2017

Kocha wa Simba awaambia wachezaji wake kutowadharau Lipuli katika mechi yao Kesho



KOCHA wa Simba, Joseph Omog amewataka wachezaji wake kutowadharau wapinzani wao wa kesho timu ya Lipuli ya Iringa na kuwataka kuwa makini kwa dakika zote 90.

Akizungumza kabla ya kuanza mazoezi ya jana kwenye uwanja wa chuo cha Polisi Kurasini, Omog, alisema kuwa hawatakiwi kuwabeza wapinzani wao hao kwa kuwa mpira ni mchezo wa makosa.

“Hakuna timu ndogo kwenye ligi, wachezaji nimekuwa nikiwaambia hivyo, lazima nidhamu ya mchezo ifuatwe, kama wachezaji watafuata maelekezo tuna nafasi nzuri ya kushinda,” alisema Omog.

Alisema kuwa kwenye mazoezi ya timu hiyo inayodhaminiwa na kampuni ya Sportpesa, amekuwa akikazania wachezaji wake kucheza soka la kasi na kuhakikisha wanatumia vyema nafasi wanazozipata.

“Kwanza naangalia zaidi ushindi kabla ya kutazama wingi wa mabao, kama tutatengeneza nafasi nyingi na kuzitumia vizuri tunaweza kupata ushindi wa mabao mengi,” aliongeza kusema Omog.

Alisema kuwa licha ya ugeni wa Lipuli kwenye ligi, anaamini nao wamejiandaa vizuri kwa ajili ya kupata ushindi kwenye mchezo huo wa kesho utakaochezwa kwenye uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

“Walipata pointi moja walipokuja hapa kucheza na Yanga.., kwa hiyo si timu ya kubeza, tutapambana kwa ajili ya pointi tatu,” aliongezea kusema Omog.

Simba ipo kileleni kwa msimao wa ligi ikiwa na pointi 22 sawa na Azam FC wanaoshika nafasiya pili lakini wekundu hao wa msimbazi wana magoli mengi.

No comments:

Post a Comment