Saturday 25 November 2017

RC Aggrey Mwanri aamua kuwapa fursa hii vijana




Vijana Mkoani Tabora wametakiwa kuacha tabia ya kukaa vijiweni na kusikiliza maneno ambayo hayawasaidii wala kuwafundisha namna ya kupata maendeleo.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri katika maeneo mbalimbali ya Kata za Wilaya ya Kaliua kwenye zoezi la uhamasishaji wa kilimo cha kisasa cha zao la Pamba na mazao mengine.

Aidha mkuu huyo wa mkoa amewataka vijana kutumia muda wao kujiajiri katika sekata ya kilimo na uzalishaji wa pamba pamoja na mazao mengine yatakayowasaidia kujipatia kipato na kuinua maisha yao.

“Kijana uliyekuja hapa leo ninakuambia kuwa kama unarafiki yako unashinda nae kijiweni na kucheza karata, Pool kuanzia leo achana naye, kwani hana nia njema nawewe, mwambie kuwa mkuu wa mkoa amenifundisha juu ya kulima pamba kisasa kuanzia sasa urafiki wangu mimi na wewe bye bye”, amesema RC Mwanri.

Mkuu wa Tabora yuko katika ziara mkoani mwake kuhamasisha kilimo cha kisasa cha zao la pamba na mazao mengine ambayo yatawasaidia wakulima kupata pesa zitakazoboresha maisha yao.

Lema amueleza Mrisho Gambo maneno haya



Mbunge wa Arusha Mjini, Mh. Godbless Lema amemtaka Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mrisho Gambo kutojaribu kufanya hila zozote za kuisababishia CCM ipate ushindi kwenye uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika hapo kesho, Nov 26.

Lema amesema kwmba anafahamu kila hatua na vikao ambavyo Mkuu huyo wa Mkoa na kwamba ana ushahidi wa kutosha wa kila kitu kunachopangwa.

"Mrisho Gambo,unapaswa kujua kwamba huna mamlaka wala  uwezo wa kushinda huu uchaguzi kwa nguvu/hila, hakuna kikao umekaa ambacho sina taarifa zake na ushahidi wa kila kitu".  Lema
Aidha Lema ameongeza kwa kumkanya kiongozi huyo asijaribu kufanya hivyo.

"Unataka kushinda uchaguzi huu kwa gharama yoyete ile ?sababu polisi wako nyuma yako ? usijaribu" Lema ameandika kupitia ukurasa wake wa Twitter asubuhi ya leo
Kesho kata 43 zinatarajiwa kufanya uchaguzi wa marudio wa kuwapata madiwani.

Waziri Kigwangalla awajibu wanaosema vyuma vimekaza



Waziri wa Maliasili na Utalii Mh. Hamisi Kigwangalla amesema maisha yataendelea kuwa magumu kwa watu wasio na shughuli maalum ambao wamezoea kuishi kwa ujanja ujanja.

Ameyasema hayo wakai akijibu maswali ya wananchi kupitia mtandao wa ‘Twitter’ ambao wengi walitaka kujua kuhusu utendaji kazi wake na hali halisi ya maisha yalivyo wakidai kuwa ni magumu.

“Wanaofanya shughuli zao halali hawatoona vyuma vimekaza, badala yake watafurahia sema watoto wa mjini, wasanii sanii na wajanja wajanja ndiyo watapata shida! Hawa wajanja wajanja ni wangapi? Na wenye shughuli halali ni wangapi?”, alisema Kigwangalla akiacha maswali kwa mmoja wa watu waliomuuliza.

Waziri Kigwangalla aliendelea kwa kutoa ufafanuzi juu ya namna ya kujenga uchumi kupitia kufanya kazi na sio kutegemea kupata pesa kwa njia rahisi rahisi.

“Mfumo wa uchumi unataka watu tufanye kazi kwa ubunifu ndipo tupate maisha mazuri siyo kufanya usanii kidogo tayari ukatajirika! Kukaza vyuma maana yake kuziba mianya ya wasanii ili walio kwenye uchumi halisi na wasanii wawe sawa siyo kuonea watu!” alimaliza.

Waziri Kigwangalla hivi sasa yupo jimboni kwake Nzega vijijini akiwa amepiga kambi kwaajili ya kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata ya Nata.

Bwana harusi afariki, mkewe ajeruhiwa katika ajali wakitoka kufunga ndoa



Watu 12 wamekufa na wengine 22 kujeruhiwa katika ajali iliyotokea kijiji cha Ighuka wilayani Ikungi kwenye Barabara Kuu ya Singida – Manyoni baada ya Toyota Hiace waliyokuwa wakisafiria kutoka kumchukua bibi harusi kugongana uso kwa uso na Toyota Noah iliyokuwa imepakia watu kutoka msibani.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Debora Magiligimba alisema kuwa ajali hiyo ilitokea juzi saa mbili usiku kwa kulihusisha gari lenye namba za usajili T 581 BBV iliyokuwa ikitokea Singida kwenda Manyoni na T 423 CFF iliyokuwa ikitokea Manyoni kwenda Singida.

Alisema kuwa ingawa uchunguzi wa kina juu ya chanzo cha ajali hiyo bado unaendelea, taarifa za awali zinaonesha kuwa sababu kuu ni mwendo kasi na uzembe wa madereva.

“Baadhi ya majeruhi walituambia dereva wa Toyota Hiace aliyekuwa anatoka Singida mjini alihama kutoka upande wake na kwenda upande wa pili wa barabara ambako aligongana uso kwa uso na Noah iliyokuwa imebeba watu waliokuwa wakitoka msibani na kusababisha vifo vya abiria 10 hapo hapo na majeruhi 24,” alisema.

Mganga Mfawidhi Hospitali ya Rufaa mkoa wa Singida, Dk Ng’hungu Kusenza alisema kuwa majeruhi wawili waliofikishwa Hospitali ya Misheni Puma kwa ajili ya matibabu pia walikufa hivyo kufanya idadi ya watu waliokufa kuwa 12.

Aliwataja waliokufa ambao miili yao imehifadhiwa Hospitali ya mkoa kuwa ni John Duma, Jasson Nsunza, Abubakar Omari, Mary Kinku, Mwanaidi Juma na Husna Juma, Wengine ambao miili yao imehifadhiwa Hospitali ya Misheni Puma wilayani Ikungi ni Ezekiel Joseph, Mussa Daniel, Namtaki Daniel, Hamis Omari, Jumanne Mganga na Wansola Shalua. Habari ambazo hazijathibitishwa zinadai kuwa Bwanaharusi na madereva wa magari yote mawili ni miongoni mwa watu waliopoteza maisha katika ajali hiyo.

Chanzo: Habarileo

Mbeya City yafanya mabadiliko haya



Klabu ya soka ya Mbeya City imelazimika kubadili jezi yake iliyokuwa imepanga kuitumia kwenye mechi ya ugenini leo dhidi ya Singida United.

Mbeya City imefikia uamzi huo baada ya kuwepo kwa mfanano kati ya jezi yake ya Singida United ambao ni wenyeji wao katika mchezo wa leo.

Jezi hizo ni kama zinavyoonekana hapo chini ambapo kushoto ni jezi ya wenyeji Singida United na kulia ni jezi ya Mbeya City iliyokuwa imepangwa kutumika leo.



Hata hivyo bado Mbeya City hawajasema ni jezi gani ambayo watatumia lakini msimu huu jezi zao za pili kwaajili ya mechi za ugenini ni zile zenye rangi ya damu ya mzee hivyo huenda ndio zitakazotumika leo.

Singida United inayoshika nafasi ya 5 ikiwa na alama 17 inacheza leo na Mbeya City yenye alama 11 katika nafasi ya 10 kwenye mchezo wa raundi ya 11, uwanja wa Namfua mjini Sungida.

Kocha wa Simba awaambia wachezaji wake kutowadharau Lipuli katika mechi yao Kesho



KOCHA wa Simba, Joseph Omog amewataka wachezaji wake kutowadharau wapinzani wao wa kesho timu ya Lipuli ya Iringa na kuwataka kuwa makini kwa dakika zote 90.

Akizungumza kabla ya kuanza mazoezi ya jana kwenye uwanja wa chuo cha Polisi Kurasini, Omog, alisema kuwa hawatakiwi kuwabeza wapinzani wao hao kwa kuwa mpira ni mchezo wa makosa.

“Hakuna timu ndogo kwenye ligi, wachezaji nimekuwa nikiwaambia hivyo, lazima nidhamu ya mchezo ifuatwe, kama wachezaji watafuata maelekezo tuna nafasi nzuri ya kushinda,” alisema Omog.

Alisema kuwa kwenye mazoezi ya timu hiyo inayodhaminiwa na kampuni ya Sportpesa, amekuwa akikazania wachezaji wake kucheza soka la kasi na kuhakikisha wanatumia vyema nafasi wanazozipata.

“Kwanza naangalia zaidi ushindi kabla ya kutazama wingi wa mabao, kama tutatengeneza nafasi nyingi na kuzitumia vizuri tunaweza kupata ushindi wa mabao mengi,” aliongeza kusema Omog.

Alisema kuwa licha ya ugeni wa Lipuli kwenye ligi, anaamini nao wamejiandaa vizuri kwa ajili ya kupata ushindi kwenye mchezo huo wa kesho utakaochezwa kwenye uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

“Walipata pointi moja walipokuja hapa kucheza na Yanga.., kwa hiyo si timu ya kubeza, tutapambana kwa ajili ya pointi tatu,” aliongezea kusema Omog.

Simba ipo kileleni kwa msimao wa ligi ikiwa na pointi 22 sawa na Azam FC wanaoshika nafasiya pili lakini wekundu hao wa msimbazi wana magoli mengi.

Faiza Ally amuonyesha mpenzi wake mambo mapya


Muigizaji wa Filamu Bongo, Faiza Ally ameamua kumuweka wazi mpenzi wake mpya baada ya kuachana na Mr. Sugu aliyebahatika kupata naye mtoto mmoja aitwaye Sasha.

Mrembo huyo ametumia fursa ya mtandao wa kijamii wa Instagram kuweka picha akiwa na mwanaume huyo anayehisiwa  kuwa  baba mzazi wa mtoto wake wa pili wa kiume aliyempata miezi kadhaa iliyopita, picha hiyo imewaonyesha wawili hao wakiwa wanapigana busu zito.





Rais Magufuli ampongeza kikwete



Rais wa Serikali ya awamu ya tano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ametoa sifa na pongezi kwa rais mstaafu wa awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kufanikisha ujenzi wa hospitali ya Mloganzila.

Rais ametoa pongezi hizo leo wakati akihotubia wananchi waliohudhuria ufunguzi wa Hospitali na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kampasi ya Mloganzila jijini Dar es salaam.

“Wakati ujenzi wa Hospitali hii unaanza mimi nilikuwa naagizwa tu na niliambiwa nikatafute eneo kubwa nikawaza nitalitoa wapi lakini baadae mzee Jakaya akanipigia tena simu  akaniambia kuna eneo huko Mloganzila ni la serikali nenda kaangalie na ujenzi uanze haraka, ndio nikaja hapa”, amesema Rais Magufuli.

Rais magufuli ameongeza kuwa “Watu tunapenda sifa lakini hizi sifa sio zangu ni za rais Mstaafu wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwani mimi nilikuwa naagizwa tu nikiwa waziri wa Ujenzi, ndio maana nimeona niseme wazi kuwa sifa zote zimwendee mzee Kikwete”.

Aidha rais Magufuli ameweka wazi kuwa wakati anakwenda kuona eneo la Mloganzila wala hakukuwa na barabara lakini aliambiwa na rais Kikwete aanze ujenzi wa miundombinu ikiwemo barabara haraka iwezekanvyo na alifanya hivyo sambamba na waziri wa maji amnbaye naye aliagizwa kuanza ujenzi wa miundombinu ya maji.

Rais Magufuli amesisitiza kuwa kukamilika kwa ujenzi wa Hospitali na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kampasi ya Mloganzila jijini Dar es salaam ni mpango na jitihada za rais wa awamu ya nne.




Hiki ndio kikosi cha Yanga dhidi ya Tanzania Prisons leo



Yanga wanaokwenda Chamazi kuwava Tanzania Prisons kwenye Uwanja wa Azam Complex Chamazi, leo, hawa hapa..

1. Youthe Rostand
2. Juma Abdul
3. Gadiel Michael
4. Andrew Vincent
5. Nadir Haroub
6. Pato Ngonyani
7. Pius Buswita
8. Raphael Daud
9. Obrey Chirwa
10. Ibrahim Ajibu
11. Emmanuel Martin

AKIBA:
 Beno Kakolanya
Hassan Kessy
Maka Edward
Yusuph Mhilu
Said Mussa
Geofrey Mwashiuya

Mali: Maafisa 4 wa UN wauawa



Umoja wa Mataifa umesema maafisa wake wanne walinda amani pamoja na mwanajeshi mmoja wameuawa na wengine kujeruhiwa katika shambulio lililofanywa eneo la mpakani baina ya Mali na Niger.

Afisa mkuu anayekiongoza kikosi hicho cha walinda amani walioko Mali bw. Mahamat Saleh Annadif, bila kutaja washambulizi ni akina nani, amelaani vikali tukio hilo akisema ametamaushwa na kisa hicho dhidi ya maafisa wake ambao walikuwa wakiendeleza kazi ya udumishwaji wa amani na vilevile kutoa misaada hasa ya kimatibabu kwa wakaazi wa maeneo ambayo yamekumbwa na hali mbaya ya kuzorota kwa usalama.

Kuna makundi kadhaa ya wapiganaji yanayopatikana eneo hilo la Mali, yaliyo na uhusiano na kundi la Al Qaeda.

Umoja wa mataifa umekuwa na kikosi cha walinda amani huko Mali tangu 2013 wakisaidiwa pia na kikosi cha kijeshi cha Ufaransa.

Mbowe afunguka kuhusu kampeni za udiwani



Moshi. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema wamewazidi CCM kimkakati katika kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani utakaofanyika kesho  katika kata 43 nchini.

Mbowe amesema chama tawala hakina mpango mkakati wa kufahamu mambo gani wananchi wanataka na shida gani zinawakabili zaidi ya kuzungumzia kwa jumla na kujinasibu kufanya mambo makubwa ikiwamo kujenga barabara, kununua ndege na kupambana na mafisadi.

Amesema leo Jumamosi Novemba 25,2017 kuwa ndiyo maana katika kampeni za kuwanadi wagombea wa uchaguzi huo alinadi ajenda tatu ambazo ni dhana ya uhuru, maendeleo na demokrasia.

Mbowe amesema maendeleo hayapimwi kwa kununua magari, kujenga viwanja vya ndege, kupambana na mafisadi bali yanapimwa kwa maisha ya mwananchi mmoja mmoja.

"Tunaaminishwa uchumi unakuwa kwa sababu nchi imenunua ndege, inapambana na mafisadi na inajenga viwanja vya ndege, hayo ni mambo mazuri hakuna anayepinga, lakini je, mwananchi wa kawaida ananufaika vipi," amesema Mbowe.

Amesema hali ya maisha ni ngumu, hivyo Serikali isijifungie na isizibe masikio kusikia wanacholalamika wananchi.

"Wananchi wana hali ngumu, sisi tuliozunguka na kuzungumza nao tunajua, biashara zinafungwa, wananchi masikini hali zao zimezidi kuwa ngumu, watumishi hawajapandishiwa mishahara hivyo hali kuzidi kuwa duni kwa wanaotegemea kuchuuza bidhaa kwa sababu hakuna anayemudu kununua," amesema Mbowe.

Amesema amani ya kudumu na demokrasia haiwezi kuwepo kama hakuna nafasi ya vyama vya siasa kufanya kazi zake bila kuonekana kama wahalifu.

Mbowe amesema wananchi wana kiu na shauku ya kuhudumia mikutano ya kisiasa.

Mwananchi:

Zitto Kabwe asema kinachotakiwa ni mabadiliko ya maendeleo kabla ya 2020


 

Mtwara. Kiongozi wa Chama wa ACT -Wazalendo, Zitto Kabwe amesema kitendo cha kuchukua watu kutoka vyama vya upinzani siyo mafanikio bali kinachotakiwa ni kuwaletea wananchi mabadiliko ya maendeleo kabla ya mwaka 2020.

Zitto alisema hayo juzi katika mkutano wa kampeni za udiwani Kata ya Reli mjini Mtwara.

“CCM kazi yao sasa hivi ni kuchukua watu kutoka vyama vya upinzani, wanaona ni mafanikio wakisajili dirisha dogo. Huu mtaa wenu si ulikuwa hivi tangu mwaka 2015 kuna mabadiliko yoyote?

“Itakapofika mwaka 2020 mtaangalia wamechukua watu wangapi kutoka upinzani au mtaangalia mabadiliko kwenye mtaa wenu?” Alihoji Zitto.

Pia, alisema ameshangaa kuona foleni ya watu waliojipanga kwenye meli ya Wachina inayotoa huduma za afya jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kupata huduma akidai hiyo ni dalili ya kuonyesha kuna tatizo.

Aliendelea kusema kuwa maendeleo si idadi ya madaraja, bandari na barabara za juu zilizojengwa bali ni afya, elimu na uwezo wa wananchi kufanya shughuli za kiuchumi.

Zitto alisema kwa sasa Tanzania inajenga reli lakini inachukua vyuma kutoka Uturuki ikiwa ni pamoja na kampuni ya kuponda kokoto kwa ajili ya ujenzi wa reli.

“Nchi ya aina gani, kuna haja gani ya huu uhuru ambao tunao mpaka sasa? CCM inaamini ninyi nyote mtawapa kura,” alisema.

Mgombea wa udiwani wa kata hiyo, Mwajuma Hassan alisema kwamba vipaumbele vyake ni kuhakikisha kila mkazi wa kata hiyo anajiajiri.

Pia, mgombea huyo aliahidi kusimamia huduma za kijamii kama afya, maji na elimu.

Mwananchi:

Waziri wa zamani wa fedha Zimbabwe afikishwa mahakamani




Aliyekuwa waziri wa fedha wa Zimbabwe,Ignatius Chombo amefika mahakamani kujibu mashtaka ya  ulaji rushwa dhidi yake.

Kwa mujibu wa habari,Chombo huyo alikamatwa wiki mbili zilizopita wakati jeshi lilipochukua utawala nchini humo.

Bwana Chombo alifukuzwa katika chama cha ZANU-PF Jumapili iliyopita.

Hata hivyo Chombo ameonekana akiingia mahakamani akiwa hana wasiwasi.

Emmerosn Mnangagwa ameapishwa kuwa rais mpya wa Zimbabwe.Baada ya kuapishwa kwake rais huyo mpya ametakwa na baadhi ya wafuasi wake kulishughulikia kundi la G-40 linalosemekana kuwa lilikuwa likimuunga mkono Mugabe na mkewe.

Chombo alikuwa kati ya wanachama wa G40

Hii kali...Roboti iliyopewa uraia nchini Saudi Arabia yataka kuwa na familia



Roboti iliyopewa uraia nchini Saudi Arabia imesema kuwa ina haki ya kuwa na familia.

Roboti hiyo kwa jina la Sophia  ilitengenezwa nchini Hong Kong na kupewa uraia nchini Saudi Arabia mwezi uliopita.

Roboti hiyo Ä°imesema kuwa ingependa kuwa na familia wakati ilipohudhuria mkutano wa habari ulioandaliwa nchini UAE.

Kwa mujibu wa habari roboti hiyo imesema kuwa familia ni kitu muhimu sana.

Robot hiyo imesema kuwa kila mwanadamu ana haki ya kuwa na familia na watu wenye hisia sawa na yeye.Jambo hilo ni muhimu sana hata kwa roboti.Aliwaambia wanadamu wajisikie furaha kuwa na familia.

Filamu mpya ya bollywood yazua mzozo nchini India



Filamu mpya ya Bollywood  ambayo bado haijazinduliwa imeleta kizaazaa baina ya viongozi wa juu nchini India.

Filamu hiyo kwa jina la Padmavati imepingwa vikali na wanasiasa wa chama tawala serikalini pamoja na makundi ya mrengo wa kulia hata kabla ya uzinduzi wake.

Maisha ya mtayarishaji wa filamu hiyo pamoja na waigizaji yapo hatarini kutokana na kuigizizwa kwa filamu hiyo.

Filamu inaelezea historia ya Malkia Padmavati wa dini ya kihindu wakati wa karne ya 14.

Malikia Padmavati alijichoma moto akiwa hai baada ya Mfalme Khalji ambae alikuwa ni muislamu kuwavamia na kumuua mumewe.

Waigizaji maarufu Deepika Padukone na  Ranveer Singh wamecheza kama Padmavati na Sultan Khalji.

Makundi yanayoipinga filamu hiyo yanadai kuwa filamu hiyo imebadilisha baadhi ya matukio ya kihistoria.

Hata hivyo mtayarishaji wa filamu hiyo amekana tuhuma hizo.

Baadhi ya watu kutoka katika Kabila la warajput pamoja na waumini wa kihindu wamepinga filamu hiyo kutokana na mahusiano ya kimapenzi yaliyoonyeshwa kati ya mfalme wa kiislamu na malkia wa kihindu.

Wamedai ni aibu kubwa na uvunjaji heshima kwa kabila lao.

Dk Shika kupanda jukwaani kumnadi mgombea wa CCM


Mwanza. Katika kampeni za lala salama leo, CCM itawapandisha jukwaani aliyekuwa mwenyekiti wa Bavicha, Patrobas Katambi na Dk Louis Shika, aliyejizolea umaarufu baada ya kuibuka kwenye mnada wa nyumba za mfanyabiashara Said Lugumi.

Katambi aliyejiunga na CCM akitokea Chadema na Dk Shika watamnadi kwa wapiga kura wa Kata ya Mhandu jijini Mwanza mgombea wake, Constantine Sima.

Katibu wa uenezi wa CCM Wilaya ya Nyamagana, Mustapha Banigwa amesema leo Jumamosi Novemba 25,2017 kuwa wengine watakaopanda jukwaani katika mkutano utakaofanyika mtaa wa Machinjioni ni waziri wa zamani wa Mambo ya Ndani ya Nchi na mbunge wa Nyamagana, Lawrence Masha aliyerejea CCM akitokea Chadema.

Mkutano huo pia utahutubiwa na mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM na aliyekuwa mbunge wa Bunda, Stephen Wasira, mbunge wa Nzega Mjini, Hussein Bashe na mbunge wa Bukombe, Doto Biteko.

Uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata 43 nchini utafanyika kesho Jumapili Novemba 26,2017.

Mwananchi:


Chadema yawaomba wapiga kura kukaa mita 100



Dar es Salaam. Chadema wamewataka   wapiga kura kukaa umbali wa mita 100  wakati wa kusubiri matokeo yao kwenye uchaguzi mdogo wa madiwani utakaofanyia kesho katika kata 42 nchini, ili kulinda kura zao.

Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, Jeshi la Polisi lilipinga wapiga kura kukaa umbali wa mita 100 na baadaye Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kuhitimisha sakata hilo kwa kutamka kuwa kukaa umbali wa mita 200, baada ya kupiga kura hairuhusiwi.

Akielezea mwenendo wa uchaguzi huo, Mkurugenzi wa Operesheni na Mafunzo wa Chadema,  Benson Kigaila amesema  sheria inaruhusu wapiga kura kukaa umbali huo ili kulinda kura zao.

“Sheria ya vyama vya siasa ya mwaka 1992 inataka wapiga kura kusimama umbali wa mita 100, kwa hiyo tuwaambie wapiga kura wetu wakishamaliza kupiga kura wakae umbali wa mita hizo, waongeze na nyingine moja walinde kura zao,” amesema

Kigaila amewataka  wapiga kura hao kwenda kwenye vituo vya kupigia kura na kutimiza wajibu wao bila kuogopa kitisho chochote na baadaye walinde kura zao hadi zitakapotangazwa.

“Waende wakapige kura wasiogope kitisho chochote,” amesema a kuwataka baadaye waende kwenye makao makuu ya kata yatakako tangazwa matokeo hayo kuhakikisha, washindi wanatangazwa kwa haki.

Kiongozi huyo wa Chadema amesema kumekuwa matukio ya uvunjaji wa haki kwenye mikutano yao ya kampeni ikiwamo makada wake kuvamiwa na kupigwa.

“Upinzani ukishinda utatangazwa wapende wasipende, ambaye atatangaza matokeo tofauti ashughulikiwe kama mwizi mwingine wa kawaida kwa sababu wezi huwa wanashughulikiwa,”

“Kwa hiyo watu waende walinde haki yao ya kikatiba, wapige kura na walinde matokeo. Yatangazwe matokeo sahihi.” amesema  kiongozi huyo wa  Chadema

Rais Magufuli aeleza sababu ya kuliacha jengo la Tanesco akiwa waziri



Dar es salaam. Rais John Magufuli amesema hakubomoa jengo la Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) lililopo Ubungo alipokuwa waziri wa ujenzi kwa kuwa aliogopa kufukuzwa kazi.

Rais Magufuli amesema hayo leo Jumamosi Novemba 25,2017 alipozindua Hospitali ya Taaluma na Tiba ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (Muhas), kampasi ya Mloganzila.

Akizungumza mbele ya waziri mkuu wa Serikali ya Awamu ya Nne, Mizengo Pinda aliyehudhuria uzinduzi huo, Magufuli amesema wakati huo aliogopa baada ya kuzuiwa na waziri mkuu huyo, lakini sasa yeye ndiye Rais hakuna wa kumzuia.

Akizungumzia ubomoaji unaoendelea sasa amesema, “Nilishatoa maagizo, najua Mizengo Pinda kwenye hili alinipinga wakati ule, lakini najua leo hawezi akanipinga kwa sababu mimi ndiye Rais. Wakati ule nilikuwa waziri wake, ndiyo maana nilinyamaza nilijua ninaweza nikafukuzwa, hutakiwi kumpinga mkubwa.”

 “Hilo jengo la Tanesco, narudia kama itakuwa ni kubomoa nusu, no problem (hakuna tatizo); kama ni lote hakuna tatizo, pamoja na jengo la wizara ya maji. Najua katibu mkuu wa wizara ya maji yupo hapa ananiangalia, wakaanze kulitoa eneo lililopo kwenye hifadhi ya barabara,” amesema.

Machi 6, 2011 akihutubia wananchi katika mkutano wa hadhara mjini Chato, mkoani Kagera, Pinda ambaye alisifia utendaji wa Dk Magufuli alimwagiza kusimamisha ubomoaji maeneo kadhaa yaliyokuwa kwenye hifadhi ya barabara likiwemo jengo la Tanesco hadi Serikali itakapotoa kauli nyingine kuhusu hilo.

Pinda alikuwa akizungumzia hatua ya Dk Magufuli aliyekuwa amewaagiza wananchi waliojenga nyumba ndani ya hifadhi ya barabara kuanza kubomoa nyumba hizo na wasitarajie kulipwa fidia.

Pinda wakati huo akiwa waziri mkuu alisema spidi (kasi) ya Magufuli ilikuwa kubwa hivyo alimuagiza kusimamisha ubomoaji huo hadi suala hilo litakapojadiliwa na Baraza la Mawaziri.

Pinda, ambaye alikuwa waziri mkuu kuanzia 2008 baada ya kujiuzulu kwa Edward Lowassa alisimamisha ubomoaji huo ili kutoa nafasi kwa Serikali kujipanga upya.

Alisema Serikali inamuamini Magufuli kuwa kiongozi mwenye uwezo na ndio maana ilimpa nafasi akawabane makandarasi wazembe.

Dk Magufuli akiwasilisha bajeti bungeni mwaka 2012/13, alizungumzia ubomoaji akisema siasa iachwe akisisitiza sheria zimepitishwa ikiwamo Sheria namba 13 ya mwaka 2007 na ya hifadhi ya barabara iliyoanza tangu mwaka 1932.

Alizungumzia jengo la Tanesco alisema liko kwenye hifadhi ya barabara na kwamba hata kama asipolibomoa yeye kuna siku litabomolewa vinginevyo sheria ibadilishwe.

Novemba 15 akitokea Chato alipokwenda kwa mapumziko baada ya ziara ya Uganda, Magufuli alimuagiza wakala wa barabara nchini (Tanroads) kuweka alama ya X katika jengo la Tanesco na Wizara ya Maji, sehemu zilizo katika hifadhi ya barabara.

Mwananchi:

Mourinho amponda Mkhitaryan, amwambia kiwango chake kimeshuka



Mkufunzi wa Manchester United Jose Mourinho ameukosoa mchezo wa Henrikh Mkhitaryan huku Borussia Dortmund ikisema kuwa iko tayari kumsajili kwa mara nyengine mshambuliaji huyo wa Armenia

Mkhitaryan, ambaye alijiunga na United kutoka Dortmund mwezi Julai 2016 kwa dau la £26.3m, hakushirikishwa katika kikosi cha United katika mechi mbili zilizopita.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 28 hatahivyo atarudi katika kikosi cha kwanza cha United katika mechi ya Jumamosi dhidi ya Brighton.

Mourinho alisema kuwa kiwango cha mchezo wa Mkhitaryan kimekuwa kikipungua hatua baada ya hatua

Mkhitaryan alianzishwa mechi 10 kati ya 11 za ligi ya Uingereza kabla ya kuachwa nje baada ya kutolewa katika dakika 62 katika mechi ambayo United ilipoteza kwa Chelsea kwa 1-0 mnamo tarehe 5 mwezi Novemba.

"Sikufurahia kiwango chake cha mchezo'', alisema Mourinho kuhusu mchezaji ambaye amefunga mabao mawili pekee katika mechi 16 alizochezeshwa msimu huu.

Waziri Kigwangalla awajibu wanaosema vyuma vimekaza




Waziri wa Maliasili na Utalii Mh. Hamisi Kigwangalla amesema maisha yataendelea kuwa magumu kwa watu wasio na shughuli maalum ambao wamezoea kuishi kwa ujanja ujanja.

Ameyasema hayo wakai akijibu maswali ya wananchi kupitia mtandao wa ‘Twitter’ ambao wengi walitaka kujua kuhusu utendaji kazi wake na hali halisi ya maisha yalivyo wakidai kuwa ni magumu.

“Wanaofanya shughuli zao halali hawatoona vyuma vimekaza, badala yake watafurahia sema watoto wa mjini, wasanii sanii na wajanja wajanja ndiyo watapata shida! Hawa wajanja wajanja ni wangapi? Na wenye shughuli halali ni wangapi?”, alisema Kigwangalla akiacha maswali kwa mmoja wa watu waliomuuliza.

Waziri Kigwangalla aliendelea kwa kutoa ufafanuzi juu ya namna ya kujenga uchumi kupitia kufanya kazi na sio kutegemea kupata pesa kwa njia rahisi rahisi.

“Mfumo wa uchumi unataka watu tufanye kazi kwa ubunifu ndipo tupate maisha mazuri siyo kufanya usanii kidogo tayari ukatajirika! Kukaza vyuma maana yake kuziba mianya ya wasanii ili walio kwenye uchumi halisi na wasanii wawe sawa siyo kuonea watu!” alimaliza.

Waziri Kigwangalla hivi sasa yupo jimboni kwake Nzega vijijini akiwa amepiga kambi kwaajili ya kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata ya Nata.

CAF yataka Yanga, Simba Kupeleka Majina




Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limezitaka Simba na Yanga haraka kupeleka majina ya wachezaji wake kwa Shirikisho la Soka Afrika (Caf) kwa ajili ya ushiriki wa michuano yake mwakani, pia watakaguliwa mahesabu yao.

Yanga itashiriki Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kuwa bingwa wa Ligi Kuu Bara msimu uliopita, huku Simba wakishiriki Kombe la Shirikisho kutokana na kuwa mabingwa wa Kombe la FA.

Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas, alisema klabu hizo zinatakiwa kuwasilisha majina yao Caf mapema kabla ya mwisho wa mwezi huu.

“Simba na Yanga wanatakiwa kutuma majina ya usajili wa wachezaji wao mapema kabla ya Novemba 30, mwaka huu kwa sababu wakichelewa inaweza
kuwa tatizo kwao,” alisema Lucas.

 “Na kwa sasa kamati ya leseni za klabu inakwenda kufanya ukaguzi katika klabu hizo ili kufahamu kama zimetimiza matakwa ya kupata leseni ya kushiriki michuano ya Caf.

“Timu zitakaguliwa ofisini na watendaji wake, umiliki wa nyaraka mbalimbali, ukaguzi wa mahesabu na ripoti ya fedha ya mwaka mzima kama Kanuni ya 11 ya ligi kuu na kanuni ya saba ya Caf zinavyojieleza kuhusiana na leseni za klabu,” alisema Lucas.

Chelsea wawasili Liverpool tayari kwa kazi



Chelsea wametua salama jijini Liverpool kwa ajili ya mechi yao dhidi ya Liverpool ambayo inasubiriwa kwa hamu leo Anfield.

Lakini kiungo mkongwe wa timu hiyo, Cesc Fabregas amefanya kituko wakati wakiwasili, ameonekana akiwa amefunika uso wake gubi gubi.

Kwa kila timu, mechi hiyo ni muhimu, Liverpool ikataka kurejesha imani na kasi yake katika EPL lakini Chelsea ambao ni mabingwa watetezi wanataka kujiweka katika nafasi nzuri zaidi ya kutetea taji.

Tambwe yupo fiti kuivaa Tanzania Prisons leo



MSHAMBULIAJI Mrundi, Amissi Joselyn Tambwe anatarajiwa kurejea leo timu yake, Yanga ikimenyana na Tanzania Prisons Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Tambwe hajacheza mechi hata moja ya mashindano msimu huu, baada ya kuumia katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Chipukizi Uwanja wa Gombani kisiwani Pemba Agosti  20 mwaka huu, Yanga ikijiandaa na mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya mahasimu, Simba.

Na baada ya kufanya mazoezi mfululizo wiki hii, ikiwa ni mara ya kwanza kufuatia kushindwa kufanya mazoezi japo kwa siku mbili mfululizo awali, kocha Mzambia wa Yanga, George Lwandamina anatarajiwa kumtumia Tambwe katika sehemu ya mchezo wa leo.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Yanga, Dissmas Ten alisema jana mjini Dar es Salaam kwamba Tambwe yuko fiti na atakuwepo kwenye mchezo wa leo.

Ten alisema majeruhi ambao wataendelea kukosekana katika kikosi hicho ni Wazimbabwe, kiungo Thabani Kamusoko na mshambuliaji Donald Ngoma ambao wote wanapambana na hali zao warejee uwanjani mapema. 

Kiungo Mkongo, Papy Kabamba Tshishimbi alikuwa anasumbuliwa na Malaria naye anaweza kukosekana katika mchezo wa pili mfululizo leo, baada ya kutokuwepo pia wakati Yanga ikiichapa 5-0 Mbeya City Jumapili iliyopita.

Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara iliendelea jana kwa mchezo mmoja tu, wenyeji Ndanda FC wakilazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 na Njombe Mji FC Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara.

Mechi nyingine za leo, Singida United watakuwa wenyeji wa Mbeya City Uwanja wa Namfua, Singida, Mbao FC wataikaribisha Mwadui FC Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, Kagera Sugar wataikaribisha Stand United Uwanja wa kambarage Shinyanga na Ruvu Shooting watakuwa wenyeji wa Maji Maji Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.

Kesho Simba SC watakuwa wenyeji wa Lipuli ya Iringa Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na mzunguko wa 11 wa Ligi Kuu inayoonyeshwa moja kwa moja na Televisheni ya Azam TV utakamilishwa Jumatatu ijayo kwa mchezo mmoja kati ya wenyeji, Azam FC na Mtibwa Sugar Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Zimbabwe: Morgan Tsvangirai aomba Mugabe kusamehewa



Kiongozi wa chama cha ZANU-PF Lovemore Matuke amesema kuwa hakushiriki katika harakati za kumuondoa Mugabe madarakani.

Kwa mujibu wa habari,Matuke amesema kuwa Mugabe na familia wako salama na daima atakumbukwa kama shujaa.

Wakati huohuo kiongozi wa upinzani Morgan Tsvangirai amewataka wananchi wamsamehe Mugabe.

Morgan Tsvangirai amesema kuwa ni vyema Mugabe akasamehewa na taifa kwani si taifa halijengwi kwa kulipiza visasi.

Misri: Rais al Sisi aahidi adhabu kali kwa wliohusika na shambulizi dhidi ya mskiti Sinai


Rais wa Misri Abdel Fatah al Sisi aahidi adhabu kali kwa magaidi waliohusika na ashambulizi dhidi ya mskiti lililopelekea vifo vya watu zaidi ya 230  Sinai

Rais wa Misrii Abdel Fatah al Sisi ameahidi adhabu kali kwa magaidi waliohusika na shambulizi walilotekeleza  katika mskiti wakati wa kutekelezwa ibada ya Ijumaa.

Watu 235 walifariki na wengine zaidi ya 130 kujeruhiwa katia shambulizi lililolenga mskiti wa al Arish unaopatikana Sinai nchini Misri.

Jeshi la Polisi litatoa jibu linalostahili kwa waliotekeleza shambulizi hilo.


Wastara ateswa na macho yake




STAA wa filamu za Kibongo, Wastara Juma ameibuka na kueleza jinsi macho yake yanavyomtesa kwani watu wamekuwa wakimsema vibaya kuwa anajilegeza makusudi akitaka kutupia picha mtandaoni.

Akipiga stori na Risasi Jumamosi,Wastara alisema kuwa macho yake ndivyo yalivyo kwani amezaliwa hivyo ni macho yaliyolegea kama mtu mwenye usingizi wakati wote na kutokana na vichambo anavyovipata amejikuta akitamani kuhama Insta lakini hawezi kwa sababu ana manufaa na page yake.

“Jamani haya macho yananitesa kwani kutwa kucha natukanwa mitandaoni kuwa nalegeza macho hawajui kuwa nimeumbwa hivi kwani hata nikijitahidi kuyafanya yawe magumu nashindwa, hivyo watu wakisema najifanyisha huwa najisikia vibaya kusema ukweli,” alisema Wastara.

Baada ya kimya kirefu, Jokate afunguka kuhusu Lulu



MWANAMITINDO Jokate Mwegelo hivi karibuni baada ya kukaa kimya bila kumposti msanii mwenzake Elizabeth Michael ‘Lulu’ wala kuongea lolote kuhusiana na hukumu yake ambapo mastaa kibao walionesha kumuhurumia na k
umposti kwa kuweka maneno tofauti tofauti, yeye ameibuka na kusema kuwa anamuombea dua huko alikoenda kwani ndio jambo pekee ambalo anaweza kulifanya.

Akilonga na Risasi Jumamosi, Jokate alisema kuwa yeye anamuombea dua Lulu Mungu amfanyie wepesi huko alikokwenda kwani ndio njia pekee ya kumfariji.

Mwanamitindo huyo aliongea hayo baada ya kuulizwa sababu ya yeye kutomposti na maoni yake juu ya hukumu hiyo. “Kikubwa ni kumuombea na mimi namuombea ndicho ninachoweza kusema,” alisema Jokate.




Sikutarajia Dk Slaa kuwa balozi - Profesa Lipumba



   Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chama cha CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amezungumzia uteuzi wa Dk Wilbroad Slaa kuwa balozi akisema hakutarajia.

Rais John Magufuli juzi alimteua Dk Slaa aliyewahi kuwa katibu mkuu wa Chadema kabla ya kukihama chama hicho wakati wa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Wakati wa mchakato wa uchaguzi huo, Profesa Lipumba na Dk Slaa ambao vyama vyao vilikuwa katika umoja uliojulikana Ukawa, walijiondoa baada ya Chadema kumpitisha Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kuwa mgombea wake wa urais.

Akizungumza na Mwananchi jana, Profesa Lipumba alisema, “Imekuwa kama surprise, sikutegemea kama Dk Slaa atateuliwa kwa sababu muda mwingi yupo Canada.”

Hata hivyo, Profesa Lipumba alisema hana shaka na uteuzi huo kwa kuwa Dk Slaa ni mzoefu wa siasa na mzalendo ambaye ataitumikia vyema nafasi hiyo mpya.

“Narudia, sikutegemea. Ila popote atakapopangiwa kazi Dk Slaa atafanya kwa sababu najua ni mchapakazi,” alisema.

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema Rais Magufuli ana mamlaka kisheria ya kumteua mtu atakayemuona anafaa katika nafasi fulani.

“Huu ni uamuzi wa Rais sisi wengine hatuna comments zaidi ya kuwatakia kila heri katika utendaji wao wa kazi,” alisema Mbowe ambaye pia ni mbunge wa Hai mkoa wa Kilimanjaro.

Akizungumza uteuzi huo wa Dk Slaa, Makamu Mwenyekiti wa Chadema, Profesa Abdallah Safari alisema Rais Magufuli amemuonea huruma Dk Slaa ndiyo maana akaamua kumpa nafasi ya ubalozi.

Profesa Safari alisema hawezi kumsema vibaya Dk Slaa lakini nafasi hiyo ni huruma na zawadi ya Rais Magufuli.

Amedai Dk Slaa alijaribu kuivuruga Chadema wakati wa uchaguzi mkuu mwaka 2015 lakini hakufanikiwa.

“ Hii ni huruma. Siku zilizopita Dk Slaa aliandikwa katika vyombo vya habari kuwa anafanya kazi Super Market. Mimi nimekaa Ulaya najua maisha ya kule na Dk Slaa ni rafiki yangu sana lakini kwa kitendo alichokifanya mwaka juzi, haya ndiyo matokeo yake,” alisema Profesa Safari.

Kwa upande wake, aliyewahi kuwa Balozi wa Tanzania nchini Urusi kuanzia mwaka 2002 hadi 2008, Patrick Chokala alimpongeza Rais Magufuli kwa kumteua Dk Slaa kuwa balozi.

“Sina shaka hata kidogo na Dk Slaa ana uwezo wa kufanya kazi nchi yoyote. Hii kazi anaiweza na ni mtu mwenye dhamira ya kweli,” alisema Balozi Chokala.

Alisema anamfahamu Dk Slaa kwa kipindi kirefu tangu akiwa padre na kwamba, amekuwa ni mchapakazi hodari na mwenye hekima kwa watu.

Akizungumza na kituo cha televisheni cha Azam TV, Dk Slaa alimshukuru Rais Magufuli kwa kumteua ili aungane naye kujenga nchi na hivyo atafanya kazi kwa uwezo wake wote.

Dk Slaa ambaye hivi sasa anaishi Canada alisema, “Ni mapenzi ya Mungu, nashukuru kwa uteuzi. Ninachoweza kusema katika hatua hii, huu ni wajibu mkubwa kwenye kipindi cha kulijenga Taifa letu.”    

Mwananchi:

Wema Sepetu asema ameirudisha heshima ya Bongo Movie

Wema Sepetu asema ameirudisha heshima ya Bongo Movie


Msanii wa filamu nchini Tanzania, Mrembo Wema Sepetu ambaye yupo nchini Rwanda tangu Jumatano ya wiki hii, amesema ndiye aliyeifufua tasnia ya Bongo Movie iliyokufa baada ya kifo cha Kanumba.

Wema amesema marehemu Kanumba alipofariki  hata kiwanda cha Bongo Movie kilionekana kuyumba kwani alikuwa ndiye nguzo muhimu kwenye ramani ya filamu Tanzania.

“Zamani Bongo Movie ilikuwa inafanya vizuri sana enzi za marehemu Steven Kanumba, alivyofariki kama na yenyewe ikafa. Tumekuwa tukiomboleza kifo chake na kifo chake kimetusababishia mazingira mabaya sisi kama waigizaji  kwa sababu tuko kwenye fani moja. Wengi wetu tumejikuta watu wanaona Bongo Movie haina mashiko.“amesema Wema Sepetu kwenye mkutano na Waandishi wa Habari jijini Kigali nchini Rwanda na kuelezea jinsi alivyoinyanyua Bongo Movie baada ya kifo cha Kanumba.

“Kwa bahati nzuri mimi nimeweza kuirudisha tena Bongo Movie back to where it was (ilipokuwa enzi za Kanumba) baada ya kutoa filamu yangu ya Heaven Sent. Bongo Movie kama Bongo Movie zilikuwa zimelala kiukweli kabisa mpaka nilipozindua filamu yangu hiyo na nimeweza kuiweka kwenye application yangu kumekuwa kuna muhemko, yaani waigizaji wengi hata mkiwaona kwenye mitandao ya kijamii wanashoot, wanafanya vipindi, yaani Bongo Movie haijafa ni kazi nzuri tu tumeshindwa kuziweka sokoni. Tukiwa tuna kazi nzuri tukafanya vitu ambavyo vitapendwa na watu Bongo Movie itakuwa imara tena Inshallah!“.

Steven Charles Kanumba almaarufu The Great alifariki katika mazingira ya kutatanisha mnamo mwezi Aprili 2012 akiwa chumbani kwake na mpenzi wake Elisabeth Michael ‘Lulu’ ambaye mwezi huu amehukumiwa kifungo cha miaka miwili jela kwa kosa la kumuua Kanumba bila kukusudia.