Friday 12 January 2018

Joh Makin akana kuwa na bifu na Fid Q



Kama wewe ni mpenzi au mdau wa muziki wa Hip Hop hapa Bongo, basi hakuna ubishi kuwa kolabo kubwa inayosubiriwa na mashabiki ni kolabo kati ya Joh Makini na Fid Q.

Je, unajiuliza kolabo hii huenda ikatokea? ukweli ni kwamba ondoa shaka kwa hilo kwani Joh Makini amesema kuwa ni muda tu unasubiriwa kwani wawili hao hawajahi kukaa pamoja kuzungumzia ishu za kolabo lakini endapo ikitokea nafasi ya kufanya hivyo watafanya.

“Mimi na Fid Q hatuna matatizo kama ambavyo watu wanafikiri, kwa sababu mimi mwenyewe binafsi sijawahi kuwa na matatizo naye na wala sijawahi kuona kama anamatatizo na mimi. Kwa hiyo mimi kama msanii na yeye kama msanii Chochote kinaweza kutokea anytime,“amesema Joh Makini kwenye kipindi cha Playlist cha Times FM huku akielezea kikwazo cha muda

“Ni vile labda hatujawahi kukutana kwenye hiyo vibe, hatujawa bado kwenye hiyo Chemistry ya kusema tufanye ngoma pamoja so you never know..hakuna mipaka 2018,“amemaliza Joh Makini.

Waziri awaapisha bodaboda kuwalinda watoto wa kike


Madereva Bodaboda wa wa Manispaa ya Mpanda Mkoa wa Katavi wamekula kiapo cha uaminifu cha kuwalinda watoto wa kike dhidi ya vitendo vya ngono na mimba za utotoni zinazo sababisha kukatisha haki yao ya kuendelezwa.

Kiapo hicho kimeongoza na Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile(Mb) ikiwa ni mwendelezo wa utekelezaji wa Kampeni ya “Mimi ni Msichana Najitambua Elimu Ndio Mpango mzima” iliyozinduliwa tarehe 11 Oktoba, 2017 kwa lengo la kuhamasisha wananchi kupambana na kuzuia matukio ya mimba za utotoni katika jamii zetu.

Dkt.Ndugulile amesema kuwa ili kufanikisha kutokomeza mimba za utotoni hatuna budi kuweka ushirikiano baina ya wazazi, walezi, jamii, Serikali na wadau wengine ili kuwaepusha watoto wa kike kupata vishawishi vya mahusiano ya kingono katika umri mdogo na hatimaye kupata mimba za utotoni.

Ameongeza kuwa lengo la Kampeni ya “Mimi ni Msichana Najitambua Elimu ndio Mpango Mzima” imelenga kuunganisha nguvu za pamoja za wanajamii wakiwemo madreva wa Bodaboda kushirikiana na Serikali kuzuia na kutokomeza matukio ya mimba za utotoni katika ngazi ya jamii na shuleni.

“Niseme kampeni hii itasaidia kwa asilimia kubwa kuunganisha nguvu zetu kama wananchi na sisi Serikali katika kutokomeza vitendo hivi viovu”alisisitiza Mhe. Dkt. Ndugulile.

Aidha Dkt. Ndugulile amewaasa madereva hao kuondokana na tamaa za kujihususha na mahusiano na kingono na watoto wadogo bali wao kuwa walinzi wao katika kutokomeza suala mimba kwa watoto wetu.

Amewataka kufichua vitendo vyovyote vyenye ushawishi wa mahusiano yanayosababisha mimba kwa watoto wa kike ili Sheria iweze kuchukua mkondo wake.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Mhe. Lilian Matinga amesema kuwa wataendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kwa kuweka mikakati ya kupambana na wanaume na vijana wakware wanaotumia fursa zao kuwa na mahusiano maovu na watoto wa kike katika Wilaya ya Mpanda Mkoa wa Katavi ambao ndio unaoongoza kitaifa kwa kuwa na asilimia 45.

Mmoja wa dereva Boda boda wa Wilaya ya Mpanda Bw. Juma Salum kwa wakati tofauti wameishukuru Serikali kwa kuandaa Kampeni hiyo itakayowajengea uelewa wananchi kusaidiana katika kuwalinda watoto wa kike kwa kuweka miundo mbinu salama ya kusomea na kujifunzia ili kupunguza kiwango cha mimba za utotoni kwa silimia 50 ifikapo mwak 2021/22.

Naibu Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile (Mb) alikuwa na ziara ya siku mbili mkoani Katavi kuhamasisha wananchi kupambana na kuzuia mimba za utotoni kupitia “Kampeni ya Mimi ni Msichana Najitambua Elimu Ndio Mpango mzima”.




Staa wa Soka Nigeria awa kichaa



Ijumaa ya January 12 2018 katika mitandao ya kijamii zimeenea taarifa za kusikitisha kuhusu staa wa zamani wa soka wa kimataifa wa Nigeria aliyewahi kuvichezea vilabu mbalimbali Ulaya Wilson Oruma kuripotiwa kuwa amepata ukichaa.

Oruma ameripotiwa kupata ukichaa baada ya kutapeliwa na mchungaji (Pastor) wake Naira bilioni 1.2 ambazo ni zaidi ya shilingi Bilioni 75 za kitanzania, ambapo mchungaji huyo alimshauri Oruma ampatie pesa hizo ili wafanye uwekezaji katika biashara ya mafuta.

Kama utakuwa unakumbuka vizuri Wilson Oruma licha ya kuiongoza Nigeria U-17 kama nahodha na kutwaa Ubingwa wa dunia 1993, amewahi kuvichezea vilabu mbalimbali Ulaya kama Olympique Marseille, Sochaux, Servette na Lens.


Wandishi DRC waanzisha mgomo baada ya mwenzao kutekwa


Siku ya leo taarifa ambazo zimeshika vichwa vya vyombo vingi vya habari  nchini DR Congo ni kuhusu wandishi wa habari nchini humo kuitisha mgomo usio na kikomo baada ya kutekwa kwa mwandishi mwenzao.

Mwandishi wa habari wa Radio China (CRI), Molelwa Mseke Jide ameripoti kuwa waandishi wa Habari wa mji wa Beni nchini humo walikuwa kwenye kikao cha kuazimia mgomo huo.

Jide amesema kuwa mwandishi aliyetekwa ni Kiongozi Mkuu wa Radio Graben iliyopo mji wa Goma anayeitwa Kasereka Jadomwangwingwi.

Ameeleza kuwa mwandishi huyo alitekwa jana January 11, 2018 saa 11 jioni akiwa ndani ya msafara wa magari yaliyokuwa yakitokea mji wa Kasindi ambao upo mpakani mwa Congo na Uganda akielekea mji wa Beni.

Akisimulia mkasa huo Jide amesema msafara wa mwandishi huyo na watu wengine ulitekwa na majambazi waliovalia sare zilizofanana na za jeshi la taifa, ambapo waliwachukua watu wengine akiwemo na yeye

Lipumba, Nchemba na Nape wafunga kampeni za udiwani


Kampeni za uchaguzi mdogo wa ubunge na udiwani utakaofanyika zimefungwa leo kwa wagombea na wapambe wao kutoa tambo mbalimbali.

Majimbo yatakayofanya uchaguzi huo kesho Januari 13, 2018 ni Longido, Singida Kaskazini, Songea Mjini pamoja na Udiwani kwenye Kata kadhaa.

Katika jimbo la Singida Kaskazini, Mbunge wa Iramba Magharibi (CCM), Dk Mwigulu Nchemba amefunga kampeni hizo katika Kijiji cha Pohama tarafa Mgori alikozaliwa aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Lazaro Nyalandu.

Dk Mwigulu ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Ndani akimnadi mgombea wa CCM Justine Monko amewahimiza wapinga kura kumpingia kura Monko kama njia ya kuunga mkono kazi inayofanywa na Rais John Magufuli.

"Ndugu zangu wa Pohama na hasa marafiki wa Nyalandu (Lazaro), msinune kwa vile rafiki yenu amehama mkaacha kuipigia CCM, mpeni kura Monko kwa vile Nyalandu pengine alighafilika na akazinduka akarejea CCM ambayo wewe hukuipigia kura,” amesema Dk Mwigulu.

Dk Mwigulu ametumia mkutano huo kuwaonya wale wote watakaothubutu kuvurunga uchaguzi huo wa udiwani na Ubunge kwamba hatua kali zitachukuliwa dhidi yao.

Akiomba kura, Monko amewaomba wananchi wa Singida Kaskazini kumchagua kwani uzoefu anao kupitia majukumu aliyonayo sasa ya Ukurugenzi wa Halmashauri ya Liwale mkoani Lindi na pindi wakimwamini kumpa jukumu la kuwawakilisha ataanza na kero za Pohama.

Naye mbunge wa zamani wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi) ambaye amehamia CCM, Moses Machali amesema  “Rais Magufuli amefilisi sera zote za upinzani na ndicho kitendo kilichotufanya sisi kuja CCM.”

“Enzi zetu sisi ndio tulikuwa wapinzani wa kweli, upinzani wa sasa umejimaliza wenyewe baada ya kuamua kwa makusudi kupokea mafisadi na ndio maana hawana nguvu,” ameongeza

Naye mbunge wa Mtama Nape Nnauye (CCM) akifunga kampeni Longido amewataka wananchi wa jimbo hilo kumchagua Dk Steven Kiruswa kwani kwa sasa upinzani umekufa na waliopo wanapaswa kuondoka wasing’ang’anie huko kama kupe katika ng’ombe wasubiri hadi afe.

Huko Songea Mjini, Mwenyekiti wa CUF anayetambuliwa na ofisi ya Msajili wa vyama vya siasas, Profesa  Ibrahim Lipumba akifunga kampeni katika Viwanja vya Soko Kuu amewataka wananchi kuchagua mgombea wa Chama hicho Christina  Thinangwa.

Profesa LIpumba amesema endapo watamchagua mgombea wa CCM, Dk Damas Ndumbaro hawatoweza kutatua migogoro inayoendelea ndani ya Baraza la madiwani wa Manispaa ya Songea.

Amesema Thinangwa atasaidia kupunguza matatizo ya vifo vya kinamama kwani wanawake wengi  wanafariki dunia kutokana na kukosa damu, kutokuwa na uwezo wa kulipia gharama za afya iwapo watapata mtu wa kuwasemea matatizo yao yatatatuliwa na mtu pekee ni mgombea wa CUF.

Kuhusu hali ya uchumi, Profesa Lipumba amesema Tanzania haiwezi kufikia  uchumi wa kati iwapo haitaboresha sekta ya kilimo kwani Serikali imeshindwa kuwajengea uwezo wakulima ili waweze kuzalisha chakula kwa wingi.

Bodi za Elimu matatani Handeni


BODI za elimu za shule za msingi wilayani Handeni mkoani Tanga zimepewa miezi sita kuhakikisha kiwango cha elimu kinakua ili kuepuka bodi hizo kuvunjwa.

Hayo yalisemwa jana na Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Godwin Gondwe, wakati wa kikao cha wadau wa elimu wa halmashauri za wilaya za vijijini na mjini za wilaya hiyo kilichoandaliwa na ofisi yake kwa lengo la kuongeza kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wilayani humo.

Gondwe alisema bodi hizo ziandaliwe barua kukumbuka majukumu yao ili kupandisha kiwango cha ufaulu na bodi itakayoshindwa kufanya hivyo ndani ya muda uliopangwa, itavunjwa.

“Bodi za shule wilaya ya Handeni zisimamie ukuaji wa elimu kuanzia mwezi huu hadi Juni na itakayoshindwa itavunjwa kupitia ofisi za wakurugenzi,” alisema.

Aidha alisema kiwango cha ufaulu kwa mwaka 2017 walichojiwekea wilayani humo kilipanda na kuvuka lengo kutoka asilimia 10 hadi asilimia 12, na katika kikao hicho wameazimia kiwango cha ufaulu kifikie asilimia 30 kwa mwaka huu.

Hata hivyo, baadhi wa walimu wakuu wa shule walieleza changamoto zinazowakumba katika shule zao na  kusema ongezeko la wanafunzi kwa mwaka huu ni kubwa ikilinganishwa na mahitaji ya shule.

“Mimi katika shule yangu nimeandikisha wanafunzi 1,085 kuanzia awali hadi darasa la saba, vyumba vya madarasa hatuna na tupo walimu 11 tu, tuna uhaba mkubwa wa walimu tulitegemea tutapata mwaka huu, lakini nimeambiwa walimu walikuja 24 na tayari wameshapangiwa shule mimi sikupata kabisa,” alisema Saidi Kiduo, Mwalimu Mkuu Shule ya Msingi Sua.

Akijibu hoja hizo mkuu wa wilaya alisema Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 400 ili kupata uwiano wa ikama kwa walimu wa shule za msingi nchini, hivyo tatizo la uhaba wa walimu linashughulikiwa na litakwisha.



Naibu waziri wa Ujenzi ameiagiza Temesa kupeleka Kivuko



NAIBU Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi,  Elias Kwandikwa, ameuagiza uongozi wa Wakala wa Ufundi na Umeme (Temesa) makao makuu kusaini haraka mkataba kwa mkandarasi atakayebeba kivuko kipya  kutoka eneo kinapotengenezwa wilayani Pangani mkoani Tanga hadi mkoani Lindi.

Taarifa ya wizara hiyo ilimkariri Kwandikwa akitoa agizo hilo wakati akizungumza baada ya kukagua maegesho ya kivuko hicho ambacho alisema kinatarajiwa kutoa huduma za usafiri kutoka Lindi Mjini-Kitunda mkoani humo, na kuwahakikishia wananchi kutegemea kupata huduma nzuri za usafiri kwani ujenzi wa kivuko na  maegesho  yake kwa sasa umefika katika hatua nzuri.

“Naagiza mamlaka husika kusaini haraka mkataba kwa mkandarasi atakayebeba kivuko hiki kutoka Tanga hadi hapa ili wananchi waone kwamba kivuko kimefika na kipo tayari kwa ajili ya kutoa huduma,” Naibu Waziri Kwandikwa alikaririwa akisema.

Aidha, Naibu Waziri huyo aliridhishwa na ujenzi wa maegesho hayo ambayo kwa sasa ujenzi wake umebakia asilimia 10, hivyo kutarajiwa kukamilika muda wowote.

Katika hatua nyingine, Kwandikwa, alitembelea na kukagua uwanja wa ndege wa Lindi ambapo alisema Serikali inaendelea na mpango wake wa kuboresha viwanja vya ndege nchini ili kuimarisha huduma katika usafiri wa anga.

Alifafanua kuwa Serikali kupitia mwaka wa fedha 2018/19 licha ya kuwa na mpango wa kuboresha uwanja huo, pia itaboresha uwanja wa ndege wa Kilwa Masoko lengo ni kuleta maendeleo kwa wananchi.

Meneja wa Temesa mkoani Lindi, Greyson Maleko, alimhakikishia Naibu Waziri huyo kujipanga katika kuhakikisha wananchi wa Lindi wanapata huduma bora za kivuko.

Naye, Mbunge wa Viti Maalum kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), mkoani humo, Hamida Abdallah, aliipongeza na kuishukuru Serikali kwa kusogeza maendeleo kwa wananchi na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili.

Kwandikwa alimaliza ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani humo kwa kutembelea na kukagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na Wizara yake ili kujionea m

Mkuu wa Wilaya kupambana na Uvuvi haramu


MKUU wa Mkoa wa Rukwa, Joachim Wangabo, amemwagiza Mkuu wa Wilaya ya Kalambo na kamati yake ya ulinzi na usalama, kuandaa mkakati wa kumaliza uvuvi haramu katika mwambao wa Ziwa Tanganyika.

Amesema uvuvi haramu unaoendelea katika mwambao huo, unahatarisha maendeleo ya viwanda vya samaki vilivyopo na hatimae kudhoofisha ajira za wananchi walioko karibu na viwanda hivyo, hivyo kukwamisha juhudi za serikali ya awamu ya tano katika maendeleo ya viwanda.

“Mwisho wa mwezi huu nataka taarifa ya namna mlivyojipanga kupiga marufuku uvuvi haramu ikiwa ni pamoja na kutoa elimu na kuwakamata wale wanaokaidi na kuendesha uvuvi haramu. Vitendo hivi vikiendelea hiki kiwanda hakitakuwapo kwa sababu ya kuua samaki na watoto wake. Achaneni na uvuvi haramu, mnamaliza samaki katika ziwa letu hili,” alisema Wangabo alipokuwa katika ziara yake juzi.

Alisema samaki ndiyo rasilimali pekee inayowaajiri na kuendesha kiwanda na kuwataka wananchi kuungana kuhakikisha wanatunza na kupiga marufuku aina zote za uvuvi haramu. Pia alionya kuwa hataki kusikia kiwanda kimefungwa kutokana na kukosa samaki kwa sababu ya uvuvi haramu.

Katika ziara hiyo, Wangabo alitembelea viwanda viwili vya samaki vya Migebuka Fisheris Tanzania Limited na Akwa Fisheries Tanzania Limited, vilivyoko katika kata ya Kasanga. Kati ya hivyo, Migebuka ndicho kiwanda pekee kinachojikongoja huku  Akwa kikiwa kimesimamisha uzalishaji.

Awali, akisoma taarifa ya kiwanda cha Migebuka, Mtendaji wa Kijiji cha Muzi, Gasper Kateka, alisema mbali na ukosefu wa samaki changamoto nyingine ni umeme na barabara jambo linalowafanya kutumia gharama kubwa kuendesha kiwanda hicho kwa majenereta na kupakia samaki kwenye boti hadi bandari ya Kasanga ili kuwasafirisha kwenda Sumbawanga kukwepa kipande cha barabara cha Km 1.2 kilichojaa mawe.

Kwa upande wake, Ofisa Uvuvi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo, Godfrey Makoki, alisema makubaliano ya matumizi ya Ziwa Tanganyika yaliyofanywa na nchi nne (Zambia, Burundi, Tanzania na DR Congo) katika kikao kilichofanyika mwaka 2012 Bujumbura, Burundi, katika kanuni ya nne ya makubaliano hayo imekataza uvuvi wa dagaa mchana katika Ziwa Tanganyika.

“Jambo linalotupa shida ni uvuvi wa dagaa mchana. Kitaalamu dagaa huwa wanakuja kutaga mchana hivyo wanakuwa wakubwa kwa sababu wana mayai na usiku huwaoni, sasa huwa tunawaambia kuwa huo ni uvuvi haramu hapo inakuwa tatizo,” Makoki alibainisha.

Kuhusu changamoto ya umeme na barabara, Wangabo alimwagiza Meneja wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) Mkoa wa Rukwa kuhakikisha umeme wa vijijini awamu ya tatu unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA)  unawafika haraka katika kijiji hicho.

Pia alisema atawasiliana na Wakala wa Barabara Vijijini (TARURA) na wakala wa Taifa wa Barabara (Tanroads) kushirikiana na Mkurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha ndani ya miezi mitatu wanairekebisha barabara ya Km 1.2 ili ipitike kwa urahisi.

Mwambao wa Ziwa Tanganyika kwa Mkoa wa Rukwa una viwanda vinne vya samaki.  Viwili viko Kata ya Kipili Wilaya ya Nkasi na viwili vipo Kata ya Kasanga, wilaya ya Kalambo.


Serikali kuchunguza madai ya Meli ya Tanzania kukamatwa Ugiriki

SERIKALI imesema inachunguza taarifa za meli iliyokamatwa nchini Ugiriki ikiwa na bendera ya Tanzania ikipeleka vilipuzi Libya.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk. Susan Kolimba, akizungumza na Nipashe jana kuhusu tukio hilo, alisema wanafuatilia kwa kina ili kupata ukweli wake.

“Kwa sasa ni kwamba jambo hilo tunalifuatilia ili kujua habari hizo kama zina ukweli na tutakapopata taarifa tutawajulisha, bado tunafuatilia,” alisema Kolimba.

Jana, Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) ilieleza kuwa maofisa wa Ugiriki wanaofanya doria baharini  wameizuia meli hiyo iliyokuwa inapeperusha bendera ya Tanzania ikiwa imebeba vilipuzi.




Taarifa hiyo ya BBC ilieleza kuwa meli hiyo inadaiwa kusafirisha vilipuzi hivyo kutoka Uturuki kwenda Libya, kinyume cha sheria iliyowekwa ya kutosafirisha silaha kwenda Libya.

Iliongeza kuwa maofisa hao wameeleza kwamba meli hiyo ilikuwa imebeba kreti 29 zilizojaa vilipuzi pamoja na kemikali zinazotumiwa kuunda vilipuzi.

"Maofisa wa kushika doria baharini wamezima bomu lililokuwa linasafiri," ofisa mkuu wa walinzi hao wa Ugiriki, Yiannis Sotiriou alikaririwa na BBC jana.

Taarifa ya BBC ilieleza kuwa Wizara ya Safari za Baharini ilisema meli hiyo ilisimamishwa ikiwa katika kisiwa cha Crete kusini mwa Ugiriki baada ya maofisa kupatiwa taarifa na ilisindikizwa hadi katika bandari ya kisiwa hicho na kufanyiwa ukaguzi.

Sotiriou alikaririwa katika taarifa hiyo akieleza kuwa meli hiyo ambayo ilinaswa Jumamosi ilikuwa pia na kasoro nyingi na haikufaa kuwa baharini.

"Ingesababisha madhara makubwa sana kwa watu na mazingira pia," alikaririwa katika ripoti hiyo ya BBC.

Ilielezwa zaidi katika ripoti hiyo kuwa nahodha wa meli hiyo ambaye alifahamika kwa jina moja la Andromeda, alidai meli hiyo ilikuwa inasafiri kuelekea Djibouti lakini baadaye ikabainika kwamba ilikuwa inasafiri kuelekea mji wa bandarini wa Misrata nchini Libya.

Kwa mujibu wa ripoti ya BBC, mabaharia wanane ambao ni raia wa India, Ukraine na Albania waliokuwa kwenye meli hiyo, walitarajiwa kufikishwa mbele ya mwendesha mashtaka jana.

TLS kimefanikiwa kukusanya mamilioni kugharamia matibabu ya Lissu




Dar es Salaam. Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) kimesema kimefanikiwa kukusanya Sh138 milioni kugharamia matibabu ya Rais wa Chama hicho, Tundu Lissu aliyelazwa Hospitali ya Chuo Kikuu cha Leuven nchini Ubelgiji.

Taarifa iliyotolewa na Makamu Mwenyekiti wa TLS, Godwin Ngwilimi amesema kiasi hicho wamekipata kutoka kwa watu mbalimbali walijitolea kuchangia wa ndani na nje ya nchi wakiwemo wanachama wa chama hicho.

Kuhusu mchanganuo wa fedha hizo, Ngwilimi amesema kimetumika kulipa gharama za matibabu ya Lissu katika Hospitali ya Nairobi, Leuven na visa kwa watu watatu wakiwa nchini Ubelgiji.

Ngwilimi ametoa shukuran kwa wale wote waliojitokeza kuchangia matibabu ya Lissu ambaye pia ni mbunge wa Singida Mashariki na mwanasheria mkuu wa Chadema.

Lissu aliyeshambuliwa kwa risasi zaidi ya 30 na watu wasiojulikana Septemba 7, 2017 akiwa katika makazi yake mjini Dodoma ambapo alipelekwa Hospitali ya Rufaa ya Dodoma na usiku wa siku hiyo alihamishiwa Hospitali ya Nairobi alikolazwa hadi Januari 6 baada ya kahamishiwa Leaven, Ubelgiji kwa mazoezi ya viungo na saikolojia.

Mzee akilimali amkingia kifua Chirwa


Ibrahim Akilimali.

MWENYEKITI wa Baraza la Wazee wa Yanga, Ibrahim Akilimali amemtetea mshambuliaji wa kimataifa wa Yanga, Mzambia, Obrey Chirwa kufuatia kukosa penalti katika mechi ya juzi dhidi ya URA ya Uganda kwenye Kombe la Mapin­duzi.

Yanga iliondolewa katika nusu fainali kwa penalti 5-4 ambapo Chirwa alikosa kwa upande wa Yanga na kusaba­bisha kuwa gumzo kutokana na tukio hilo.


Mshambuliaji wa kimataifa wa Yanga, Mzambia, Obrey Chirwa.

Akizungumza na Championi Ijumaa, Akilimali alisema Chirwa hakufan­ya makosa katika kupiga penalti ya mwisho kwani alidhamiria kufunga na kilichotokea ni bahati mbaya na kudai kuwa, kocha ndiye anayepaswa kulaumiwa kutokana na kumtumia licha ya kutokuwa na ma­zoezi ya pamoja na wenzake.

“Yanga tumetolewa kiume katika michuano ya Mapinduzi kwani hadi tunatoka tumefanikiwa kufanya vyema hadi dakika 90 lakini kili­chotokea hakipaswi kulaumiwa mchezaji.

“Timu ilicheza vizuri ilipamba­na na hatimaye kuweza kufikia hapo tulipofikia na ilikuwa ni lazima timu moja isonge mbele.

“Siwezi kumlaumu Chirwa, kilichotokea ni bahati mbaya kwani, hata wachezaji wa­zuri Ulaya wanakosa penalti sembuse yeye, anayepaswa kulaumiwa ni kocha kwanini amemchezesha mchezaji akiwa hana mazoezi, naona anayarudia yaleyale ya Kocha Hans Pluijm,” alisema Akilimali.


Ronaldo amfungukia Neymar




Mshambuliaji wa zamani wa Barcelona Ronaldo Luís Nazário de Lima, amesema uhamisho wa nyota wa sasa wa Brazil Neymar Jr kutoka Barcelona kwenda PSG ni kama amepiga hatua moja nyuma.

Ronaldo ameyasema hayo kwenye mahojiano na chaneli ya 'Youtube' ya mchezaji wa zamani wa Brazil Arthur Antunes Coimbra maarufu kama Zico, alipoulizwa juu ya hatua alizopiga Neymar baada ya kuondoka Barcelona.

"Kwangu mimi uamzi huo ni kama kapiga hatua kurudi nyuma, lakini kila mtu huwa anatafuta changamoto mpya kama ilivyokuwa kwangu nilipoondoka Barcelona wakati huo nikajiunga na Inter Milan lakini ligi ya Italia ilikuwa na ushindani zaidi kuliko ilivyosasa ligi ya Ufaransa'', amesema Ronaldo.

Neymar aliondoka Barcelona kwenye majira ya kiangazi 2017 na kuhamia Paris Saint-Germain ya Ufaransa kwa dau la rekodi ya dunia € 222, zaidi ya shilingi bilioni 600. Neymar ameshaifungia PSG jumla ya mabao 20 katika michuano yote msimu huu ikiwemo 11 katika ligi kuu ya Ufaransa Ligue 1.

Hatua hii ya Ronaldo imekuja ikiwa ni siku mbili tu tangu Neymar mwenye miaka 25 aachwe kwenye kikosi cha UEFA mwaka 2017, huku nyota wawili Lionel Messi na Cristiano Ronaldo wakijumuishwa.