Monday 29 January 2018

Kumbe Ngassa bado anaidai Mbeya City



Kiungo mshambuliaji wa Ndanda FC, Mrisho Ngassa, amesema kuwa amechoka usumbufu wa kuidai klabu yake ya zamani, Mbeya City, mshahara wake wa miezi minne, lakini akasisitiza anaomba fedha zake.

Ngassa alijiunga na Ndanda hivi karibuni katika usajili wa dirisha dogo akitokea Mbeya mara baada ya mkataba wake kumalizika kabla ya kugoma kumuongezea mwingine.

Ngassa alisema kuwa anaidai klabu hiyo shilingi milioni 4.8 alizotakiwa alipwe tangu Desemba, mwaka jana.

Ngassa alisema amefikia hatua ya kuweka wazi madai hayo baada ya hivi karibuni viongozi wa timu hiyo kumwambia watampatia fedha hizo baada ya kulipwa fedha kutoka Azam TV ambao wanadhamini klabu za ligi kuu.

“Nimechoka kuongopewa na viongozi wa Mbeya City, kwani kila wakati nikiwapigia simu kudai malipo yangu ya mshahara ambayo ni shilingi milioni 4.8 wamekuwa hawapokei simu.

“Lakini hata wakipokea wakati mwingine wananipiga Kiswahili, kwa maana ya kunitajia siku nyingine na hivi karibuni walinipa maneno mazuri ya kuwa watanilipa fedha zangu baada ya wao kulipwa na Azam TV.

“Ninajua tayari wamepatiwa fedha hizo, lakini wamejikausha kunilipa fedha hizo ambazo ninadai hadi leo (jana Jumapili), hivyo nimechoshwa nao, naomba wanilipe fedha zangu,” alisema Ngassa aliyewahi kuzichezea Simba, Yanga na Azam FC.


Alipotafutwa jana mchana, Katibu Mkuu wa Mbeya City, Emmanuel Kimbe, alisema hayupo katika nafasi nzuri kuzungumzia suala hilo.

No comments:

Post a Comment