Wednesday 31 January 2018

Wadau wajadili changamoto ya wataalamu wa dawa za usingizi


Upungufu wa wataalamu wa dawa za usingizi nchini umepelekea Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (Muhas) kuanza kufikiria kutoa mafunzo ya uuguzaji wa dawa hizo kwa ngazi ya shahada.

Hatua hiyo ya Muhas kuanza kutoa mafunzo hayo imetokana na upungufu wa madaktari wenye utaalamu huo hasa wakati wa huduma ya upasuaji kuwa mdogo ambapo kwa sasa waliopo ni asilimia 1.2.

Hiyo maana yake ni kwamba katika idadi ya madaktari 2000 ambao wanahitajika kutoa huduma hiyo Tanzania inayo madaktari 30 pekee.

Kufuatia changamoto hiyo leo wadau mbalimbali wa afya na elimu walikutana na kujadili mtaala utakaotumika kufundishia chuoni hapo kabla ya kuupeleka kwa Tume ya Vyuo Vikuu Nchini (TCU).

" Ni kweli kumekuwepo kwa changamoto hiyo ya watalaamu wa dawa hizo lakini sasa mpango huu ukikamilika maana yake tutaongeza idadi ya madaktari kamili maana hawa waliopo wengi ni wale ambao wamesoma kozi kwa mwaka mmoja au miwili.

" Mafunzo yakianza kutolewa hapa chuoni Muhimbili wataweza kuchukua wanafunzi 200, Bugando 50 na KCMC 50 jambo ambalo litaongeza idadi kubwa ya watalaamu ili kuweza kufikia lengo letu la kuwa na wataalamu 2000 nchi nzima," Alisema Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Mpoki Ulisubisya.

No comments:

Post a Comment