Wednesday 29 November 2017

Mchakato wa hisa za Simba kuanikwa



JAJI MSTAAFU WA MAHAKAMA KUU, THOMAS MIHAYO

MWENYEKITI wa Kamati ya Zabuni ya Klabu ya Simba, Jaji mstaafu wa Mahakama Kuu, Thomas Mihayo, amesema kamati yake imepanga kuweka wazi kila kitu juu ya mchakato wa kutoa zabuni ya kununua hisa  za klabu hiyo.

Akizungumza jana, Mihayo alisema kuwa kamati yake bado haijamaliza mchakato huo, lakini wataweka wazi walipofikia na nini kinaendelea.

Alisema hayo yote watayaweka wazi kwenye mkutano mkuu wa dhararu wa wanachama wa klabu hiyo ulioitishwa na uongozi huku ukitarajiwa kufanyika Desemba 3, mwaka huu.

“Naomba niweke wazi, hatuendi kwenye mkutano kutaja mshindi kwa sababu kazi bado haijamalizika, ila kumekuwa na minong'ono na presha ya kujua nini kinaendelea, kwenye huu mkutano ambao sisi tumewaomba viongozi wauitishe, tutaweka wazi kila kitu,” alisema Jaji Mihayo.

Alisema kamati yake itaeleza kila kitu bila kuficha na kutaja ni watu wangapi wamejitokeza kuomba kununua hisa za klabu hiyo.

Simba ipo kwenye mchakato wa kufanya mabadiliko ya uendeshaji wa klabu hiyo ambapo wanataka kuendeshwa kwa hisa.

Mmoja wa wanachama wanaotajwa kutaka kununua hisa hizo asilimia 50 ni mfanyabiashara na mdau wa soka wa siku nyingi, Mohamed ‘Mo’ Dewji.

No comments:

Post a Comment