Thursday 30 November 2017

Majibu ya DNA yapotea katika mazingira ya kutatanisha



Hai. Familia ya binti wa kidato cha pili anayedaiwa kubakwa na kupewa ujauzito mwaka jana na mzee wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania(KKKT)  Kanda ya Usharika wa Nkuu Kiserenyi, wamemuomba mwanasheria mkuu wa Serikali kuingilia kati baada ya majibu ya vinasaba (DNA) kupotea katika mazingira ya kutatanisha.

Mzee huyo aliukana ujauzito huo, hali iliyosababisha hakimu mkazi wilaya ya Hai, Anold Kerekiano anayeisikiliza kesi hiyo kuamuru mtoto afanyiwe vipimo vya DNA ili kujua ukweli.

Hata hivyo, baada ya kufanyiwa vipimo majibu yalichukua mwaka mmoja na yalipotoka hayakuonekana.

Inaelezwa majibu hayo yalitolewa Juni 13, lakini hayakuwafikia wahusika hali ambayo inaitia shaka familia hiyo kuwa huenda yamechukuliwa.

Binti huyo anadai kuwa, baba huyo tangu mtoto azaliwe hajawahi kumpa matunzo mtoto wake.

Alisema anaishi maisha magumu kutokana na familia yake kuwa duni, hivyo anashinda mtoni na mtoto wake kupondaponda mawe ili kupata fedha ya kumnunulia mwanae maziwa.

Naye mama mzazi wa binti huyo, Martha Kweka aliiomba Serkali kuingilia kati suala hilo kutokana na binti yake kuishi kwa shida na ndoto zake zimeharibika.

Martha alisema binti yake ni mtoto wake wa kwanza na alikuwa akimtegemea kwa asilimia kubwa, ili baada ya kumaliza masomo angemsaidia kutokana na maisha duni wanayoishi.

Baba mzazi wa binti huyo, Kulasauko Nyuki alisema anashangaa unyama aliofanya mzee huyo na kuachiliwa wakati  watoto wake wanaendelea kusoma.

“Hii si sawa naomba sheria ifuate mkondo wake mimi nashindwa kuvumilia kuona mtuhumiwa anadunda na kutamba kuwa, hatuwezi kumfanya kitu chochote maana familia yangu ni maskini, naumia sana,” alisema Nyuki.

Hata hivyo, ofisa ustawi wa jamii wa Hai, Helga Njuyui alikiri majibu ya DNA kutumwa Juni  13, lakini inashangaza hayajawafikia.

No comments:

Post a Comment