Thursday 2 November 2017

Watu 34 wahukumiwa kunyongwa



Watu 34 wamehukumiwa kunyongwa hadi kufa baada ya kukutwa na hatia ya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi, (Albino), ambapo matukio 67 ya ukatili dhidi ya albino yakiwa yameripotiwa.

Takwimu hizo zimetolewa katika muendelezo wa mkakati wa kitaifa wa kupiga vita ukatili, mauaji na unyanyasaji dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi ambapo Wakili kutoka Ofisi Mkurugenzi wa Mashtaka, Beatrice Isembo, amesema, pamoja na adhabu za vifo, watuhumiwa 17 wamehukumiwa vifungo tofauti huku kesi nyingine zikiendelea.

"Tumegundua mikoa ya kanda ya Ziwa ndiyo iliyoongoza kwa matukio ya aina hii  na yote ni kutokana na imani za kishiriki kama kutaka utajiri kwenye uvuvi, mazao nk." Mwanza inaongoza kwa kuwa na kesi za aina hii 15, na jumla ya matukio 67 yameripotiwa katika kipindi cha miaka 11" amesema Bi. Isembo.

Kwa upande wake, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Ralph Meela, kutoka Makao Makuu ya jeshi la polisi Idara ya Upelelezi kitengo cha makosa dhidi ya binadamu na usalama barabarani, amesema, asilimia kubwa ya mauaji hayo yanatokana na imani za kishirikina hasa maeneo ya migodini na uvuvi pembezoni mwa ziwa Victoria.

No comments:

Post a Comment