Tuesday 31 October 2017

Sababu za kukamatwa Zitto hizi hapa



JESHI la Polisi linaendelea kumshikiria Kiongozi wa chama cha ACT-Wazalendo na Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe kwa mahojiano kwa kosa ya kutoa kauli za uchochezi katika mkutano wa hadhara alioufanya Kata ya Kijichi, Temeke,

Zitto alikamatwa mapema leo asubuhi nyumbani kwake na kupelekwa katika kituo cha polisi cha Chang’ombe kwa mahojiano kwa makosa hayo ambayo anadaiwa kufanya katika mkutano wa uzinduzi wa kampeni za udiwani wa kata ya Kijichi.

Kwa mujibu wa viongozi wa ACT-Wazalendo, Zitto anahojiwa kwa kutoa maneno yanayoweza kupelekea uvunjifu wa amani kwa wananchi na kujenga chuki kwa serikali yao.

Maneno hayo yaliyopelekea Zitto kushikiliwa na kuhojiwa ni pamoja na kusema: “Wananchi wasiichague CCM kwa sababu Serikali yake imeshindwa kufanya uchunguzi na kuwakamata watu waliompiga risasi Mbunge Tundu Lissu mpaka siku hiyo.”

Zitto pia anadaiwa kusema: “Wananchi wasiichague CCM kwa sababu Serikali yake imeshindwa kueleza chanzo cha miili ya watu wanaookotwa kwenye fukwe za bahari kama Coco Beach. Hivyo kuichagua CCM ni sawa na kuwaunga mkono waliofanya vitendo vya kumshambulia Tundu Lissu na wanaoua watu wanaookotwa kwenye fukwe.”

Timu ya mawakili wa chama cha ACT-Wazalendo na ndugu na jamaa wa Zitto wapo pamoja naye katika mahojiano hayo na wataendelea kutoa taarifa kila kinachoendelea

No comments:

Post a Comment