Thursday 25 January 2018

TAKUKURU yaeleza haya baada ya kukamilisha upelelezi kesi ya Malinzi


 Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imeieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa upelelezi wa kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili aliyekuwa Rais wa (TFF), Jamal Malinzi na wenzake umekamilika.

Mbali ya Malinzi, wengine ni Katibu wa TFF, Mwesigwa Selestine na Mhasibu wa shirikisho hilo, Msiande Mwanga.

Wakili wa TAKUKURU, Leornad Swai amemueleza Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba kuwa kesi hiyo imeitishwa kwa ajili ya kutajwa, pia jalada la kesi hiyo wameshalifanyia kazi ambapo upelelezi wamekamilisha.

Swai amedai kuwa jalada la kesi hiyo watalirudisha kwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kama alivyowaagiza walirudishe kwake ili alikague tena baada ya upelelezi wao kukamilika.

Baada ya kueleza hayo, Hakimu Simba ameahirisha kesi hiyo hadi February 8,2018 kwa ajili ya kutajwa.

Washtakiwa kwa pamoja wanakabiliwa na mashtaka 28, ikiwemo ya utakatishaji fedha ambazo ni Dola za Marekani, 375,418 na washtakiwa wote wamerudishwa rumande.

No comments:

Post a Comment