Monday, 29 January 2018

Kumbe Ngassa bado anaidai Mbeya City



Kiungo mshambuliaji wa Ndanda FC, Mrisho Ngassa, amesema kuwa amechoka usumbufu wa kuidai klabu yake ya zamani, Mbeya City, mshahara wake wa miezi minne, lakini akasisitiza anaomba fedha zake.

Ngassa alijiunga na Ndanda hivi karibuni katika usajili wa dirisha dogo akitokea Mbeya mara baada ya mkataba wake kumalizika kabla ya kugoma kumuongezea mwingine.

Ngassa alisema kuwa anaidai klabu hiyo shilingi milioni 4.8 alizotakiwa alipwe tangu Desemba, mwaka jana.

Ngassa alisema amefikia hatua ya kuweka wazi madai hayo baada ya hivi karibuni viongozi wa timu hiyo kumwambia watampatia fedha hizo baada ya kulipwa fedha kutoka Azam TV ambao wanadhamini klabu za ligi kuu.

“Nimechoka kuongopewa na viongozi wa Mbeya City, kwani kila wakati nikiwapigia simu kudai malipo yangu ya mshahara ambayo ni shilingi milioni 4.8 wamekuwa hawapokei simu.

“Lakini hata wakipokea wakati mwingine wananipiga Kiswahili, kwa maana ya kunitajia siku nyingine na hivi karibuni walinipa maneno mazuri ya kuwa watanilipa fedha zangu baada ya wao kulipwa na Azam TV.

“Ninajua tayari wamepatiwa fedha hizo, lakini wamejikausha kunilipa fedha hizo ambazo ninadai hadi leo (jana Jumapili), hivyo nimechoshwa nao, naomba wanilipe fedha zangu,” alisema Ngassa aliyewahi kuzichezea Simba, Yanga na Azam FC.


Alipotafutwa jana mchana, Katibu Mkuu wa Mbeya City, Emmanuel Kimbe, alisema hayupo katika nafasi nzuri kuzungumzia suala hilo.

Kampeni za Kinondoni CHADEMA, CCM wazidi kutifuana


Wagombea ubunge jimbo la Kinondoni, Maulid Mtulia (CCM) na Salum Mwalimu (Chadema) wameendelea kujinadi katika mikutano ya kampeni, huku Mtulia akiwashangaa wanaobeza kujiondoa kwake CUF na kujiunga na chama tawala.

Wakati Mtulia akimwaga sera leo Jumatatu Januari 29, 2018 katika uwanja wa Hananasif Kinondoni, Mwalimu alikuwa uwanja wa Mtambani kata ya Mzimuni.

Tangu kuanza kwa kampeni hizo, hoja ya hamahama ya madiwani na wabunge imekuwa ikitawala kutokana na CCM kujikita kuzungumzia sababu za mgombea wake wa Kinondoni, Mtulia kuteuliwa kuwania tena nafasi hiyo, huku Chadema wakitumia kete hiyo kumnadi Mwalimu.

 “Nyalandu (Lazaro-aliyekuwa mbunge Singida Kaskazini) na Godwin Mollel (Siha) nao walihama vyama vyao lakini mimi ndiye nazungumzwa sana na kusema kila chama kimepoteza mbunge wake lakini kuna chama kimeumia kuliko vingine,” amesema na Mtulia.

Amesema, “Wakati nikiwa upinzani sikuwa na namba ya Rais, sasa ninayo mkiwa na matatizo mnaniambia mimi nampigia na mambo yanatekelezwa. Kama kawaida yake yuko kwa ajili ya kuwaletea maendeleo wananchi wote bila ubaguzi.”

Kama ilivyo kwa Mtulia, Dk Mollel naye alikuwa mbunge wa Chadema jimbo la Siha lakini Desemba 14,2017 alihamia CCM na kupitishwa kuwania ubunge huku Nyalandu ambaye alikuwa mbunge kwa tiketi ya CCM, alihamia Chadema.

Akizungumza katika kampeni hizo Mtulia amesema, “Nitakuwa mbunge wa chama dola na ninakwenda kutekeleza ilani ya uchaguzi, mtu yeyote asijaribu kuzuia ilani hii kutekelezwa. Naomba kila mmoja awe mwakilishi wangu wa kuniombea kura. Ukichagua Mtulia umechagua maendeleo.”

Akiomba kura, Mwalimu alisema, “Naahidi kwenda kuwa mbunge wa kuwatumikia wananchi wote si Chadema tu. Siendi kuwa mbunge mnafiki, nitatumia talanta zote na ninaahidi makazi bora Kinondoni, kuna changamoto ya mafuriko.”

Mwalimu amesema, “Naahidi  tutatenga fedha kuondoa mafuriko. Kuna tatizo kubwa la afya, tuna kata nne tu zenye zahanati na kituo kimoja cha afya. Napaswa kusimamia afya. Naenda kusimamia, hakuna bodaboda wala mama ntilie atakayenyanyaswa.”

Sh 1.1 Tirilioni zatolewa kusaidia mapambano dhidi ya Malaria


Shirika la Global Fund limetoa ufadhili wa dola za Marekani 525 milioni sawa na Sh1.1 trilioni kwa Serikali ya Tanzania kwa ajili ya kusaidia mapambano dhidi ya malaria, kifua kikuu na Ukimwi kati ya mwaka 2018 na 2020.

Kati ya fedha hizo, Sh67 bilioni zimetengwa kwa ajili ya kifua kikuu zikihusisha elimu kwa wanajamii, vipimo na dawa  kwa watu ambao watabainika kuwa na ugonjwa huo.

Hatua hiyo inalenga kufikia dhamira ya Serikali ya kuwapa matibabu asilimia 70 ya wagonjwa wote wa kifua kikuu ifikapo mwaka 2020.

Kuhusu malaria Sh320 bilioni zimetengwa kwa ununuzi wa vyandarua, vipimo (mRDTs) na dawa za kutibu ugonjwa huo.

Kwa mapambano dhidi ya Ukimwi zimetengwa Sh769 bilioni kiasi ambacho Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amekitaja kuwa ni kikubwa kuwahi kutolewa na shirika hilo kwa ugonjwa huo.

Akizungumza leo Jumatatu Januari 29,2018 wakati wa utiaji saini makubaliano ya ufadhili huo, Ummy amesema Serikali inatambua na kuthamini kazi inayofanywa na wadau wa masuala ya afya.

Waziri Ummy amemhakikishia mwakilishi wa shirika hilo kuwa, Serikali itaongeza usimamizi katika fedha zinazotolewa na wafadhili kuhakikisha zinatumika kama ilivyokusudiwa.

“Rais mwenyewe ameniambia kuwa fedha hizi ni nyingi, hivyo tufanye kila linalowezekana kuhakikisha zinatumika kama ilivyoelekezwa, nami naahidi nitazifuatilia kuona zinafanya kazi iliyopangwa,” amesema.

Mwakilishi wa Global Fund nchini, Linden Morris amesema shirika hilo litaendelea kusaidia mapambano dhidi ya maradhi hayo.

Morris amesisitiza wasimamizi wa fedha hizo kuhakikisha zinafanya kazi iliyokusudiwa.
 

Pep Guardiola azidisha sifa EPL, sasa kumnasa Laporte


Mlinzi wa Athletico Bilbao, Aymeric Laporte akikabiliana ba Staa wa Barcelona Lionel Messi

Hizi sasa sifa! Ndivyo unavyoweza kusema baada ya klabu ya Manchester City kufikia makubaliano na klabu ya Athletic Bilbao kulipa kiasi cha £57m  takribani shilingi bilioni 158 kwaajili ya kukamilisha usajili wa mlinzi wa kati wa klabu hiyo Aymeric Laporte.

Kiasi hicho ambacho Man City inakilipa kwa Bilbao ni kwa ajili ya kuvunja mkataba wa mchezaji huyo (Buy Out Clause) na Pep Guardiola ameonekana kuhitaji huduma ya beki huyo ili kuimarisha safu yake ya ulinzi.

Ripoti nchini England zinasema kuwa Laporte raia wa Ufaransa mwenye miaka 23 huenda kesho akakamilisha vipimo na kusaini mkataba na vinara hao wa ligi kuu soka nchini humo.

Endapo Laporte atatua ndani ya Man City atakuwa ndiye mchezaji ghali zaidi akivunja rekodi ya usajili ya klabu hiyo inayoshikiliwa na kiungo Kevin de Bruyne ambaye alisajiliwa kwa dau la £55m mwaka 2015 akitokea VfL Wolfsburg ya Ujerumani.

Laporte huenda akaungana na walinzi wengine ghali duniani ambao ni John Stones na Kyle Walker waliosajiliwa ndani ya uongozi wa Pep Guardiola.


Baada ya vichapo Mbao FC kujiuliza kwa Kariakoo ya Lindi


Baada ya kuchezea vichapo viwili mfululizo katika Ligi Kuu kwa Mbao FC, sasa imepanga kufanya kweli katika mchezo wao wa kombe la FA dhidi ya Kariakoo Lindi utakaopigwa Jumatano hii.

Wababe hao wa vigogo wa Ligi Kuu Simba na Yanga, walichezea vipondo mechi zao mbili bila majibu,ambapo walianza kulizwa na Stand United bao 1-0 wakiwa nyumbani, kisha kuchapwa tena na Ruvu Shooting mabao 2-0 ugenini.

Nahodha kikosi hicho,Yusuph Ndikumana alisema wanawafuata Kariakoo kwa lengo moja tu kusaka ushindi ili kusonga mbele kwenye mashindano hayo.

Alisema makosa waliyoyafanya katika mechi zao za Ligi Kuu hawatarajii yajirudie na kwamba wanahitaji kutwaa ubingwa huo ambao waliukosa msimu uliopita.

“Tunaenda kwa lengo moja la kusaka ushindi ili kusonga mbele,ni mchezo mgumu na muhimu sana kwetu,makosa tuliyoyafanya hatutarajii kuyarudia kwenye FA”alisema Ndikumana.

Beki huyo aliongeza kuwa Kariakoo hawaijui kiundani, hivyo watakuwa makini kuzuia aina yoyote ya mashambulizi langoni mwao kuhakikisha hawapiti kirahisi ili kufikia malengo yao.

“Hatuwajui Kariakoo, kwahiyo tutakuwa na tahadhari sana nao kuwakabili, tunalenga sana kutwaa ubingwa msimu huu baada ya kuukosa msimu uliopita”alisema nahodha huyo Mrundi.

Mbao ilifanikiwa kufika fainali ya mashindano hayo katika msimu uliopita na kufungwa mabao 2-1 dhidi ya Simba, ambayo tayari imeshayaaga mashindano hayo.


Wakazi Wa Dar Wamiminika Ofisi za Mkuu Wa Mkoa Kujua Hatima Yao


Zaidi ya Wananchi  elfu tatu leo wamejitokeza ikiwa ni Siku ya kwanza ya Utatuzi wa Malalamiko ya Kisheria kwa Wananchi waliodhulumiwa chini ya Wanasheria Magwiji 160 ikiwa ni Mkakati wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda kusaidia wanyonge waliodhulumiwa Mali zao kupata haki pasipo kuvunja sheria.

Wananchi hao wametaabika kwa muda mrefu baada ya kudhulumiwa Mali zao Walizochuma kwa Tabu na sasa kupitia huduma ya Masada wa kisheria uliotangazwa na RC Makonda wanaamni watarejeshewa haki yao.
Makonda amesema idadi kubwa ya wananchi waliojitokeza leo inatoa picha kamili Kuwa wapo viongozi wasiotekeleza vyema majukumu yao ya kiofisi kwenye idara zao ambapo ameahidi kuwawajibisha.

Aidha  Makonda amesema kilichomgusa kuandaa Wiki ya msaada wa kisheria ni baada kubaini uwepo wa wananchi wanaonyanyasiki na hata kufikia hatua ya kufa kwa presha au kupooza miili baada ya kudhulumiwa na watu wenye pesa au wanaotumia uelewa wa sheria kukandamiza wanyonge.

Kutokana na idadi kuwa kubwa wanaoendelea kujitokeza Makonda anaongeza wanasheria wengi zaidi ili kuhakikisha Kila anaefika na kupata namba anahudumiwa ipasavyo ambapo amewaomba wanasheria kuhakikisha wanawasikiliza wananchi kwa umakini na kuchambua nyaraka kwa ufasaha na wasitoe hukumu.

Makonda amesema katika zoezi hili limehusisha Wanasheria wabobezi, Wataalamu wa kutambua nyaraka zilizogushiwa, watendaji wa Ardhi na watumishi wa Mahakama ambao wapo kwaajili ya kuwahudumia Wananchi.

Pia Makonda amesema baada ya kupokea ripoti kamili ya kesi zote atasimama kuhakikisha Hakuna mnyonge anabaki akinyanyasika.
Zoezi la kusikiliza wananchi waliodhulumiwa Mali zao ikiwemo Nyumba, Viwanja, Magari, Mirathi na Kazi litaendelea hadi siku ya Ijumaa ya February 2.

Nao wananchi waliojitokeza wamemshukuru  Makonda kwa kutambua Tabu wanazozipata baada ya kudhulumiwa na wajanja ambapo wengine wamesema wamepoteza Waume, Wake zao na wengine kupata magonjwa baada ya kudhulumiwa na wametaabika Muda mrefu kutafuta haki pasipo kufanikiwa lakini kupitia utendaji kazi makini wa  Makonda wanaamni haki inapatikana.


Saturday, 27 January 2018

Alichokisema Mr T kuhusu Darassa kuwa teja



Baada ya kimya cha muda mrefu kwa msanii Darassa ambaye mwaka juzi 2016 alitingisha sana na wimbo wake 'Muziki' kumeibuka tetesi kuwa msanii huyo naye amejiingiza katika matumizi ya dawa za kulevya, jambo ambalo limewashtua wengi. 

Kufuatia tetesi hizo mtangazaji wa kipindi cha Bongo fleva Top 20 ya East Africa Radio, Jr Junior alimvutia waya msanii huyo lakini bahati mbaya hakuweza kupokea simu yake jambo ambalo lilimfanya kumpigia simu mtu wake wa karibu ambaye ni producer wake Mr T Touchez ili kufahamu ukweli juu ya tuhuma au tetesi hizo. 

Baada ya Mr T Touchez kupigiwa simu alisema yeye hafahamu lolote juu ya jambo hilo na kukiri kuwa kwa sasa hajakutana na msanii huyo muda kidogo, hivyo hafahamu lolote kuhusu hicho kinachoelezwa kutumia dawa za kulevya. 


Kikosi cha Yanga VS Azam FC

                                            Kikosi cha Yanga kitakachovaana na Azam FC leo

Kabila ataja mwezi wa kufanyika uchaguzi DR Congo

Rais Joseph Kabila amepinga ukosoaji unaotekelezwa na jamii ya kimataifa kuhusu kucheleweshwa kwa uchaguzi katika jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Katika mkutano na wanahabari kuadhimisha miaka 17 madarakani, aliahidi kwamba uchaguzi huo utafanyika mwisho wa mwaka huu.

Kulingana na mwandishi wa BBC Alex Duval Smith mkutano huo na vyombo vya habari mjini Kinshasa ulikuwa wa kwanza katika kipindi cha miaka mitano.Na ulichukua saa tatu.

Aliikosoa Monusco akisema ujumbe huo wa Umoja wa Mataifa hauko nchini DRC ili kuendesha shughuli za taifa hilo.

Katika shutuma dhidi ya muungano wa Ulaya na Marekani, ambao wamekosoa makabiliano dhidi ya waandamanaji, alisema: DRC sio koloni .Taifa hili lazima liheshimiwe.

Alionekana akilikumbusha kanisa katoliki akisema kuwa maandamano yanayofanywa na wakristo dhidi ya serikali yake yanafaa kuruhusiwa lakini waandalizi ni lazima washtakiwe.

Serikali hiyo hivi majuzi ilitangaza kwamba uchaguzi utafanyika tarehe 23 Disemba, ikiwa ni miaka miwili baada ya kukamilika kwa muda wa utawala wa rais huyo.

Kampuni ya Mugabe yaingia kwenye matatizo

Kampuni moja ya rais wa zamani wa Zimbabwe Robert Mugabe inatakiwa kuondoka katika kipade kimoja cha ardhi kinachomilikiwa na shule moja la sivyo ishtakiwe.

Kampuni hiyo kwa Jina Gushungu Holdings inadaiwa kunyakuwa kipande hicho cha ardhi chenye ukubwa wa hekari 23 katika eneo moja la makaazi ya mji wa Harare.

Kanisa la Reform linasema kuwa ardhi hiyo inamilikiwa na kundi la shule zake la Eaglesvale.

Wakili wa shule hiyo Rodney Makausi aliambia BBC kwamba mwaka 2016 serikali ilichukua ardhi hiyo kwa nguvu.

Serikali baadaye ikaondoa madai yake baada ya swala hilo kuwasilishwa mahakamani.

Lakini mwenyekiti wa bodi ya shule hiyo Enos Chomutiri anasema kuwa mahindi yalipandwa katika shamba hilo mwaka uliopita na bango kubwa la shule hiyo likaondolewa.

Mawakili wametaka kampuni hiyo kuondoka katika shamba hilo mwisho wa mwezi huu ama ishtakiwe.

Sio mara ya kwanza familia ya Mugabe imetuhumiwa kuchukua mali kwa nguvu.

Awali, familia hiyo imekuwa na mgogoro na wakulima masikini kuhusu ardhi moja inayodaiwa kuwa na utajiri wa dhahabu ,pia familia hiyo imetuhumiwa kwa kunyakua shamba moja linalalozalisha ndimu zinazouzwa nje ya taifa katika eneo hilo hilo.

Bodi ya Ligi yaipiga rungu Mbeya City

Timu ya Mbeya City

Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania kupitia Mkurugenzi wa Ligi Boniface Wambura imetangaza kuipiga faini ya jumla ya shilingi milioni moja klabu ya Mbeya City kwa makosa mawili tofauti.

Wambura amebainisha hayo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam na kusema timu hiyo ilitenda kosa la kutumia mlango usio rasmi kuingilia uwanjani katika mechi iliyofanyika Januari 1,2018 Jijini Mbeya ambapo kitendo hicho ni kosa kwa mujibu wa kanuni za ligi kuu na kutozwa laki 5 kama adhabu yao.

Aidha, Wambura alisema Kamati iliiagiza Sekretarieti ya Bodi ya Ligi kutoa waraka kwa wamiliki wa viwanja kuhakikisha timu zote zinaingia uwanjani kwa kutumia milango rasmi nasio vinginevyo.

Mbali na hilo, Wambura amesema Klabu hiyo pia imepigwa faini ya laki 5 kutokana na mashabiki wake kuingia uwanjani na kumzonga mwamuzi kwa madai alikataa kutoa 'penalti' kwa timu hiyo.

Kwa upande mwingine, Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania kupitia Mkurugenzi wa Ligi Boniface Wambura imetangaza kumfungia kocha wa timu hiyo Ramadhani Mwazurimo mechi mbili na kupigwa faini ya laki 5 kutokana na kutoa lugha ya kashfa katika mechi ya Tanzania Prisons dhidi ya Mbeya City iliyochezwa Januari 14, 2018 kwenye uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Lowassa amnadi Salum Mwalimu Kinondoni

Waziri Mkuu Mstaafu na Mjumbe wa Kamati Kuu wa Chama cha Demokrasia na  Maendeleo CHADEMA, Edward Lowassa jioni leo amemnadi Mgombea wa Ubunge wa Kinondoni kupitia chama hicho, Salumu Mwalimu huku akiwataka wakazi wa Kinondoni kuacha kumuongelea mgombea wa CCM, Maulid Mtulia maana amekuwa msaliti kwao.

Lowassa alitumia wakati huo pia kuwashukuru wananchi wa Kinondoni kwa kumpigia kura wakati wa uchaguzi mkuu uliopita, na kuwaomba zile kura walizompigia 2015 basi wazielekeze kwa Mwalimu ambaye anaamini ni msomi mwenye kuweza kuwatetea wakazi wa Kinondoni.

" Msiogope vijana wa Kinondoni wenzetu wamekuwa wajanja wakilinda kura zao sasa na sisi kama ambavyo wazungumzaji wengine wamesema basi tunaomba mlinde kura zetu ikiwezekana tulale katika vituo vya kupigia kura kuhakikisha hatuibiwi.

Nae Waziri Mkuu Mstaafu wa awamu ya tatu, Fredrick Sumaye alisem, " Hakikisheni mnamchagua Mwalimu huyu ndie mtu safi wa kuhakikisha analeta maendeleo katika jimbo lenu,"

Kwa upande wake Mwalimu ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, alisema " Achaneni na wao wanaosema mimi sio mkazi wa hapa nachoomba ni kura zenu ambazo zitanifanya nikawatetee kuwajengea shule, kuhakikisha ajira kwa vijana,"

Kampeni za chama hicho zitaendelea kesho katika eneo la Kigogo jijiji Dar es Salaam ambapo zitaongozwa na Mwenyekiti wa Chama hicho, Freeman Mbowe.

Taliban watumia 'ambulance' iliojaa vilipuzi kuwaua watu 95 Afghanistan

Mlipuaji wa kujitolea mhanga amewaua takriban watu 95 na kuwajeruhi wengine 158 katika mji mkuu wa wa Afghanistan Kabul, kulingana na maafisa.

Washambuliaji waliendesha ambyulensi iliokuwa imejaa vilipuzi kupitia kizuiazi cha polisi hadi katika barabara ambayo ilikuwa imetengewa wafanyikazi wa serikali.

Kisa hicho kilitokea katika jumba la wizara ya maswala ya ndani na afisi ya Muungano wa Ulaya na baraza kuu la amani.

Kundi la wapiganaji wa Taliban linasema kuwa walitekeleza shambulio hilo ambalo ni baya zaidi katika kipindi cha mwezi mmoja.

Walioshuhudia wanasema eneo hilo ambalo lina majumba ya balozi nyingi pamoja na makao makuu ya polisi mjini humo, lilikuwa na watu wengi wakati bomu hilo lilipolipuka siku ya Jumamosi .

Maafisa wanasema kuwa idadi ya waliofariki inaendelea kuongezeka huku majeruhi wakipelekwa hospitalini kwa matibabu.
Shirika la kimataifa la msalaba mwekundi limesema kuwa utumizi wa 'ambulence' unakera.Wiki moja iliopita ,wapiganaji wa Taliban waliwaua watu 22 katika hoteli moja ya kifarahari mjini Kabul.

Hili ndilo shambulizi baya zaidi kuwahi kufanyika mjini Kabul katika kipindi cha miezi kadhaa.

Mnamo mwezi Oktoba, watu 176 waliuawa katika shambulio la bomu mjini Afghanistan katika kipindi cha wiki moja.

Vikosi vya maafisa wa usalama vya Afghanistan vimeshambiliwa pakubwa na wapiganaji wa Taliban ambao wanataka kuweka sheria ya kiislamu katika taifa hilo.

Mnamo mwezi Mei, takriban watu 150 waliuawa na mpiganaji wa kujitolea mhanga mjini Kabul.

Kundi la wapiganaji wa Taliban walikana kutekeleza shambulio hilo lakini serikali ya Afghanistan inasema kuwa kundi la Haqqani ambalo ni mshirika wake lilitekeleza shambulio hilo kupitia usaidizi wa Pakistan.

Pakistan imekana kusaidia kundi lolote la wapiganaji linalotekeleza mashambulizi nchini Afghanistan .

Mwezi huu, Marekani ilikatiza usaidizi wake wa usalama kwa Pakistan, ikisema kuwa taifa hilo limeshindwa kuchukua hatua dhidi ya makunni ya kigaidi katika ardhi yake.