Monday, 29 January 2018

Sh 1.1 Tirilioni zatolewa kusaidia mapambano dhidi ya Malaria


Shirika la Global Fund limetoa ufadhili wa dola za Marekani 525 milioni sawa na Sh1.1 trilioni kwa Serikali ya Tanzania kwa ajili ya kusaidia mapambano dhidi ya malaria, kifua kikuu na Ukimwi kati ya mwaka 2018 na 2020.

Kati ya fedha hizo, Sh67 bilioni zimetengwa kwa ajili ya kifua kikuu zikihusisha elimu kwa wanajamii, vipimo na dawa  kwa watu ambao watabainika kuwa na ugonjwa huo.

Hatua hiyo inalenga kufikia dhamira ya Serikali ya kuwapa matibabu asilimia 70 ya wagonjwa wote wa kifua kikuu ifikapo mwaka 2020.

Kuhusu malaria Sh320 bilioni zimetengwa kwa ununuzi wa vyandarua, vipimo (mRDTs) na dawa za kutibu ugonjwa huo.

Kwa mapambano dhidi ya Ukimwi zimetengwa Sh769 bilioni kiasi ambacho Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amekitaja kuwa ni kikubwa kuwahi kutolewa na shirika hilo kwa ugonjwa huo.

Akizungumza leo Jumatatu Januari 29,2018 wakati wa utiaji saini makubaliano ya ufadhili huo, Ummy amesema Serikali inatambua na kuthamini kazi inayofanywa na wadau wa masuala ya afya.

Waziri Ummy amemhakikishia mwakilishi wa shirika hilo kuwa, Serikali itaongeza usimamizi katika fedha zinazotolewa na wafadhili kuhakikisha zinatumika kama ilivyokusudiwa.

“Rais mwenyewe ameniambia kuwa fedha hizi ni nyingi, hivyo tufanye kila linalowezekana kuhakikisha zinatumika kama ilivyoelekezwa, nami naahidi nitazifuatilia kuona zinafanya kazi iliyopangwa,” amesema.

Mwakilishi wa Global Fund nchini, Linden Morris amesema shirika hilo litaendelea kusaidia mapambano dhidi ya maradhi hayo.

Morris amesisitiza wasimamizi wa fedha hizo kuhakikisha zinafanya kazi iliyokusudiwa.
 

Pep Guardiola azidisha sifa EPL, sasa kumnasa Laporte


Mlinzi wa Athletico Bilbao, Aymeric Laporte akikabiliana ba Staa wa Barcelona Lionel Messi

Hizi sasa sifa! Ndivyo unavyoweza kusema baada ya klabu ya Manchester City kufikia makubaliano na klabu ya Athletic Bilbao kulipa kiasi cha £57m  takribani shilingi bilioni 158 kwaajili ya kukamilisha usajili wa mlinzi wa kati wa klabu hiyo Aymeric Laporte.

Kiasi hicho ambacho Man City inakilipa kwa Bilbao ni kwa ajili ya kuvunja mkataba wa mchezaji huyo (Buy Out Clause) na Pep Guardiola ameonekana kuhitaji huduma ya beki huyo ili kuimarisha safu yake ya ulinzi.

Ripoti nchini England zinasema kuwa Laporte raia wa Ufaransa mwenye miaka 23 huenda kesho akakamilisha vipimo na kusaini mkataba na vinara hao wa ligi kuu soka nchini humo.

Endapo Laporte atatua ndani ya Man City atakuwa ndiye mchezaji ghali zaidi akivunja rekodi ya usajili ya klabu hiyo inayoshikiliwa na kiungo Kevin de Bruyne ambaye alisajiliwa kwa dau la £55m mwaka 2015 akitokea VfL Wolfsburg ya Ujerumani.

Laporte huenda akaungana na walinzi wengine ghali duniani ambao ni John Stones na Kyle Walker waliosajiliwa ndani ya uongozi wa Pep Guardiola.


Baada ya vichapo Mbao FC kujiuliza kwa Kariakoo ya Lindi


Baada ya kuchezea vichapo viwili mfululizo katika Ligi Kuu kwa Mbao FC, sasa imepanga kufanya kweli katika mchezo wao wa kombe la FA dhidi ya Kariakoo Lindi utakaopigwa Jumatano hii.

Wababe hao wa vigogo wa Ligi Kuu Simba na Yanga, walichezea vipondo mechi zao mbili bila majibu,ambapo walianza kulizwa na Stand United bao 1-0 wakiwa nyumbani, kisha kuchapwa tena na Ruvu Shooting mabao 2-0 ugenini.

Nahodha kikosi hicho,Yusuph Ndikumana alisema wanawafuata Kariakoo kwa lengo moja tu kusaka ushindi ili kusonga mbele kwenye mashindano hayo.

Alisema makosa waliyoyafanya katika mechi zao za Ligi Kuu hawatarajii yajirudie na kwamba wanahitaji kutwaa ubingwa huo ambao waliukosa msimu uliopita.

“Tunaenda kwa lengo moja la kusaka ushindi ili kusonga mbele,ni mchezo mgumu na muhimu sana kwetu,makosa tuliyoyafanya hatutarajii kuyarudia kwenye FA”alisema Ndikumana.

Beki huyo aliongeza kuwa Kariakoo hawaijui kiundani, hivyo watakuwa makini kuzuia aina yoyote ya mashambulizi langoni mwao kuhakikisha hawapiti kirahisi ili kufikia malengo yao.

“Hatuwajui Kariakoo, kwahiyo tutakuwa na tahadhari sana nao kuwakabili, tunalenga sana kutwaa ubingwa msimu huu baada ya kuukosa msimu uliopita”alisema nahodha huyo Mrundi.

Mbao ilifanikiwa kufika fainali ya mashindano hayo katika msimu uliopita na kufungwa mabao 2-1 dhidi ya Simba, ambayo tayari imeshayaaga mashindano hayo.


Wakazi Wa Dar Wamiminika Ofisi za Mkuu Wa Mkoa Kujua Hatima Yao


Zaidi ya Wananchi  elfu tatu leo wamejitokeza ikiwa ni Siku ya kwanza ya Utatuzi wa Malalamiko ya Kisheria kwa Wananchi waliodhulumiwa chini ya Wanasheria Magwiji 160 ikiwa ni Mkakati wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda kusaidia wanyonge waliodhulumiwa Mali zao kupata haki pasipo kuvunja sheria.

Wananchi hao wametaabika kwa muda mrefu baada ya kudhulumiwa Mali zao Walizochuma kwa Tabu na sasa kupitia huduma ya Masada wa kisheria uliotangazwa na RC Makonda wanaamni watarejeshewa haki yao.
Makonda amesema idadi kubwa ya wananchi waliojitokeza leo inatoa picha kamili Kuwa wapo viongozi wasiotekeleza vyema majukumu yao ya kiofisi kwenye idara zao ambapo ameahidi kuwawajibisha.

Aidha  Makonda amesema kilichomgusa kuandaa Wiki ya msaada wa kisheria ni baada kubaini uwepo wa wananchi wanaonyanyasiki na hata kufikia hatua ya kufa kwa presha au kupooza miili baada ya kudhulumiwa na watu wenye pesa au wanaotumia uelewa wa sheria kukandamiza wanyonge.

Kutokana na idadi kuwa kubwa wanaoendelea kujitokeza Makonda anaongeza wanasheria wengi zaidi ili kuhakikisha Kila anaefika na kupata namba anahudumiwa ipasavyo ambapo amewaomba wanasheria kuhakikisha wanawasikiliza wananchi kwa umakini na kuchambua nyaraka kwa ufasaha na wasitoe hukumu.

Makonda amesema katika zoezi hili limehusisha Wanasheria wabobezi, Wataalamu wa kutambua nyaraka zilizogushiwa, watendaji wa Ardhi na watumishi wa Mahakama ambao wapo kwaajili ya kuwahudumia Wananchi.

Pia Makonda amesema baada ya kupokea ripoti kamili ya kesi zote atasimama kuhakikisha Hakuna mnyonge anabaki akinyanyasika.
Zoezi la kusikiliza wananchi waliodhulumiwa Mali zao ikiwemo Nyumba, Viwanja, Magari, Mirathi na Kazi litaendelea hadi siku ya Ijumaa ya February 2.

Nao wananchi waliojitokeza wamemshukuru  Makonda kwa kutambua Tabu wanazozipata baada ya kudhulumiwa na wajanja ambapo wengine wamesema wamepoteza Waume, Wake zao na wengine kupata magonjwa baada ya kudhulumiwa na wametaabika Muda mrefu kutafuta haki pasipo kufanikiwa lakini kupitia utendaji kazi makini wa  Makonda wanaamni haki inapatikana.


Saturday, 27 January 2018

Alichokisema Mr T kuhusu Darassa kuwa teja



Baada ya kimya cha muda mrefu kwa msanii Darassa ambaye mwaka juzi 2016 alitingisha sana na wimbo wake 'Muziki' kumeibuka tetesi kuwa msanii huyo naye amejiingiza katika matumizi ya dawa za kulevya, jambo ambalo limewashtua wengi. 

Kufuatia tetesi hizo mtangazaji wa kipindi cha Bongo fleva Top 20 ya East Africa Radio, Jr Junior alimvutia waya msanii huyo lakini bahati mbaya hakuweza kupokea simu yake jambo ambalo lilimfanya kumpigia simu mtu wake wa karibu ambaye ni producer wake Mr T Touchez ili kufahamu ukweli juu ya tuhuma au tetesi hizo. 

Baada ya Mr T Touchez kupigiwa simu alisema yeye hafahamu lolote juu ya jambo hilo na kukiri kuwa kwa sasa hajakutana na msanii huyo muda kidogo, hivyo hafahamu lolote kuhusu hicho kinachoelezwa kutumia dawa za kulevya. 


Kikosi cha Yanga VS Azam FC

                                            Kikosi cha Yanga kitakachovaana na Azam FC leo

Kabila ataja mwezi wa kufanyika uchaguzi DR Congo

Rais Joseph Kabila amepinga ukosoaji unaotekelezwa na jamii ya kimataifa kuhusu kucheleweshwa kwa uchaguzi katika jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Katika mkutano na wanahabari kuadhimisha miaka 17 madarakani, aliahidi kwamba uchaguzi huo utafanyika mwisho wa mwaka huu.

Kulingana na mwandishi wa BBC Alex Duval Smith mkutano huo na vyombo vya habari mjini Kinshasa ulikuwa wa kwanza katika kipindi cha miaka mitano.Na ulichukua saa tatu.

Aliikosoa Monusco akisema ujumbe huo wa Umoja wa Mataifa hauko nchini DRC ili kuendesha shughuli za taifa hilo.

Katika shutuma dhidi ya muungano wa Ulaya na Marekani, ambao wamekosoa makabiliano dhidi ya waandamanaji, alisema: DRC sio koloni .Taifa hili lazima liheshimiwe.

Alionekana akilikumbusha kanisa katoliki akisema kuwa maandamano yanayofanywa na wakristo dhidi ya serikali yake yanafaa kuruhusiwa lakini waandalizi ni lazima washtakiwe.

Serikali hiyo hivi majuzi ilitangaza kwamba uchaguzi utafanyika tarehe 23 Disemba, ikiwa ni miaka miwili baada ya kukamilika kwa muda wa utawala wa rais huyo.

Kampuni ya Mugabe yaingia kwenye matatizo

Kampuni moja ya rais wa zamani wa Zimbabwe Robert Mugabe inatakiwa kuondoka katika kipade kimoja cha ardhi kinachomilikiwa na shule moja la sivyo ishtakiwe.

Kampuni hiyo kwa Jina Gushungu Holdings inadaiwa kunyakuwa kipande hicho cha ardhi chenye ukubwa wa hekari 23 katika eneo moja la makaazi ya mji wa Harare.

Kanisa la Reform linasema kuwa ardhi hiyo inamilikiwa na kundi la shule zake la Eaglesvale.

Wakili wa shule hiyo Rodney Makausi aliambia BBC kwamba mwaka 2016 serikali ilichukua ardhi hiyo kwa nguvu.

Serikali baadaye ikaondoa madai yake baada ya swala hilo kuwasilishwa mahakamani.

Lakini mwenyekiti wa bodi ya shule hiyo Enos Chomutiri anasema kuwa mahindi yalipandwa katika shamba hilo mwaka uliopita na bango kubwa la shule hiyo likaondolewa.

Mawakili wametaka kampuni hiyo kuondoka katika shamba hilo mwisho wa mwezi huu ama ishtakiwe.

Sio mara ya kwanza familia ya Mugabe imetuhumiwa kuchukua mali kwa nguvu.

Awali, familia hiyo imekuwa na mgogoro na wakulima masikini kuhusu ardhi moja inayodaiwa kuwa na utajiri wa dhahabu ,pia familia hiyo imetuhumiwa kwa kunyakua shamba moja linalalozalisha ndimu zinazouzwa nje ya taifa katika eneo hilo hilo.

Bodi ya Ligi yaipiga rungu Mbeya City

Timu ya Mbeya City

Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania kupitia Mkurugenzi wa Ligi Boniface Wambura imetangaza kuipiga faini ya jumla ya shilingi milioni moja klabu ya Mbeya City kwa makosa mawili tofauti.

Wambura amebainisha hayo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam na kusema timu hiyo ilitenda kosa la kutumia mlango usio rasmi kuingilia uwanjani katika mechi iliyofanyika Januari 1,2018 Jijini Mbeya ambapo kitendo hicho ni kosa kwa mujibu wa kanuni za ligi kuu na kutozwa laki 5 kama adhabu yao.

Aidha, Wambura alisema Kamati iliiagiza Sekretarieti ya Bodi ya Ligi kutoa waraka kwa wamiliki wa viwanja kuhakikisha timu zote zinaingia uwanjani kwa kutumia milango rasmi nasio vinginevyo.

Mbali na hilo, Wambura amesema Klabu hiyo pia imepigwa faini ya laki 5 kutokana na mashabiki wake kuingia uwanjani na kumzonga mwamuzi kwa madai alikataa kutoa 'penalti' kwa timu hiyo.

Kwa upande mwingine, Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania kupitia Mkurugenzi wa Ligi Boniface Wambura imetangaza kumfungia kocha wa timu hiyo Ramadhani Mwazurimo mechi mbili na kupigwa faini ya laki 5 kutokana na kutoa lugha ya kashfa katika mechi ya Tanzania Prisons dhidi ya Mbeya City iliyochezwa Januari 14, 2018 kwenye uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Lowassa amnadi Salum Mwalimu Kinondoni

Waziri Mkuu Mstaafu na Mjumbe wa Kamati Kuu wa Chama cha Demokrasia na  Maendeleo CHADEMA, Edward Lowassa jioni leo amemnadi Mgombea wa Ubunge wa Kinondoni kupitia chama hicho, Salumu Mwalimu huku akiwataka wakazi wa Kinondoni kuacha kumuongelea mgombea wa CCM, Maulid Mtulia maana amekuwa msaliti kwao.

Lowassa alitumia wakati huo pia kuwashukuru wananchi wa Kinondoni kwa kumpigia kura wakati wa uchaguzi mkuu uliopita, na kuwaomba zile kura walizompigia 2015 basi wazielekeze kwa Mwalimu ambaye anaamini ni msomi mwenye kuweza kuwatetea wakazi wa Kinondoni.

" Msiogope vijana wa Kinondoni wenzetu wamekuwa wajanja wakilinda kura zao sasa na sisi kama ambavyo wazungumzaji wengine wamesema basi tunaomba mlinde kura zetu ikiwezekana tulale katika vituo vya kupigia kura kuhakikisha hatuibiwi.

Nae Waziri Mkuu Mstaafu wa awamu ya tatu, Fredrick Sumaye alisem, " Hakikisheni mnamchagua Mwalimu huyu ndie mtu safi wa kuhakikisha analeta maendeleo katika jimbo lenu,"

Kwa upande wake Mwalimu ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, alisema " Achaneni na wao wanaosema mimi sio mkazi wa hapa nachoomba ni kura zenu ambazo zitanifanya nikawatetee kuwajengea shule, kuhakikisha ajira kwa vijana,"

Kampeni za chama hicho zitaendelea kesho katika eneo la Kigogo jijiji Dar es Salaam ambapo zitaongozwa na Mwenyekiti wa Chama hicho, Freeman Mbowe.

Taliban watumia 'ambulance' iliojaa vilipuzi kuwaua watu 95 Afghanistan

Mlipuaji wa kujitolea mhanga amewaua takriban watu 95 na kuwajeruhi wengine 158 katika mji mkuu wa wa Afghanistan Kabul, kulingana na maafisa.

Washambuliaji waliendesha ambyulensi iliokuwa imejaa vilipuzi kupitia kizuiazi cha polisi hadi katika barabara ambayo ilikuwa imetengewa wafanyikazi wa serikali.

Kisa hicho kilitokea katika jumba la wizara ya maswala ya ndani na afisi ya Muungano wa Ulaya na baraza kuu la amani.

Kundi la wapiganaji wa Taliban linasema kuwa walitekeleza shambulio hilo ambalo ni baya zaidi katika kipindi cha mwezi mmoja.

Walioshuhudia wanasema eneo hilo ambalo lina majumba ya balozi nyingi pamoja na makao makuu ya polisi mjini humo, lilikuwa na watu wengi wakati bomu hilo lilipolipuka siku ya Jumamosi .

Maafisa wanasema kuwa idadi ya waliofariki inaendelea kuongezeka huku majeruhi wakipelekwa hospitalini kwa matibabu.
Shirika la kimataifa la msalaba mwekundi limesema kuwa utumizi wa 'ambulence' unakera.Wiki moja iliopita ,wapiganaji wa Taliban waliwaua watu 22 katika hoteli moja ya kifarahari mjini Kabul.

Hili ndilo shambulizi baya zaidi kuwahi kufanyika mjini Kabul katika kipindi cha miezi kadhaa.

Mnamo mwezi Oktoba, watu 176 waliuawa katika shambulio la bomu mjini Afghanistan katika kipindi cha wiki moja.

Vikosi vya maafisa wa usalama vya Afghanistan vimeshambiliwa pakubwa na wapiganaji wa Taliban ambao wanataka kuweka sheria ya kiislamu katika taifa hilo.

Mnamo mwezi Mei, takriban watu 150 waliuawa na mpiganaji wa kujitolea mhanga mjini Kabul.

Kundi la wapiganaji wa Taliban walikana kutekeleza shambulio hilo lakini serikali ya Afghanistan inasema kuwa kundi la Haqqani ambalo ni mshirika wake lilitekeleza shambulio hilo kupitia usaidizi wa Pakistan.

Pakistan imekana kusaidia kundi lolote la wapiganaji linalotekeleza mashambulizi nchini Afghanistan .

Mwezi huu, Marekani ilikatiza usaidizi wake wa usalama kwa Pakistan, ikisema kuwa taifa hilo limeshindwa kuchukua hatua dhidi ya makunni ya kigaidi katika ardhi yake.


Matapeli wa Viwanja DSM kukiona

Serikali ya Mkoa wa Dsm Imetangaza rasmi vita dhidi ya Matapeli wa Viwanja na Nyumba ambao wamekuwa wakitumia mbinu mbali mbali ikiwemo ofisi za mawakili ,mahakama pamoja na Madalali kuwadhulumu wajane pamoja na watu wasiokuwa na Uwezo.

Mkuu wa Mkoa wa Dsm Paul makonda akizungumza na waandishi wa habari baada ya kwenda kwa familia ya Bi,Stella Bejumula pamoja Mume wake ambao ni watumishi wastaafu wa serikali ambao wametapeliwa nyumba kwa zaidi ya Miaka sita na kuishi maisha ya Kutangatanga na kutegemea Misaada ikiwemo chakula kutoka kwa watu mbali mbali..

Aidha Familia hiyo ya Bejumula ilitoa mtiririko mzima wa kadhia ya Kutapeliwa ambapo mwaka 2012 walikopa bank ya Crdb Mkopo na kufanikiwa kurejesha zaidi ya asilimia 80,na kubaki million ishirini ambayo alitokea Mtu mmoja kuwakopesha kwa riba lakini baadae akadaiwa kutengeneza Mkataba bandia wa mauzo kuwa familia hiyo imemuuzia kwa milion 96 Huku nyumba hiyo ikiuzwa kwa mtu mwingine katika kipindi cha siku 4 tu baada ya deni kulipwa.

Aidha Makonda alikwenda katika nyumba iliyopo kitalu B namba 91 ambayo ilikuwa ikimilikiwa na mzee na Bi,Bejumula na kutoa agizo la mmiliki aliyeuziwa eneo hilo kufika ktika ofisi za Mkuu wa Mkoa na nyaraka alizofanikisha kununua eneo hilo.

Makonda pia aliwakabidhi wazee hao wastaafu vyakula mbali mbali ikiwemo,Mchele,mafuta,unga, ngano na sukali huku akimtaka mfadhili anayewasaidia malazi aendelee kuwasaidia wakati akishughulikia suala hilo hali iliyozua simanzi eneo hilo …

Yanga SC yavunja rekodi ya Azam FC Chamazi

Mchezo wa ligi kuu soka Tanzania Bara baina ya mabingwa watetezi klabu ya Yanga dhidi ya Azam FC umemalizika katika uwanja wa Azam Complex Chamazi kwa mabingwa hao kushinda jumla ya mabao 2-0.

Kwa ushindi wa Yanga SC unaifanya timu hiyo kuvunja rekodi ya wana lamba lamba Azam FC ya kutokupoteza hata mchezo mmoja toka kuanza kwa ligi kuu soka Tanzania Bara msimu huu wa mwaka 2017/18.

Wafungaji katika mchezo alikuwa Shabani Chilunda wa Azam FC wakati kwa upande wa Yanga SC akiwa Obrey Chirwa na Gadiel Michael.

Kwa matokeo hayo inaifanya mabingwa watetezi Yanga SC kufikisha jumla ya pointi 28 wakiwa nafasi ya tatu, Azam FC ikisalia na alama zake 30 nafasi ya pili huku Simba SC ikiongo katika msimamo wa ligi kwa kuwa na pointi 32 na mchezo mmoja mkononi ambao unatarajiwa kupigwa hapo kesho siku ya Jumapili.

Katika michezo mingine iliyopigwa hii leo timu ya Mbeya City ikiwa nyumbani imekubali kutoka sare ya mabao 0 – 0 dhidi ya Mtibwa Sugar wakati Mwadui FC ikiwa nyumbani imelizimishwa sare ya magoli 2 – 2 na Njombe Mji wakati Kagera Sugar ikitoka suluhu ya bila kufungana dhidi ya Lipuli FC.