Saturday, 3 February 2018

Wanaofanya udanganyifu kwenye asasi za kiraia waonywa

Asasi za kiraia zimetakiwa kufuata taratibu kabla ya kutoa elimu ya ujasiriamali kwa wananchi ili kukwepa udanganyifu, ikiwa ni pamoja na kuwachangisha fedha na kutokomea kusikujulikana.

Kauli hiyo imetolewa leo Februari 3, 2018  na ofisa maendeleo ya jamii Manispaa ya Temeke, John Bwana wakati akizindua  mradi wa kuwajengea wanawake uwezo kuhusu ujasiriamali ili  kujiinua kiuchumi ulioandaliwa na asasi ya Iwapoa.

Amesema kuna lundo la asasi za kiraia zinazotoa mafunzo kiholela na kuwatapeli wanawake kwa kuwachangisha michango na kutokomea na fedha zao.

“Iwapoa mmefanya jambo la maana kufuata taratibu za kuonana na mamlaka husika na kupata wataalamu kutoka katika kata mtakazofanya kampeni hii ya kupunguza umasikini kwa kuwajengea wanawake uwezo,|” amesema na kuongeza,

“Nawaunga mkono na ninatoa rai kwa asasi nyingine zisizofuata utaratibu zifanye hivyo mara moja kwa sababu tunazifuatilia na tukizibaini tutazizuia kufanya kazi zake katika maeneo yetu.”

Mratibu wa  mradi huo kutoka Iwapoa,  Yusuph Kutegwa amesema mradi huo utatekelezwa katika kata sita za Manispaa ya Temeke.

Amezitaja kata hizo kuwa ni Buza, Keko, Chamazi, Vituka, Azimio na Charambe.

Amesema utawafikia wanawake 150 kutoka katika maeneo hayo waliyoyachagua kutokana na kuwa na wingi wa watu, wakiwamo wanawake wasiokuwa na shughuli za kudumu.

“Ili kuwapatia masoko na mitaji tutawaunganisha katika vikundi vya watu watano watano, ili iwe rahisi kuwapa ujuzi kwa pamoja, ”amesema Kutegwa.

Nduda, Mbonde njiani kurejea dimbani

Mlinda mlango namba mbili wa Simba, Said Mohammed 'Nduda' wiki ijayo anatarajia kujiunga na wenzake tayari kuanza mazoezi baada ya kuwa nje kwa miezi mitano, kufuatia kufanyiwa upasuaji wa goti Oktoba mwaka jana nchini India.

Nduda aliyesajiliwa na klabu ya  Simba Julai mwaka jana akitokea Mtibwa Sugar ya Morogoro, hajacheza mechi yoyote msimu huu kutokana na maumivu ya goti aliyoyapata Agosti mwaka jana mazoezini akiwa visiwani Zanzibar wakati Simba inajiandaa na mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya mahasimu wa jadi, Yanga Agosti 23, mwaka jana Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.

Kwa sasa mlinda mlango huyo ameanza programu za mazoezi yake binafsi tangu mwanzoni mwa mwaka huu, akijifua ufukweni kwa mazoezi.

Wakati huo huo, beki wa kati wa Simba, Salim Mbonde anaendelea na mazoezi ya gym baada ya kuwa nje kwa zaidi ya miezi mitatu kufuatia kuumia Oktoba 15, mwaka jana katika mchezo wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara dhidi ya timu yake ya zamani, Mtibwa Sugar uliomalizika kwa sare ya 1-1 mjini Dar es Salaam.

Kiongozi mwengine wa Upinzani akamatwa Kenya

Mbunge mwingine nchini Kenya, amekamatwa kuhusiana na mzozo unaozunguka kujiapisha kwa aliyekuwa waziri mkuu Raia Odinga kwa kile anachokitaja kama rais wa watu wa Kenya.

Mbunge wa Makadara jijini Nairobi George Aladwa alikamatwa asubuhi ya Jumamosi nyumbani kwake na maafisa wa idara ya upelelezi na kupelekwa hadi makao makuu ya idara hiyo kwa mahojiano zaidi.

Aladwa ambaye amewahi kuwa meya wa jiji la Nairobi, alikuwa katika mstari wa mbele katika mipango ya sherehe hizo ambayo haikuwa na idhini ya serikali.

Aladwa sasa ni mbunge wa pili kukamatwa kuhusiana na hafla hiyo ambayo pia imeshutumiwa na jamii ya kimataifa.

Mbunge mwingine wa Nairobi Tom Kajwang alikamatwa na kufikishwa mahakamani na hatimaye kuachiliwa kwa dhamana.

Mwanaharakati mwingine wa upinzani wakili Miguna miguna pia alikamatwa siku ya Ijumaa na angali anazuliwa na polisi licha ya mahakama kuruhusu kuachiliwa kwake kwa dhamana.

Bwana Aladwa alikamatwa siku ya Ijumaa usiku katika nyumba yake iliopo Buruburu kulingana na kiranja wa walio wachache bungeni Junet Mohamed.

Bwana Mohammed ambaye pia mbunge wa Suna Mashariki alisema kuwa bwana Aladwa kwa sasa anazuiliwa katika makao makuu ya ujasusi.

Polisi hawajatoa tamko lolote kuhusiana na kukamatwa kwa Aladwa

Msanii Radio azikwa kwao Uganda

Msanii Radio wa nchini Uganda ambaye alifariki Februari 1, amezikwa leo kijijini kwao Nakawuka nchini Uganda, na kuhdhuriwa na maelfu ya watu kutoka sehemu mbali mbali za nchi hiyo na wasanii wa nchi jirani.

Hapo jana Ijumaa ya Februari 2, wananchi wa Uganda na mashabiki wa muziki walipata fursa ya kufanya ibada ya mwisho ya kumuombea marehemu kanisani, na kisha baadaye mwili wake kupelekwa kwenye uwanja wa michezo wa Airstip, ambapo walikesha nao huku kukipigwa show ya nguvu kutoka kwa wasanii mbali mbali wa nchini Uganda.

Kabla ya mazishi hayo kuliibuka mvutano mkubwa wa nguo ya kuvalishwa marehemu, huku Lilian Mbabazi ambaye ni mama wa watoto wake wawili ambaye mwenyewe alimtambulisha kama mke wake akitaka marehemu azikwe na suti aliyovaa kwenye tamasha la 'Nakudata' ambayo ndio ngoma iliyompa umaarufu na kumfanya atoboe kwenye game, na mwanamke wake mzungu ambaye amezaa naye mtoto mmoja akisema marehemu alitaka akifa azikwe na nguo za jeshi kwani alipenda kuitwa mwanajeshi, na hatimaye akavalishwa gwanda za jeshi.

Asubuhi ya leo mwili huo ulipelekwa kijijni kwao Nakawuka na kuwekwa kwenye makazi yake ya milele, ambapo kwenye tukio hilo watu walionekana kuwa wengi na baadhi wakizimia.

Miongoni mwa wasanii waliohudhuria mazishi hayo ni msanii na mbunge Jaguar wa Kenya, wasanii mbali mbali wa Uganda na viongozi wa serikali.

Diwani Dar Aja Na Mpango Kunusuru Wananchi Wake



Diwani wa kata ya Salanga jijini Dar es salaam Harun Mdoe amekuwa na mpango mkakati wa mda mfupi na mrefu kuhusiana na barabara ambayo kwa sasa imekua kero kwa wananchi wa eneo hilo.

Mdoe amesema hayo leo alipotembelea barabara hiyo ambayo inaunganisha Matangini, Michungwani, King'ongo, Matosa, Kata ya Goba pia kuelekea Bagamoyo ambapo kwa mkakapi wa mda mfupi wamekuwa wakiweka vifusi ambavyo vinasaidia angalau kupitika kwa urahisi.

Kutokana na kero hiyo pia amewataka wananchi wanaoishi maeneo hayo kuacha mara moja tabia ya kumwaga maji barabarani ambayo yanasababisha uharibifu na wataoendelea kufanya hivyo watachukuliwa hatua za sheria.

Kwa upande wake mwenyekiti wa mtaa wa Michungwani Ismaili Kipungula amesema kuwa kuna shida kubwa katika barabara hiyo ambayo inaunganisha mitaa mitatu.

"hii barabara imekuwa ni tatizo kwamba imeoza na sio kuharibika tumejaribu kuhangaika kama mtaa tukishirikiana na wananchi pamoja  Diwani wetu kama mnavyoona hizi ni jitihada za wananchi wenyewe lakini barabara bado sio nzuri hivyo tunaiomba Serikali waiangalie hii barabara pia wenzetu wa Tarura ambao wamekubali kutengeza wafanya haraka kwani ilifika hatua tulika mawasiliano" amesema Kipungula

Aidha kwa upanda wake mkazi na mtumiaji wa barabara hiyo Upendo Mbise amesema kuwa kina mama wamekuwa wakijifungulia njiani kutokana na adha na ubovu ulipo mimi mwenyewe nikiwa kama shahidi juzi mama mmoja alijifungulia njiani hali ambayo ni hatari pia inaweza kupelekea hata kifo


Mkuu wa shule aingia matatani kwa kuchangisha michango



Sumbawanga. Mkuu wa mkoa wa Rukwa, Joachim Wangabo ameagiza mkuu wa shule ya sekondari Muhama manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa kuchukuliwa hatua kwa tuhuma za kuwatoza wanafunzi michango ya Sh5,000 kama gharama ya kuwapatiwa fomu za maelezo ya kujiunga na shule hiyo.

Wangabo ametoa agizo hilo jana Februari 2, 2018 wakati akizungumza katika mkutano wa hadhara kata ya Malangali baada ya baadhi ya wananchi kufichua jambo hilo.

Mmoja wa wananchi hao, Sadock Kalinga amesema wazazi wamekuwa wakichangishwa kiasi hicho cha fedha ili wapatiwe fomu hizo.

“Tulilazimika kutoa fedha hizi na kupewa stakabadhi kwa kuwa tuliambiwa mwanachi ambaye hatotoa fedha  hawezi kupewa fomu hizo na hivyo kukosa sifa ya kujiunga katika shule hii,” amesema Kalinga.

Baada ya kupokea malalamiko hayo na kuonyeshwa risiti iliyotolewa kama ushahidi, Wangabo amemhoji Mkurugenzi wa Halmashauri ya manispaa ya Sumbawanga, Hamidu Njovu kuhusu uhalali wa mchango huo ambapo naye alikana kufahamu jambo hilo.

Alimuagiza mkurugenzi huyo kumchukulia hatua mkuu huyo wa shule kwa kuwa kitendo alichokifanya si sahihi kwa sababu Serikali imepiga marufuku michango shuleni.

“Ni marufuku kwa mwalimu yeyote kujihusisha na michango katika mkoa huu. Walimu kazi yao ni kufundisha na sio kuchangisha. Nakuagiza mkurugenzi kuchukua hatua katika hili na ninataka nipate taarifa’,” amesema.

Mwananchi:

Tume yaundwa kufuatilia korosho zenye kokoto

Serikali mkoani Lindi imeunda timu ya kuchunguza matukio ya baadhi ya wakulima kuchanganya mchanga na korosho kwa nia ya kuongeza uzito wakati wa kupima kwenye mizani, ili hatua za kisheria zichukuliwe kwa watakaobainika kufanya hhujuma hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Lindi Bw. Godfrey Zambi amewaambia waandishi wa habari mjini Lindi kuwa, korosho iliyochanganywa na mchanga kugundulika kwenye ghala la Buko mjini humo na korosho nyingine iliyochanganywa na kokoto za lami iligundulika nchini Vietnam baada ya kusafirishwa kutoka Tanzania, ambapo mwenye korosho hizo alidai alizinunua wilayani Liwale mkoani humo.

Amesema baada ya kupata taarifa hizo zilizosambazwa kwenye mitandao ya kijamii na kuchafua taswira ya Tanzania kibiashara, imemlazimu kukutana na viongozi wa mkoa kujadili suala hilo na hatimaye kuunda timu ya uchunguzi wa matukio hayo ili hatua zichukuliwe haraka.

Pamoja na uchunguzi unaoendelea, Mkuu huyo wa Mkoa ameeleza kuwa baadhi ya viongozi wa Chama cha Ushirika cha Pangatena wilayani Lindi wanashikiliwa kwa uchunguzi na kusimamishwa kwa bodi ya chama hicho baada ya kubainika korosho walizofikisha kwenye ghala kuu la BUCCO zina viroba vya mchanganyiko wa korosho na mchangaTume

Rais Trump awasiliana na viongozi wa Japan na Korea Kusini

Rais wa Marekani Donald Trump amewapigia simu viongozi wa Japan na Korea Kusini siku chache kabla ya michezo ya Olimpiki kuanza nchini Korea Kusini.

Kwa mujibu wa habari,Trump amefanya mazungumzo na waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe.

Viongozi hao wawili wamezungumzia mfumo wa ulinzi wa makombora wa Japan na vilevile uhamisho wa ngome ya Marekani katika kisiwa cha Okinawa.

Japan na Korea Kusini zimekuwa zikijitahidi kuidhibiti Korea Kaskazini kutofanya majaribio ya makombora ya nyuklia.

Korea Kaskazini ilirusha kombora la nyuklia mnamo mwezi Novemba mwaka jana.

Watatu wafariki kutokana na baridi kali

Watu watatu waripotiwa kufariki  nchini Uswidi kutokana na baridi kali Kaskazini mwa Uswidi.

Baridi kali katika eneo hilo la Kaskzini mwa Uswidi ilifuatiwa na theluji kali ambapo nyuzi joto ilikuwa 20 chini ya sifuri.

Uongozi wa eneo la Vesternorrland nchini Uswidi umefahamisha kuwa bariki kali katika eneo hilo imesababisha vifo vya watu watatu.

Idara ya utabiri wa hali ya hewa nchini Uswidi imetoa tahadhari kwa raia  kutokana na kiwango kĊŸkubwa cha theluji ambacho kinatarajiwa katika za usoni.

Singida United yaipiga Mwadui FC 3-2

Singida United wameshinda kwa mabao 3-2 dhidi ya Mwadui FC katika mechi kali ya Ligi Kuu Bara kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida.

Wageni Mwadui walitangulia kwa mabao mawili kabla ya Singida kusawazisha na kufunga la ushindi.

Mechi hiyo ilikuwa ni ya kushambuliana kwa zamu ingawa Singida United walifanya mashambulizi mengi zaidi mwishoni.

Shuja wa Singida United alikuwa Kenny Ally Mwambungu ambaye alifunga bao kwa shuti kali ndani ya dakika 3 za nyongeza baada ya mwamuzi kuongeza dakika 5.


Shuti kali alilopiga na kumshinda kipa Massawe wa Mwadui ni baada ya kupokea pasi nzuri ya Mudathiri Yahya.

Mabao mawili ya Singida United ikisawazisha, yalifungwa na Salum Chuku na Deus Kaseke aliyeng'ara katika mchezo huo.

Vituo 46 vya kupigia kura kinondoni kuhamishwa

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imeridhia kuhamishwa kwa vituo 46 vya kupigia Kura katika kata tatu za jimbo la Kinondoni zitakazofanya Uchaguzi mdogo wa Ubunge Februari 17 mwaka huu.

Mkurugenzi wa Uchaguzi Bw. Ramadhani Kailima ameeleza kuwa uamuzi wa NEC kuridhia kuhamishwa kwa vituo hivyo, umetokana na makubaliano yaliyofikiwa katika Mkutano wa Msimamizi  wa Uchaguzi wa  jimbo la Kinondoni na Vyama vya siasa juu ya kuhamishwa kwa vituo hivyo vilivyokuwa kwenye nyumba za Ibada, Zahanati na maeneo ya majengo ya watu binafsi.

Amesema Tume imeridhika na uamuzi huo kwasababu hatua zilizochukuliwa ni sahihi kwa mujibu sheria na kanuni namba 21 ya Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura ambayo inaeleza kuwa ;  Vituo vya Kupigia Kura havitakiwi kuwekwa katika majengo ya nyumba za Ibada, kambi za jeshi, nyumba za watu binafsi na  ofisi za vyama vya siasa.

“ Tumejiridhisha kuwa baadhi ya vituo katika Kata ya  Kigogo vilikuwa katika nyumba za Ibada na vingine kuwa katika maeneo yenye ufinyu wa nafasi hivyo tumeridhia vituo hivyo vihamishwe na kupelekwa katika majengo ya umma” Amesema.

Amesema kuwa baadhi ya vituo vya kupigia Kura vilivyokuwa katika majengo ya umma ikiwemo Zahanati vimehamishwa katika shule za msingi za umma zilizo katika kata hizo  ili kuondoa usumbufu kwa wagonjwa.

Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi Kata ya Mwananyamala Bi. Barima Omari ameeleza kuwa kata ya Mwananyamala ina vituo vya kupigia kura 65 na wapiga kura 27,589 na kuongeza kuwa vituo nane (8) vilivyokuwa katika shule ya Sekondari Kambangwa mtaa wa msisiri A vimehamishwa. Kati ya hivyo 6 vimehamishiwa katika Ofisi ya Serikali ya Mtaa ya Msolomi na 2 kuhamishiwa uwanja wa kwakopa.

Naye Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi  Kata ya Kijitonyama Elizabeth Minga ameeleza kuwa Kata hiyo ina jumla ya vituo vya kupigia Kura 101, kati ya hivyo vituo 22 vimehamishwa.

Akifafanua kuhusu vituo hivyo amesema vituo 6 vilivyokuwa katika shule ya Sekondari Kenton vimehamia shule ya Msingi Mapambano na vituo 5 vilivyokuwa nje ya Ofisi ya serikali ya Mtaa wa Bwawani vimehamishiwa mbele ya ofisi hiyo.

Aidha, vituo 6  vilivyokuwa nje ya soko la Makumbusho vimehamia ndani ya Ofisi ya Meneja wa Soko hilo na vituo 5 vilivyokuwa  katika Ofisi ya Serikali za mitaa kijitonyama vimehamishiwa katika shule ya msingi kijitonyama.

Kwa upande wake Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi Kata ya Kigogo Bw. Singoro Mdegela ameeleza kuwa kata yake ina idadi ya Wapiga kura 27,000 na Vituo vya Kupigia Kura  59.

Amesema katika Kata hiyo vituo 16 vimehamishwa ambapo vituo 5 vilivyokuwa eneo la Kiwenge kwenye Msikiti wa Shiha vimehamia Uwanja wa People na Vituo 6 vilivyokuwa kwenye Zahanati ya Kigogo vimehamishiwa katika Shule ya Msingi Kigogo ili kuruhusu shughuli za matibabu kwa wagonjwa kuendelea.

Aidha, vituo 5 katika ofisi ya serikali ya mtaa wa Mkwajuni vimehamishiwa katika  shule ya secondari Kigogo.

Masoko ya mazao kuimarishwa

Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema Serikali inataka kuimarisha masoko ya mazao yanayolimwa nchini ili kuwawezesha wakulima kupata tija.

Taarifa iliyotolewa leo Februari 3, 2018  na ofisi ya Waziri Mkuu inaeleza kuwa ametoa kauli hiyo jana Januari 2, 2018 wakati akikagua Kampuni ya Soko la Bidhaa Tanzania (TMX), iliyoanzishwa kwa lengo la kuimarisha masoko.

Amesema kupitia Wizara ya Kilimo, Serikali imedhamiria kuimarisha masoko ya mazao yanayolimwa nchini ili kuwawezesha wakulima kujikwamua kiuchumi.

“Kupitia Wizara ya Kilimo tunataka kuimarisha masoko ya mazao yanayolimwa nchini. Wakati umefika kwa wakulima nchini kuona tija ya mazao wanayolima,” amesema.

Ametoa mfano zao la pamba ambalo wakulima walikuwa wanaingia mikataba na wanunuzi, mfumo ambao ulikuwa unawanyonya badala ya kuwanufaisha.

Awali, ofisa mtendaji mkuu wa TMX, Godfrey Malekano amemhakikishia Waziri Mkuu kuwa wamejipanga vyema kuanza minada ya mazao.

“Tutaanzia na zao la ufuta mwezi Mei, 2018 na kuendelea na mazao mengine kwa kadiri ya misimu ya mazao hayo ilivyo,” amesema.

Amesema kufanikiwa kwa soko la bidhaa na mfumo wa stakabadhi ghalani kunategemea msaada wa Serikali, “Soko la bidhaa la Ethiopia linalotajwa sana kwa mafanikio limefikia malengo yake kutokana na mkono wa Serikali.”

Tshishimbi apiga bao, Yanga ikiiua Lipuli 2-0


YANGA SC imejivuta kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya wenyeji, Lipuli Uwanja wa Samora mjini Iringa.

Ushindi huo unaifanya Yanga SC ifikishe pointi 31 baada ya kucheza mechi 16, ikipanda hadi nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu, sasa ikiwazidi kwa pointi Azam FC ambao wanacheza mechi yao ya 16 usiku dhidi ya Ndanda FC Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.

Yanga pia imepunguza pengo la pointi inazozidiwa na vinara, Simba SC hadi kubaki tano – lakini Wekundu wa Msimbazi nao watacheza mechi yao ya 16 kesho dhidi ya Ruvu Shooting Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Katika mchezo huo uliochezeshwa na refa Erick Onoka aliyesaidiwa na Geoffrey Kihwilio na Janeth Balama, Yanga ilipata bao moja kila kipindi.

Na mabao hayo yalikuja baada ya Yanga kupata pigo dakika ya 17 kufuatia kipa wake wa kwanza Mcameroon, Youthe Rostand kuumia na kushindwa kuendelea na mchezo nafasi yake ikichukuliwa na chipukizi, Ramadhan Awam Kabwili.

Kiungo kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Papy Kabamba Tshishimbi alifunga bao la kwanza dakika ya 19 kwa kichwa akimalizia mpira uliotemwa na kipa Agathon Anthony Mkwando baada ya kichwa cha kuparaza cha winga Emmanuel Martin kufuatia kona ya kiungo Pius Charles Buswita

Kipindi cha pili, Yanga ya kocha Mzambia, George Lwandamina ilirudi na mchezo mzuri na kufanikiwa kupata bao la pili lililofungwa na Buswita dakika ya 55, aliyempiga chenga kipa Mkwando baada ya pasi nzuri mshambuliaji Mzambia, Obrey Chirwa kutokea pembeni kulia na kufunga bao zuri.

Yanga ilijitahidi kuendelea kusaka mabao zaidi, lakini Lipuli walikuwa imara na kumaliza mchezo kwa kipigo cha mabao 2-0.

Lipuli FC; Agathon Mkwando, Stephen Mganga, Ally Mtoni, Martin Kazila, Joseph Owino, Novaty Lufunga, Seif Karihe/Tola Mangonela dk69, Mussa Nampaka/Zawadi Mawiya dk71, Adam Salamba, Malimi Busungu na Jamal Mnyate/Jerome Lembele dk78.

Yanga SC; Youthe Rostand/Ramadhani Kabwili dk17, Hassan Kessy, Gardiel Michael, Kelvin Yondan, Said Juma ‘Makapu’, Papy Kabamba Tshishimbi, Emmanuel Martin, Raphael Daudi/Raphael Daudi dk86, Obrey Chirwa, Pius Buswita na Geoffrey Mwashiuya/Maka Edward dk81.