Tuesday, 23 January 2018

Onyo alilotoa Jaji Mkuu kwa viongozi wa serikali na wanasiasa


Jaji Mkuu wa Tananzania, Profesa Ibrahimu Juma amewataka viongozi wa serikali na vyama vya siasa kuacha mara moja vitendo vya kuingilia mhimili wa Mahakama na kuvunja amri zake.

Jaji Profesa Juma ameyasema hayo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu wiki ya Sheria inayotarajiwa kufanyika mwanzoni mwa mwezi ujao (Februari mosi), siku ambayo ndio itakayoashiria kuanza rasmi kwa shughuli za Mahakama kwa mwaka huu 2018 yatakayofanyika katika viwanja vya Mahakama vilivyopo mtaa wa Chimala jijini Dar es Salaam, ambapo mgeni rasmi atakuwa Rais John Magufuli.

"Kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania mamlaka ya utoaji haki ni ya Mahakama tu, nawasihi viongozi wote wa serikali wenye mamlaka za kikatiba na kisheria wabaki ndani ya maeneo yao ya Kikatiba na wajiepushe kuingilia maeneo yaliyo ndani ya haki, hadhi na Mamlaka ya Kikatiba ya Mahakama", alisema Jaji Profesa Juma.

Kwa upande mwingine, Jaji Profesa Juma ametoa rai kwa wananchi na wadau wote wa sheria kutembelea Mnazi Mmoja kwa ajili ya kujifunza na kupata huduma mbalimbali za Kisheria kutoka kwa Majaji, Mahakimu, Wasajili, Watendaji, Mawakili wa serikali na Mawakili wanaojitegemea ambao watakuwa tayari kuwasikiliza na kuwahudumia ipasavyo.

Tanzia:Nguli wa muziki wa Jazz Afrika Kusini Hugh Masekela afariki dunia


Mwanamuziki maarufu nchini Afrika Kusini, Hugh Masekela anayefahamika kama baba wa muziki wa Jazz amefariki dunia baada ya kusumbuliwa kwa muda mrefu na maradhi ya saratani ya tezi dume.

Hugh Masekela amefariki dunia baada ya kusumbuliwa kwa muda mrefu na maradhi ya saratani ya tezi dume.

Kwa mujibu wa vyombo vya habari nchini Afrika Kusini.  Masekela amabaye hadi kifo chake kinamkuta alikuwa na umri wa miaka 78.

Katika kipindi chake cha zaidi ya miongo mitano kwenye fani hiyo ya muziki alijijengea umaarufu kimataifa kutokana na utunzi wa nyimbo zake za muziki  wa Jazz ukiwemo wimbo  uliotumika katika harakati za kupinga ubaguzi wa rangi nchini humo.

Hugh Masekela alitumbuiza katika hafla ya ufunguzi wa fainali za kombe la dunia za mwaka 2010 zilizofanyika nchini Afrika Kusini ikiwa ni mara ya kwanza fainali hizo kufanyika barani Afrika.

Rais Magufuli kuwa mgeni rasmi siku ya Sheria nchini



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Sheria itakayofanyika Februari Mosi mwaka huu.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam na waandishi wa habari, Jaji Mkuu wa Tanzania, Prof. Ibrahim Juma kuhusu maonyesho ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria nchini yenye maudhui ya ‘Matumizi ya TEHAMA katika utoaji haki kwa wakati na kwa kuzingatia maadili’.

“Kila mwaka Mahakama ya Tanzania huadhimisha Siku ya Sheria ambayo huashiria kuanza rasmi kwa shughuli za Mahakama, kwa mwaka huu maadhimisho hayo yatafunguliwa rasmi na Rais Magufuli katika viwanja vya Mahakama vilivyopo jijini Dar es Salaam,” amesema Jaji Mkuu Juma.

Jaji Mkuu amesema kuwa kabla ya kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Sheria, Mahakama ya Tanzania pamoja na wadau muhimu katika Sekta ya Sheria watatumia siku tano kuanzia tarehe 27 hadi 31 Januari mwaka huu kwa ajili ya kufanya maonyesho yatakayotoa elimu kwa wananchi watakaopata nafasi ya kuhudhuria katika viwanja vya Mnazi Mmoja vilivyopo jijini humo.

Maonyesho hayo yatatanguliwa na matembezi maalum ya kuadhimisha Wiki ya Sheria yatakayofanyika Januari, 28 mwaka huu ambayo yataongozwa na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete yatakayoanzia katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mpaka viwanja vya Mnazi Mmoja ambapo Rais Mstaafu Kikwete atazindua rasmi Wiki ya Sheria.

Aliongeza kuwa Wiki ya Sheria inatoa nafasi nzuri kwa wananchi kuzifahamu shughuli mbalimbali zinazofanywa na Mahakama pamoja na wadau wa sekta ya sheria ili kufanikisha maboresho endelevu ya Mahakama.

Wadau wengine watakaoshiriki katika wiki ya sharia pamoja na Tume ya Utumishi wa Mahakama, Mahakama ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka, Taasisi ya Mafunzo ya Uanansheria kwa Vitendo Tanzania, Tume ya Kurekebisha Sheria, Chama cha Mawakili Tanganyika Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Jeshi la Magereza, Jeshi la Polisi, na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali.

Watumishi wa serikali wapewa masaa 72

Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi Mkoani Songwe limetoa masaa 72 kwa watendaji 37 kutoka katika kata 15 wawe wamewasilisha kiasi cha milioni 73 walichokusanya kama mapato vinginevyo watachukuliwa hatua za kisheria.

Watendaji hao wanadaiwa kukusanya fedha hizo katika kipindi cha robo mwaka kwa mwaka wa fedha 2017/2018 na kubaki nazo majumbani mwao bila kuwasilisha kwa mweka hazina wa halmashauri.



Akisoma azimio la kikao cha Baraza hilo ambalo limekutana mjini Vwawa, Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Erick Ambakisye alisema uamuzi huo unafuatia kitendo cha watendaji hao kutowasilisha fedha za makusanyo katika kipindi kilichowekwa kisheria na kusababisha halmashauri kukosa mapato hayo ya Sh. 73,777,736.29 huku wakijua kufanya hivyo ni kosa.

Mwenyekiti huyo alisema sambamba na hilo baraza limechukua hatua ya kuwaonya kwa barua kwa mara ya pili watendaji wa kata 15 za Wasa, Magamba, Ipunga, Nyimbili, Myovizi, Itaka, Mlangali, Halungu, Isansa, Kilimampimbi, Nambinzo, Bara, Ruanda, Iyula na Shiwinga huku wengine 16 wakiwa wakishindwa kutumia mashine za kielektroniki katika kukusanya mapato ya halmashauri na kutakiwa kujieleza na kuwasilisha fedha walizokusanya ifikapo tarehe hiyo saa 4.00 asubuhi.

Aidha mwenyekiti huyo alisema ili kuongeza ufanisi katika ukusanyaji mapato halmashauri yake iliweka mkataba na watendaji hao wenye lengo kukusanya asilimia 50 ya lengo la makusanyo katika kipindi cha kila robo na kutoa zawadi ya Sh. 500000 kwa kata ya kwanza itakayokusanya vizuri, Sh. 300000 (kata ya pili) na Sh.200000 (kwa kata ya tatu) na kutoa ngao ya kufanya vibaya kwa kata tatu zilizofanya vibaya.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Mbozi John Palingo akizungumza wakati akitoa salamu za serikali alisema wilaya ina fursa ya vyanzo vingi vya mapato lakini watendaji wamekuwa hawakusanyi ipasavyo kutokana na kufanya kazi kwa mazoea.

Kwa upande mwingine Mbozi alisema hatua kali lazima zichukuliwe kwa watendaji wanaoshindwa kukusanya mapato na kwamba ofisi yake itasimama imara kusaidia katika kuhakikisha halmashauri inakusanya mapato inayostahili.

Atiwa mbaroni kwa kuiba jeneza


Kijana mmoja aliyetambulika kwa jina moja la Boniface mkazi wa Mwananyamala kwa Msisiri anashikiliwa na jeshi la Polisi Mkoa wa Kinondoni kwa kuiba masanduku ya kuzikia (majeneza) mawili na kuyaficha nyuma ya choo cha mkazi mwengine wa mtaa huo.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa Polisi mkoa wa Kinondoni Jumanne Muliro, amesema tukio hilo limetokea kati ya ofisi mbili za kuuza masanduku hayo ambapo moja ndiyo iliyoibiwa majeneza hayo, ambayo moja ni la mtu mzima na moja likiwa la mtoto mdogo

“Kuna work shop mbili ambazo zinajishusisha na kutengeneza masanduku, zipo kwenye sehemu moja, asubuhi mtu kaingia kwenye work shop yake akakuta masanduku mawili hayapo akaanza kufuatilia, baada ya muda akajua yapo kwenye workshop nyingine, kwa hiyo kilichofanyika ni ufuatiliaji na askari wakafanikiwa kuyapata, ni suala ambalo linachunguzwa kujua kama wanadaiana au ni wizi umefanyika, ndipo sheria ifuate”, amesema Kamanda Muliro.

Mmiliki wa masanduku hayo Bi. Judith Carlos amesema masanduku hayo aligundua yapo kwa jirani yake baada ya kumuahidi mtu atampa elfu 50 iwapo atamsaidia kujua nani kayachukua, na ndipo baadaye akaambiwa mahali yalipo.

ANC yaendelea kumjadili Jacob Zuma


 Chama tawala cha African National Congress kimethibitisha kwamba mazungumzo yanaendelea kuona namna Rais Jacob Zuma atakavyoondoka ofisini bila shaka ikiashiria mwanzo wa mwisho wa kashfa zilizodumu miaka tisa ya utawala wake.

Zuma amekuwa akikabiliwa na shinikizo la kumtaka ajiuzulu tangu alipoachia uaongozi wa ANC kwa makamu wake Cyril Ramaphosa.

 Kashfa

Halmashauri kuu “ilijadili suala hili...kutakuwa na majadiliano kati ya maofisa, Rais Zuma na kwa chama Ramaphosa," alisema Katibu Mkuu Ace Magashule.

"Hakuna muda uliowekwa...Hatufanyi kazi kwa mtindo huo, tunashikiana, tunajadili,” aliongeza Magashule kwamba hakuna uamuzi wa mwisho uliowekwa kuhusu kuondoka kwa Zuma.

Urais wa Zuma ulikumbwa na kashfa za rushwa na ulichafuliwa na kudorora kwa uchumi hali iliyochangia chama kukosa kuungwa mkono kuelekea uchaguzi mkuu mwaka 2019.

Wafuasi wa Ramaphosa wanafanya kampeni atawazwe sasa kama rais na ajaribu kufufua uchumi kabla ya uchaguzi mkuu ambao ANC inaweza kupoteza udhibiti wake kwa mara ya kwanza tangu ulipokomeshwa utawala wa ubaguzi wa rangi.

Audio | Nutty Neithan X Wyre X J’bryte X Ketchup X Gabiro – AYAWA Remix | Mp3 Download

Audio | Nutty Neithan X Wyre X J’bryte X Ketchup X Gabiro – AYAWA Remix | Mp3 Download

Audio | Nutty Neithan X Wyre X J’bryte X Ketchup X Gabiro – AYAWA Remix | Mp3 Download

DOWNLOAD Mp3

Mtoto amuua Mama yake kwa kumkata mapanga


KAMANDA WA POLISI MKOA WA GEITA, MPONJOLI LOTSON.

MJANE mkazi wa kijiji cha Kamhanga, wilaya na mkoa wa Geita amefariki dunia baada ya kukatwakatwa na panga kichwani na mwanaye usiku na kisha mtoto huyo kutoroka.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Mponjoli Lotson alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo, jana na kumtaja marehemu kuwa ni Kabula Karume (73).

Mtuhumiwa anayedaiwa kutoroka baada ya kutekeleza  ukatili huo ni Dotto Lukenze na chanzo cha mauaji hayo bado hakijajulikana na upelelezi unaendelea.

Kamanda Mponjoli alisema kuwa taarifa za awali za kikachero zinaonyesha mtuhumiwa ana rekodi ya kuwahi kutuhumiwa kwa mauaji katika matukio mengine na uhalifu mbalimbali.

Habari kutoka eneo la tukio zinadai kuwa kabla ya mauaji hayo, mtuhumiwa ambaye ni mtoto wa marehemu alikuwa akimshinikiza mama yake kuuza mali zikiwamo ng'ombe na mashamba, hatua ilikuwa ikipingwa na marehemu.

Mponjoli alisema siku ya mauaji Januari 16, mwaka huu saa tatu usiku marehemu alikuwa akiota moto na watoto wake wengine na ghafla ndipo mtuhumiwa alipotokea na kuanza kumshambulia.

Alisema katika kutekeleza mauaji hayo mtuhumiwa alitumia kitu chenye ncha kali kumkatakata kichwani marehemu huku waliokuwapo wakijaribu kupiga kelele za kuomba msaada bila mafanikio.

Watu hao ndiyo walimtambua mtuhumiwa kabla hajakimbia, alisema Mponjoli.

Chanjo saratani kutolewa bure


WIZARA ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesema kuanzia Aprili, mwaka huu, itaanza kutoa bure chanjo dhidi ya kirusi kinachosababisha saratani ya mlango wa kizazi (human papillon virus) kwa wasichana wa kuanzia umri wa miaka 14.

Hatua hiyo inatokana na takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) za mwaka 2012 kuonyesha kuwa Tanzania inaongoza kwa kuwa na  wagonjwa wapya wa saratani ya mlango wa kizazi 51 kwa kila wanawake 100,000 huku vifo vikiwa 38 kwa kila wanawake 100,000, ikilinganishwa na nchi nyingine za Afrika Mashariki. Naibu Waziri wa wizara hiyo Dk. Faustine Ndugulile, alisema hayo jana alipokuwa akizindua kampeni ya uchunguzi wa mabadiliko ya awali ya saratani hiyo na ya matiti, uliofanyika katika Hospitali ya Rufani ya Mkoa wa Dodoma.

 Alisema hatua hiyo ya chanjo inalenga kukinga kirusi kinachoeneza saratani ya mlango wa kizazi ambayo Tanzania inaongoza kwa ukanda wa nchi za Afrika Mashariki kwa kuwa na wagonjwa wengi.

Aidha, alisema katika awamu ya kwanza ya utoaji wa chanjo hiyo mwaka huu wamepanga kuwafikia wasichana wa kuanzia miaka 14 wapatao 616,734. "Hawa 616,734 ndio tumepanga kuwapatia chanjo mwaka huu na katika mwaka ujao tutawafikia wasichana wa kuanzia miaka tisa hadi 14 na mwaka utakaofuata tutawapa chanjo wale wenye umri wa kuanzia miaka tisa," alisema Dk. Ndugulile. Alisema chanjo hiyo itasaidia kuwalinda wasichana ambao wako katika mazingira hatarishi ya kuambukizwa virusi vinavyosababisha saratani ya matiti na mlango wa kizazi. "Saratani ya mlango wa kizazi moja ya sababu ambazo zinachangia ni wasichana kushiriki ngono katika umri mdogo, kuwa na wenza wengi lakini pia kubeba mimba nyingi kunaweza kusababisha mtu kupata maambukizi," alisema.

Hata hivyo, aliwataka kinamama kupima afya zao mara kwa mara na wanapobainika kuwa na maambukizi, wanatakiwa kuwaona wataalamu ili kupatiwa matibabu. "Saratani hii inatibika kabisa kama mtu atapata vipimo vya afya yake kila mara, lakini watu wengi wamekuwa wakija katika hospitali wakiwa wamechelewa sana hali ambayo saratani inakuwa imesambaa katika maeneo mengine ya mwili kama vile mifupa, ini na damu na kuwa vigumu kutibika,"alisema  Dk. Ndugulile aliwaagiza wakuu wa mikoa wote kuhakikisha kuwa wasimamia upimaji wa saratani ya mlango wa kizazi katika mikoa yao ili kufikia malengo ya serikali iliyojipangia hadi kufikia mwishoni mwa mwaka huu iwe imefikia kimama milioni tatu.

Aliongeza pamoja na juhudi hizo pia serikali kwa sasa inaboresha Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI) ambayo ni taasisi pekee nchini katika kukabiliana na tatizo la saratani, kwa kuweka vifaa vya kisasa ambavyo vitasaidia kutoa huduma za matibabu ambazo zilikuwa zinatolewa nje ya nchi.

 "Katika mwaka 2016 Taasisi ya Saratani ya Ocean Road ilipokea wanawake 1,934 wa saratani ya mlango wa kizazi. Takwimu hizi zimekuwa zikongezeka si tu kwamba kujua ukubwa wa tatizo na hii itatusaidia kuona jinsi gani jamii imeamka na kuhamasika kufahamu athari za saratani na kuanza kuchukua hatua," alisema.

Wawili wafariki dunia, wanane wajeruhiwa ajali ya Mabas


WATU wawili wamefariki dunia papo hapo na wengine wanane kujeruhiwa vibaya katika ajali ya mabasi mawili yakugongana uso kwa uso katika kijiji cha Kamanga, Sengerema mkoani Mwanza saa nne asubuhi jana.

Akizungumzia ajali hiyo, shuhuda aliyekuwa katika pikipiki na kunusurika kugongwa na mabasi hayo, Philipo Budeba, alisema chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa mabasi yote mawili.

“Mimi nilikuwa naendesha pikipiki, mbele yangu kulikuwa na basi la Mkombozi Trans lenye namba T540 DLF na nyuma kulikuwa na Basi la Walawi Express  lenye namba T167 CSN yote yalikuwa na mwendokasi," alisema Budeba.

"Dereva wa Mkombozi ndiye aliyetaka kupita gari lingine, lakini ilishindikana na kusababisha magari hayo kuvaana... mimi nilijirusha kwenye kilima cha pembeni mwa barabara."

Naye abiria wa Mkombozi Trans iliyokuwa ikitokea Kanyara Buchosa, Sengerema, Fransisco Kansola alisema tabia ya madereva kushindwa kuchukua tahadhari na kujali kuwahi abiria ndiyo chanzo cha ajali hiyo.

Walawi Express lilikuwa likitoka Mwanza kwenda Nemba wilayani Biharamulo.

Akithibitisha kutokea kwa ajali hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi alisema dereva wa basi la Walawi, Frank Kimboka ni miongoni mwa majeruhi wanane wa ajali hiyo baada ya kujeruhiwa miguu yote.

“Waliofariki ni dereva wa basi la Mkombozi Trans aliyefahamika kwa jina la Simon Mdalesalamu na mwanamke aliyekadiriwa kuwa na umri wa miaka 18 hadi 20," alisema Kamanda Msangi.

Majeruhi watatu wametajwa kuwa ni Frank Mushi aliyevunjika miguu yote miwili, Isaack Hamisi (22) mkazi wa Nyasaka wilayani Ilemela na Mwinyi Ismail (50) aliyevunjika miguu yote miwili, alisema Kamanda Msangi.

"Chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa mabasi hayo.”

Aidha, ajali hiyo ilitokea wakati mkoa wa Mwanza ukizindua maadhimisho ya wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani, yenye kaulimbiu inayosema ‘Zuia ajali, tii sheria, okoa maisha'.

Majeruhi walikimbizwa katika Hospitali ya Rufani ya Bugando jijini Mwanza kwa ajili ya matibabu.

Neno la Buswita kwa mashabiki wa Yanga


BAADA ya kufunga bao pekee lililowapa ushindi Yanga dhidi ya Ruvu Shooting juzi, kiungo Pius Buswita, amewapa neno la faraja mashabiki wa timu hiyo kwa kuwaeleza "sasa tunarudi kwenye kasi yetu".

Buswita, alisema mashabiki wa timu hiyo hawapaswi kuwa na wasiwasi kwa nafasi ya tatu wanayoshika kwenye msimamo wa ligi.

“Mashabiki wasiwe na hofu, taratibu tunarudi kwenye kasi yetu na tunaweza kufanya vizuri zaidi, lengo letu ni kuhakikisha tunashinda katika kila mchezo bila kuangalia matokeo ya wengine,” alisema Buswita.

Aidha, alisema kuwa timu hiyo bado ina nafasi ya kutetea ubingwa wao, jambo ambalo mashabiki wanapaswa kuwa na matumaini hayo.

“Ukiangalia hakuna tofauti kubwa ya pointi na timu inayoongoza ligi, tutaendelea kupambana kuhakikisha tunatetea ubingwa wetu,” alisema Buswita.

Kiungo huyo wa zamani wa Mbao FC, juzi alifunga bao pekee wakati Yanga wakiibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Ruvu Shooting, ushindi huo umeifanya Yanga inayodhaminiwa na Kampuni ya Kubashiri Matokeo Michezoni ya SportPesa, kukusanya pointi 25 huku Azam wakiwa na pointi 30 wakifuatiwa na Simba wenye pointi 29 (kabla ya mchezo wake wa jana dhidi ya Kagera Sugar)

“Sio mimi niliesema CCM imeoza”: Ridhiwan Kikwete akanusha


Mbunge wa Chalinze kupitia Chama cha Mpainduzi (CCM), Ridhiwani Kikwete amekanusha ujumbe unaosambazwa katika mitandao ya kijamii ukidai kuwa amekikosoa chama hicho kutokana na kutoridhishwa na mwenendo wake.

Akizungumza jana jioni, Ridhiwani amewataka watanzania na wanachama wa CCM kupuuza taarifa hiyo kwani siyo yeye ameitoa na badala yake ni watu wenye lengo lakukiharibu chama hicho.

Amesema kwamba, kwa siku nzima ya jana hajaandika ujumbe wowote na kwamba alikuwa jimbo kwake katika vikao vya halmashauri wakipanga mipango ya bajeti kwa ajili ya maendeleo ya jimbo hilo.


DC aingia matatani kwa kupiga kampeni


Mgombea ubunge Jimbo la Kinondoni (CUF), Rajab Salum Juma akihutubia katika mkutano wa kampeni uliofanyika kwenye Uwanja wa Ally Mapilau, Mwananyamala jijini Dar es Salaam.

Kitendo cha Mkuu wa Wilaya ya Siha, Onesmo Buswelu kupanda jukwaani kumnadi mgombea wa CCM katika Jimbo la Siha, Dk Godwin Mollel kimechafua hali ya hewa baada ya kupingwa na vyama vya siasa huku Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ikisema hakufanya jambo sahihi.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Ramadhani Kailima ameliambia Mwananchi jana kuwa ili Buswelu aweze kuchukuliwa hatua, wenye jukumu la kumshtaki ni vyama vinavyopinga jambo alilolifanya.

Alisema vyama hivyo vinatakiwa kumshtaki katika kamati ya maadili inayoundwa na wajumbe wa vyama vinavyoshiriki uchaguzi katika jimbo husika na kwamba jambo hilo linapaswa kufanyika ndani ya saa 72, tangu apande jukwaani.

Wakati DC huyo akiibua kizazaa hicho, CCM imeendelea kumnadi Dk Mollel huku katika Jimbo la Kinondoni, wagombea ubunge wa CCM, Chadema na Sau wakiwekewa pingamizi.

Uchaguzi wa Siha na Kinondoni utafanyika Februari 17 na unavishirikisha vyama 12, huku ukitajwa kuwa ni mpambano mkali baina ya CCM na Chadema inayoungwa mkono na vyama vitano vya Ukawa ambavyo ni NLD, NCCR-Mageuzi, CUF upande wa Maalim Seif Sharif Hamad na Chaumma iliyojiunga hivi karibuni.

Uchaguzi huo unafanyika baada ya waliokuwa wabunge; Mollel (Siha- Chadema) na Maulid Mtulia (Kinondoni-CUF) kujivua uanachama wa vyama hivyo kwa maelezo kuwa wanamuunga mkono Rais John Magufuli na baadaye kujiunga CCM.

Chama hicho tawala kimewapitisha wawili hao kutetea majimbo hayo, huku Chadema ikimsimamisha naibu katibu mkuu (Zanzibar), Salum Mwalimu (Kinondoni) na Elvis Mosi (Siha).

Buswelu ‘alivyochafua hewa’

Juzi katika uzinduzi wa kampeni za Dk Mollel katika viwanja vya KKKT Karansi Jimbo la Siha, Buswelu alisema Serikali haijaribiwi hivyo ni vyema kila mmoja akahakikisha anadumisha amani na kufanya siasa za kistaarabu katika kipindi chote cha kampeni.

Alisema Dk Mollel ameleta heshima kwa wananchi wa Siha huku akiwataka wananchi wote kumuunga mkono na kuhakikisha anapata ushindi wa kishindo.

NEC ilivyomruka Buswelu

Akizungumza na Mwananchi, Kailima alikiri kitendo alichokifanya mkuu huyo wa wilaya kuwa hakikubaliki na kwamba ni kinyume cha kanuni za maadili, lakini haiwezi kumchukulia hatua.

“Wakuu wa mikoa na wilaya hawaruhusiwi kwenda katika kampeni na akifanya hivyo anakuwa amekiuka maadili ya uchaguzi,” alisema na kuongeza,

“Na kama amekiuka vyama vinavyoshiriki uchaguzi vinapaswa kuwasilisha malalamiko katika Kamati ya Maadili ndani ya saa 72.”

Alisisitiza, “Jambo hili tume hatuingii popote na vyama hivyo vya siasa vinalijua hili. Wanatakiwa kumpeleka kamati ya maadili ambayo wajumbe wake wanatoka katika vyama vinavyoshiriki uchaguzi, lakini iwe ndani ya saa 72 tangu kitendo hicho kilipotokea na wao watachukua hatua.”

Alivitaka vyama vya siasa kutokimbilia kulalamika bila kuchukua hatua kwani kama kuna uvunjifu wa maadili, kamati ina mamlaka ya kuwasilisha hilo katika ngazi nyingine ya kisheria kama polisi au kwa DPP (mkurugenzi wa mashtaka).

Kailima alibainisha kuwa NEC katika barua zao hawakuwazuia wakuu wa wilaya na mikoa kushiriki kampeni, bali waliwakumbusha kutojihusisha na kampeni kwani ni kinyume cha kanuni za maadili.

Vyama vyacharuka

Mkurugenzi wa itikadi, mawasiliano na mambo ya nje wa Chadema, John Mrema alisema, “Kama kweli NEC inasema iliwaandikia barua basi ituonyeshe hizo barua, lakini ichukue hatua kwa mkuu huyo wa wilaya ambaye amekiuka agizo hilo walilolitoa.”

Alisema waliposusia kushiriki uchaguzi wa Januari 13, moja ya sababu ni watendaji wa Serikali kuingilia chaguzi na endapo NEC haitachukua hatua wataeleza watakachokifanya kukomesha tabia hiyo.

“Sheria ya utumishi wa umma inazuia watumishi wa umma kujihusisha na siasa, huyu DC kavunja hiyo sheria na kama kuna usawa katika hili basi mamlaka zimchukulie hatua, anatumia nyenzo za Serikali katika mambo ya siasa, NEC ichukue hatua,” alisisitiza.

Mkurugenzi wa Habari wa CUF upande wa Profesa Ibrahim Lipumba, Abdul Kambaya alisema tatizo la wakuu wa mikoa na wilaya ni kubwa.

Alisema viongozi hao wamekuwa wakichangia uchaguzi kutokuwa huru na haki na kwamba jambo hilo linachangiwa na NEC kutokuwa na nguvu ya kuwashughulikia watendaji wa Serikali.

“NEC ina changamoto ya kusimamia uchaguzi na ina watendaji wachache ukilinganisha na wakurugenzi wanaosimamia uchaguzi na kutangaza matokeo. Kama akihakikishiwa ulinzi anamtangaza asiye mshindi na hii ni changamoto kubwa sana kwa tume yetu,” alisema Kambaya.

Kampeni Siha

Jana, katika kampeni za uchaguzi Siha zilizofanyika viwanja vya Ngarenairobi, katibu wa itikadi na uenezi wa CCM, Humphrey Polepole alimpigia debe Dk Mollel akitaka wananchi wamchague ili akashirikiane kwa karibu na Serikali kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili.

Alizitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni migogoro ya ardhi, miundombinu mibovu ya barabara, ukosefu wa kituo cha afya na ukosefu wa ajira.

“Mkitupa Dk Mollel, lazima turudi hapa kushughulikia tatizo la ardhi ambalo limewafanya kuishi kwa msongamano wakati mmezungukwa na maheka ya ardhi,” alisema Polepole na kuongeza,

“CCM hatubebi mizigo ya misumari, tunapokea watu ambao ni vichwa na wanaweza kushirikiana na Serikali kuwaletea wananchi maendeleo.”

Kwa upande wake, Dk Mollel aliwaambia wananchi wa Ngarenairobi kuwa anatambua mchango wao wa mwaka 2015, hivyo wamrudishe ulingoni ili akatatue changamoto zinazowakabili ambazo alishindwa kuzitatua akiwa upinzani.

Kinondoni pingamizi kibao

Katika Jimbo la Kinodnoni, wagombea watatu wa Chadema, CCM na Sau waliwekeana pingamizi.

Msimamizi msaidizi wa jimbo hilo, Latifa Almas aliwataja wagombea hao kuwa ni Mtulia, Mwalimu na Johnson Mwangosi (Sau).

Almas alisema pingamizi la kwanza ni lile la Mwalimu alilomuwekea Mtulia, la pili ni la Mtulia kumwekea Mwangosi na la mwisho ni la mgombea wa CUF, Rajab Salum Juma kumuwekea Mwalimu.

Almasi alisema wagombea hao wote wameshapewa taarifa za pingamizi hizo, tayari wameshachukua fomu za kutakiwa kujieleza wanazotakiwa kuzijaza na kuzirejesha haraka iwezekanavyo.

Alisema iwapo waliowasilisha mapingamizi hao hawataridhika, wanaweza kukata rufaa NEC.

Wakili wa Mwalimu, Fredirick Kihwelo alisema pingamizi dhidi ya mgombea wa CCM ni kutofanya mrejesho wa gharama za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Alisema nyingine ni Mtulia kushindwa kukidhi matakwa ya kisheria kwa kutojaza kwa usahihi fomu zake, kwa madai kuwa zimepigwa muhuri wa katibu wa CCM badala ya muhuri wa chama hicho tawala.

Alisema hoja ya mwisho ni Mtulia kujaza fomu akieleza kuwa anajishughulisha na kilimo cha mbogamboga, jambo ambalo Kihwelo amesema si kweli.

Hata hivyo, Mtulia alizijibu hoja hizo akisema ”Hili jambo jepesi sana na nimeandika ninachokijua na hakuna pingamizi hapo.”

Katika pingamizi la Mwalimu dhidi ya mgombea wa Sau, amesema Mwangosi amekosea kujaza fomu kwa maelezo kuwa jina lake linasomeka Mwangosi Johnson Joel badala Joel Johnson Mwangosi kama alivyoandika katika fomu ya kiapo.

Source: Mwananchi