Friday, 19 January 2018

Mwanamke aokotwa akiwa amekatwa matiti

KAMANDA WA POLISI MKOA WA KAGERA, AGUSTINE OLLOMI.

MWILI wa Betia Felix (18) mkazi wa Kijiji cha Nyakatete, wilayani Kyerwa mkoa wa Kagera, umeokotwa ukiwa umekatwa matiti na kufungwa kamba miguuni.

Marehemu huyo, alionekana kichakani Ijumaa iliyopita saa 4:00 asubuhi karibu na maeneo ya mashamba ya wanakijiji hicho baada ya ndugu kutokumwona nyumbani kwao kwa muda wa siku saba na kutoa taarifa ofisi za kijiiji.

Mwenyekiti wa kijiji hicho Josephat Mtayoba, alisema baada ya kupokea taarifa za binti huyo na kuwasiliana na ndugu wa marehemu walisema wakati akiondoka alikuwa anawasiliana na watu ambao ndugu zake hawakuwafahamu.

"Kwa kijiji hiki ni tukio la kwanza kushuhudia mauaji ya kushtua kama hatua zinazoendelea kuchukuliwa ni kuweka na kuimarisha ulinzi shirikishi, "alisema Mtayoba.

Baba wa marehemu huyo Felix Gabriel , alisema binti yake, alitoka shambani akiwa na jembe na kuliweka nyumbani kisha kuondoka akiwa anaongea na simu, lakini hakufahamu alikuwa akiongea na nani.

Aidha alisema baada ya kukaa kwa muda mrefu akiwa haonekani nyumbani alidhani kuwa mwanae atakuwa ameolewa hivyo anasubiri kupokea mahari kutoka kwa wakwe.

“Aliondoka nyumbani tangu Januari 5, mwaka huu na mwili wake kuokotwa na mdogo wake mchunguzi Felix Ijumaa iliyopita Januari 12 mwaka huu,”alisema Gabriel.

"Nilivyoona anaondoka sikushtuka kwani nilijua atarudi na alivyokaa siku nyingi nilidhani atakuwa ameolewa nilijipanga kupokea mahari ya binti yangu, "alisema Gabriel kwa uchungu.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Agustine Ollomi, alithibitisha tukio hilo na kusema kuwa Jeshi la Polisi linaendelea kuwatafuta wahalifu hao na kwamba hakuna aliyenaswa.

Kipimo cha kutambua aina tofauti za saratani chagundulika

Wanasayansi wamepiga hatua kubwa katika matibabu ya binadamu kwa kupata kipimo cha damu kinachogundua aina tofauti za Saratani.

Timu ya Watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Johns Hopkins wamefanyia utafiti njia ambazo zinaweza kugundua aina nane zinazosababisha ugonjwa huo.

Watafiti hao kutoka Uingereza wanasema mtu anapaswa kufanyiwa uchunguzi kwa mwaka, ili kuweza kugundua ugonjwa wa Saratani mapema na kuweza kuokoa maisha yake. Huku wakisifia matokeo ya utafiti wao.

Uvimbe hutokea na kuonesha dalili kwamba ni ugonjwa wa Saratani hutoa viashiria vidogo vya vinasaba -DNA- zilizobadilika pamoja na protein kwenye mfumo wa damu.

Uchunguzi wa kutafuta saratani unatafuta mabadiliko ya vinasaba 16 ambavyo hutokea mara kwa mara katika saratani, na proteni nane ambazo huwa ni viashiria vya hali ya mgonjwa.

Utafiti huo ulifanyiwa majaribio kwa wagonjwa 1,005 wenye Saratani katika ini, tumbo, mirija ya uzazi, mapafu na maeneo mengine mbalimbali ambayo bado ugonjwa huo haujaenea katika maeneo mengine.

Kwa ujumla vipimi vya utafiti huo hupata asilimia 70 ya Saratani.

Akizungumza na BBC Dokta Cristian Tomasetti kutoka Chuo Kikuu cha Johns Hopkins amesema hatu ya kutambua ugonjwa wa Saratani mapema ni muhimu na matokeo ni ya kusisimua.

Saratani inapogundulika mapema inakuwa na nafasi kubwa ya kuweza kuitibu.

Wataalamu wanasema pia kwa baadhi ya wagonjwa matibabu yanaweza kuwa mabaya zaidi kuliko kuishi na saratani yenyewe ambayo haiatarishi haraka maisha.

Wizara kuomba kubali cha Kuajiri



NAIBU Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Faustine Ndungulile, amesema wizara yake imeanza kukabiliana na changamoto ya watumishi wa Afya kwa kuomba kibali cha kuajiri.

Dk. Ndungulile alitoa kauli hiyo jana alipokuwa ziarani mkoani Mbeya baada ya kupokea taarifa ya wafanyakazi wa idara hiyo kutoka kwa Muuguzi Mkuu wa Mkoa, Elesia George, unakabiliwa na upungufu mkubwa wa watumishi wa idara hiyo.

Elesia alisema upungufu huo wa watumishi umepelekea vituo vya Afya na Zahanati za Serikali 59 mkoani humo kuongozwa na wauguzi kutokana na kutokuwa na madaktari.

Alisema hali hiyo inahatarisha afya za wananchi kutokana na uwezo mdogo wa wauguzi hao usioendana na majukumu wanayopewa.

Alisema uhaba wa watumishi hao unapelekea wauguzi wanaopewa majukumu hayo kufanya kazi nyingi kwa wakati mmoja na hivyo kuwapunguzia ufanisi wa kazi.

Aliomba Serikali iajiri watumishi wa kada hiyo ili kuimarisha utoaji wa huduma za afya kwa wananchi na kuwapunguzia mzigo wauguzi ambao wanapewa majukumu wasiyokuwa na uwezo wa kuyamudu.

“Ili huduma za afya ziwe bora ni vizuri tukawa na professionals (wanataaluma), kwenye mkoa wetu tuna upungufu mkubwa wa matabibu hivyo unakuta wauguzi wanafanya kazi zote, tunaomba kwenye kama kuna ajira mpya tunaomba kada hii izingatiwe,” alisema Elesia.

Baada ya maelezo hayo ya Muuguzi Mkuu wa Mkoa, Naibu Waziri Dk. Ndugulile alikiri kuwepo kwa changamoto hiyo, lakini akasema wizara yake tayari imeshaanza kuchukua hatua kwa kuomba kibali cha kuajiri watumishi wapya.

Alisema wanakusudia kuajiri watumishi hasa kwenye maeneo nyeti ili kukabiliana na changamoto zinazoikabili sekta ya Afya nchini na hata kuwapunguzia kazi baadhi ya watumishi ambao wana majukumu mengi wakati mwingine.

“Wekeni masanduku ya maoni kwenye maeneo yote ambayo yana mkusanyiko mkubwa wa watu, ili mjuwe malalamiko ya wananchi na myashughulikie na yale mnayoshindwa mnayaleta wizarani tunayashughulikia,” alisema Dk. Ndugulile.

Pia Dk. Ndungulile alisema Serikali inafanya jitihada kubwa kwa kushirikiana na wananchi kuhakikisha inaimarisha afya za wananchi hivyo akaeleza kuwa juhudi hizo bila watumishi wa afya wa kutosha hazitakuwa na maana.

Alisema kwa sasa juhudi kubwa zimeelekezwa kwenye ujenzi wa vituo vya Afya na zahanati nchini ikiwa ni harakati za kuimarisha afya ya msingi kwa wananchi wake.

Naye Ofisa Ustawi wa Jamii wa Mkoa wa Mbeya, Aika Temu, alisema kada hiyo hapa inakabiliwa na changamoto ya uhaba wa watumishi na hivyo kufifisha jitihada za kuhamasisha wananchi kwenye shughuli za maendeleo.

Alisema mkoa mzima wa Mbeya wenye wilaya tano na halmashauri saba una maofisa ustawi wa jamii 39 pekee, hivyo akaomba pia Serikali kuimulika idara hiyo wakati wa kuajiri watumishi wapya.

New Zealand: Waziri mkuu afunguka kuwa na ujauzito

Waziri mkuuwa New Zealand mwenye umri wa miaka 37 Jacinda Ardern asema ana ujauzito
Waziri mkuu wa New Zealand Jacinda Ardern amefichua kwamba yeye ni mjamzito.

Bi Ardern alisema kwamba yeye na mpenzi wake Clarker Gayford walikuwa wakitarajia mwana wao mwezi Juni ambapo baadaye atachukua likizo ya wiki sita.

''Na tulidhani kwamba mwaka 2017 ni mwaka mkuu'', aliandika katika mtandao wake wa Instagram.

Bi Ardern mwenye umri wa miaka 37 alikuwa waziri mkuu mwenye umri mdogo nchini New Zealand tangu 1856 akiungwa mkono wakati alipotangaza kuhusu hali yake mpya siku ya Ijumaa.

Chama cha leba cha Bi Ardern kilikuwa cha pili katika uchaguzi wa mwezi Septemba ambapo hakuna chama kilichofanikiwa kupata wingi wa kura.

Aliunda serikali kupitia usaidizi wa Winston Peters ambaye ni kiongozi wa chama kidogo cha New Zealand.

''Nitakapokuwa ugenini Bwana Peters atakuwa kaimu waziri mkuu, akifanya kazi na ofisi yangu mbali na kuwasiliana nami'', alisema bi Ardern katika taarifa ilioripotiwa na gazeti la New Zealand Herald siku ya Ijumaa.

''Nitawasiliana na kupatikana katika kipindi hicho cha wiki sita wakati nitakapohitajika''.

Bi Ardern alisema kuwa aligundua kwamba ni mjamzito siku sita kabla ya kujua kwamba atakuwa waziri mkuu , na lilikuwa swala la kushangaza.

''Mimi sio mwanamke wa kwanza kufanya kazi mbili.Sio mwanamke wa kwanza kufanya kazi huku nikihudumia mwanangu, kuna wanawake wengi ambao wamekuwa katika hali kama hii awali'', alisema.

''Bwana Gayford atakuwa baba ambaye atakuwa akisalia nyumbani'', aliongezea.

Mawaziri 2 wakuu wa zamani nchini humo walikuwa watu wa kwanza kutoa pongezi zao.

Ndege yatetemeka angani

Ndege moja ya Malaysia ililazimika kutua katika eneo la Australia ya kati baada ya tatizo la kiufundi kuifanya kuanza kutetemeka ikiwa angani, wamesema abiria.

Ndege hiyo aina ya MH122 ilikuwa inasafiri kuelekea Kuala Lumpur kutoka Sidney siku ya Alhamisi wakati iliporudi katika eneo ambalo haliko mbali na Broome, kaskazini Magharibi mwa Australia.

Ndege hiyo iliokuwa ikiwabeba watu 224 ilitua salama katika uwanja wa ndege wa Alice Springs Airport.

Abiria wanasema kuwa ndege hiyo ilikuwa ikitetemeka na kutoa sauti kubwa.

Katika taarifa yake, kampuni ya ndege ya Malaysia Airline ilisema kuwa ndege hiyo ilibadilsha safari kutokana na tatizo la kiufundi.

Hatahivyo haikusema ni matataizo gani. Abiria Sanjeev Pandev alisema kuwa ndege hiyo ilionekana kuwa na tatizo hilo saa nne kabla ya safari kuanza.

''Ilikuwa ikitetemeka na kelele zilikuwa kubwa '', aliambia BBC.

''Watu walikuwa wakiomba na wengine walikuwa wakitokwa na machozi'', aliambia BBC.

Alisema kuwa abiria walionyeshwa njia za kubaliana na dharura na wafanyikazi wengi wao wakionekana kuogopa na kushtuka.

Simba kukutana na waliokwamisha mipango

Vinara wa ligi kuu soka Tanzania Bara Simba SC leo alfajiri wameondoka kwa ndege kuelekea mjini Bukoba mkoani Kagera kwaajili ya mchezo wao wa raundi ya 14.

Simba ambayo jana ilishinda mchezo wake wa raundi ya 13 kwa mabao 4-0 dhidi ya Singida United kwenye uwanja wa Uhuru, inakwenda kukutana na Kagera Sugar ambayo ilikwamisha mipango yake ya ubingwa msimu uliopita.

Kagera Sugar ilitibua mipango hiyo April 2 mwaka jana baada ya kuifunga Simba mabao 2-1 kwenye mechi iliyopigwa uwanja wa Kaitaba hivyo kuinyima nafasi ya kurejea kileleni ikibaki na alama 55 katika nafasi ya pili na kuwaacha Yanga wakiwa na alama 56 kileleni.

Endapo Simba ingeshinda mchezo huo ingefikisha alama 58 hivyo huenda ingetwaa ubingwa kutokana na bingwa wa msimu uliopita kupatikana kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa, baada ya timu hizo mbili za Kariakoo kufungana pointi.

Simba ambayo kwasasa inaongoza ligi kwa alama 29 mbele ya Azam FC yenye alama 27, itashuka dimbani Kaitaba siku ya Jumapili.


Thursday, 18 January 2018

Audio | Jacko Beatz Ft Moni Centrozone – Baby | Mp3 Download

Audio | Jacko Beatz Ft Moni Centrozone – Baby | Mp3 Download
Audio | Jacko Beatz Ft Moni Centrozone – Baby | Mp3 Download

Batuli awataka mastaa kumrudia Mungu


Yobnesh Yusuph ‘Batuli’.

MSANII mwenye mvuto Bongo Muvi, Yobnesh Yusuph ‘Batuli’ amewasihi wasanii wenzake wajaribu kumrudia Mungu japo mara moja kwa wiki.

Akizungumza na Showbiz Xtra, Batuli alisema kuwa anatambua mastaa wengi wamesahau kusali kabisa na kujua kama kuna Mungu huku wakiendelea kufanya vingi vya kidunia.

“Jamani hakuna kitu kizuri kama kuona staa akiwa kanisani au msikitini yaani hata jamii inakuchukulia kwa mtazamo wa tofauti kabisa, tumrudie Mungu,” alisema Batuli.


Picha ya Selfie kwenye Facebook yasababisha muuaji kupatikana Canada


Mkanda unaovaliwa na Cheyenne Antoine (kushoto) unaonekana kwenye picha na rafiki yake Brittney Gargol

Mwanamme mmoja nchini Canada amepatikana na hatia ya kumuua rafiki yake baada ya polisi kugundua kuwa kifaa kilichotumiwa kuua kilichokuwa kwenye picha ya kujipiga (selfie) ya wawili hao iliyokuwa katika mtandao ya kijamiii.

Cheyenne Rose Antoine, 21, alikiri siku ya Jumatatu kumuua Brittney Gargol, 18, Machi mwaka 2015.

Gargol alipatikana amenyongwa karibu na Saskatoon, Saskatchewan, huku mkanda wa Antoine ukiwa kando na mwili wake.

Antoine alihukumiwa kifungo cha miaka saba jela kwa mauaji

Alitajwa kama mshukiwa baada ya kuchapisha picha ya selfie kwenye mtandao wa Facebook, ikionyesha amevaa mkanda uliotumika saa kadhaa kabla ya Gargol kuuliwa.

Alisema walikuwa wamekunywa pombe na pia wakavuta bangi kabla kuanza kuzozana.

Polisi wanasema kuwa taarifa ambayo alikuwa amewapa, kuwa Gargol aliondoka na mwanamume mmoja huku naye akionda kumuona shangazi yake.

Ndipo wakatumia picha zake za Facebook kufuatilia mienendo ya wawili hao usiku huo.



Hii ndio Treni inayobweka kama mbwa ili kuwafukuza swara kwenye reli



Watafiti nchini Japana wameiwekea treni kipasa sauti ambacho kinabweka kama mbwa na kutoa mlio wa swara ili kuzuia treni kugonga swara njiani.

Gazeti la Asahi Shimbun lilisema kuwa sauti hizo zinatumiwa kuwafukuza swara kutoka kwa reli kwa lengo la kupunguza idadi ya wanaogongwa na kuuawa na treni.

Maafisa kutoka kwa taasisi ya reli wanasema kuwa mlio wa sekunde tatu wa swara humfanya swara kuwa makini na kusikiliza, ukifuatiwa na sekunde 20 za mbweko wa mbwa, inaweza kusababisha swara kukimbia.

Watafiti wanasema kuwa majaribio ya usiku wakati swara wanakusanyika kando ya reli yamesababisha swara hao kupungua.

Swara hukaribia reli nyakati za usiku kulamba chuma za reli wakitafuta virutubishi muhimu vya madini ya mwili.

Wizara ya uchukuzi nchini Japan inasema kuwa kulikuwa na visa 613 vya treni kugonga swara na wanyama wengine mwaka 2016.

Abiria wasota Kivukoni


Dar es Salaam. Abiria wanaotumia kivuko eneo la feri wamejikuta wakisota kituoni hapo leo Alhamisi baada ya kivuko kikubwa cha MV Magogoni kupata hitilafu hivyo kubaki vivuko viwili ambavyo vinabeba idadi ndogo ya abiria.

Mwananchi ilifika eneo la kivukoni na kukuta msongamano mkubwa wa abiria wakiwa wanasubiri usafiri huo na wengine wakiamua kuondoka kutokana na kusubiri kwa muda mrefu.

Mmoja wa wasimamizi wa ufundi aliejitambulisha kwa jina moja la Ndunguru amesema tatizo hilo limeanza toka usiku kutokana na MV Magogoni kubeba idadi kubwa ya abiria lazima usumbufu ujitokeze.

“Tatizo limeanza tangu usiku ingawa mimi sio msemaji ila unavyoona mafundi wanaendelea na kazi kuhakikisha tatizo linaisha, kivuko hiki ni kikubwa na kinabeba idadi kubwa ya abiria hivyo kikiaribika lazima usumbufu ujitokeze,” amesema Ndunguru.

Makonda: Dar Kujengwa Kiwanda Kikubwa Zaidi Barani Afrika


Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Mhe Paul Makonda leo amekutana wawekezaji kutoka China kujadiliana kuhusu mambo ya uwekezaji nchini Tanzania.

Mhe Makonda akizungumza katika mkutano huo Mhe. Makonda amesema kuwa  kutokana na malengo yaliyo wekwa na Wizara ya TAMISEMI maelekezo kutoka kwa Rais John Pombe Magufuli kuwa kila Mkoa uhakikishe unajenga viwanda 100 hivyo wawekezaji hawa wanakwenda kuwekeza Tanga na kunduchi jijini Dar es Salaam na wana wekeza miradi yenye  thamani ya Dola  bilioni 3dola.

Aidha amewataka wanachi wa mkoa huo kuchangamkia fursa za uwekezaji
"sisi kazi yetu  kama serikali ni kuweka mazingira ya uwekezaji na hawandugu zetu wametoka jimbo la  nilizungumza nao nilipotembelea huko kwao mwakajana"Amesema Makonda.

Pamoja na hayo Makonda  amesema kuwa kuna clip ina zungunguka mtandaoni ikieleza kuwa Ethiopia wana kiwanda kikubwa zaidi kuliko nchi zote barani Afrika na kusema kuwa wananchi wasihofu kwani Dar es Salaam itajenga kiwanda kikubwa zaidi ya mara tatu ya hicho chenye  mita za mraba Milion Tano na uwekezaji huu utafanyika wilayani Kigamboni.

"Kuna mwekezaji mwingi ameonyesha nia ya kuwekeza kiwanda cha sukari nawaomba wafanyabiashara wetu mchangamkie fursa hizo za kibiashara   na vijana pia mchangamkie fursa za ajira" Amesema Makonda.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa jimbo la Gwangzou , Xie zhenghy kutoka China amesema wao wako tayari kwa uwekezaji na katika nchi ambazo zitaendana kiutamaduni kama ilivyo kwa Tanzania.
Hata hivyo amesema kuwa China imekuwa na nafasi kubwa ya kuwekeza barani Afrika ambapo imekuwa na uwekezaji mkubwa nchini Misri.

Akizungumzia uwekezaji hapanchini amesema kuwa uwekezaji watakaofanya ni ule unaendana na kaulimbiu ya Rais John Pombe Magufuli.

Bunduki ya kivita yenye skafu ya Chadema yakamatwa Shinyanga


Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule akionesha silaha aina ya AK-47 yenye namba 18116428 na mafuta ya kulainishia silaha yaliyotupwa na majambazi waliotaka kuvamia kiwanda cha Jielong

 Jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga limefanikiwa kukamata silaha ya kivita aina ya AK-47 iliyotupwa na watu wanaodaiwa kuwa ni majambazi waliokuwa wanataka kuvamia kiwanda cha kutengeneza mafuta ya kupikia cha Jielong Holdings (Tanzania) Ltd kilichopo Nhelegani katika kata ya Kizumbi manispaa ya Shinyanga.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo Alhamis Januari 18,2018 Kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Simon Haule amesema walikamata silaha hiyo usiku wa kuamkia leo majira ya saa tano eneo la Tinde wakati majambazi hao wanafuatiliwa na polisi ndipo wakaamua kutupa bunduki hiyo.

“Silaha hii aina ya AK-47 yenye namba 18116428 ilikuwa imefungwa kwenye skafu yenye rangi ya nembo ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ikiwa na risasi 25 ndani ya magazine yake na risasi zingine 8,zikiwa kwenye mfuko mdogo wa nailoni”,alieleza Kamanda Haule.

“Majambazi wawili pia walitelekeza pikipiki aina ya SANLG yenye namba za usajili MC 856 BPF,mafuta ya cherehani ya kulainishia silaha,tochi mbili na koti zito”,aliongeza.

Alisema jeshi la polisi lilipata taarifa za majambazi hao kutaka kuvamia kiwanda hicho kinachomilikiwa na raia wa China tangu tarehe 6.01.2018 kisha kuanza kuwafuatilia na kubaini kuwa baadhi yao ni wakazi wa Kahama na Ushirombo ambapo amewataka kujisalimisha polisi.