Tuesday, 23 January 2018

Neno la Buswita kwa mashabiki wa Yanga


BAADA ya kufunga bao pekee lililowapa ushindi Yanga dhidi ya Ruvu Shooting juzi, kiungo Pius Buswita, amewapa neno la faraja mashabiki wa timu hiyo kwa kuwaeleza "sasa tunarudi kwenye kasi yetu".

Buswita, alisema mashabiki wa timu hiyo hawapaswi kuwa na wasiwasi kwa nafasi ya tatu wanayoshika kwenye msimamo wa ligi.

“Mashabiki wasiwe na hofu, taratibu tunarudi kwenye kasi yetu na tunaweza kufanya vizuri zaidi, lengo letu ni kuhakikisha tunashinda katika kila mchezo bila kuangalia matokeo ya wengine,” alisema Buswita.

Aidha, alisema kuwa timu hiyo bado ina nafasi ya kutetea ubingwa wao, jambo ambalo mashabiki wanapaswa kuwa na matumaini hayo.

“Ukiangalia hakuna tofauti kubwa ya pointi na timu inayoongoza ligi, tutaendelea kupambana kuhakikisha tunatetea ubingwa wetu,” alisema Buswita.

Kiungo huyo wa zamani wa Mbao FC, juzi alifunga bao pekee wakati Yanga wakiibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Ruvu Shooting, ushindi huo umeifanya Yanga inayodhaminiwa na Kampuni ya Kubashiri Matokeo Michezoni ya SportPesa, kukusanya pointi 25 huku Azam wakiwa na pointi 30 wakifuatiwa na Simba wenye pointi 29 (kabla ya mchezo wake wa jana dhidi ya Kagera Sugar)

“Sio mimi niliesema CCM imeoza”: Ridhiwan Kikwete akanusha


Mbunge wa Chalinze kupitia Chama cha Mpainduzi (CCM), Ridhiwani Kikwete amekanusha ujumbe unaosambazwa katika mitandao ya kijamii ukidai kuwa amekikosoa chama hicho kutokana na kutoridhishwa na mwenendo wake.

Akizungumza jana jioni, Ridhiwani amewataka watanzania na wanachama wa CCM kupuuza taarifa hiyo kwani siyo yeye ameitoa na badala yake ni watu wenye lengo lakukiharibu chama hicho.

Amesema kwamba, kwa siku nzima ya jana hajaandika ujumbe wowote na kwamba alikuwa jimbo kwake katika vikao vya halmashauri wakipanga mipango ya bajeti kwa ajili ya maendeleo ya jimbo hilo.


DC aingia matatani kwa kupiga kampeni


Mgombea ubunge Jimbo la Kinondoni (CUF), Rajab Salum Juma akihutubia katika mkutano wa kampeni uliofanyika kwenye Uwanja wa Ally Mapilau, Mwananyamala jijini Dar es Salaam.

Kitendo cha Mkuu wa Wilaya ya Siha, Onesmo Buswelu kupanda jukwaani kumnadi mgombea wa CCM katika Jimbo la Siha, Dk Godwin Mollel kimechafua hali ya hewa baada ya kupingwa na vyama vya siasa huku Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ikisema hakufanya jambo sahihi.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Ramadhani Kailima ameliambia Mwananchi jana kuwa ili Buswelu aweze kuchukuliwa hatua, wenye jukumu la kumshtaki ni vyama vinavyopinga jambo alilolifanya.

Alisema vyama hivyo vinatakiwa kumshtaki katika kamati ya maadili inayoundwa na wajumbe wa vyama vinavyoshiriki uchaguzi katika jimbo husika na kwamba jambo hilo linapaswa kufanyika ndani ya saa 72, tangu apande jukwaani.

Wakati DC huyo akiibua kizazaa hicho, CCM imeendelea kumnadi Dk Mollel huku katika Jimbo la Kinondoni, wagombea ubunge wa CCM, Chadema na Sau wakiwekewa pingamizi.

Uchaguzi wa Siha na Kinondoni utafanyika Februari 17 na unavishirikisha vyama 12, huku ukitajwa kuwa ni mpambano mkali baina ya CCM na Chadema inayoungwa mkono na vyama vitano vya Ukawa ambavyo ni NLD, NCCR-Mageuzi, CUF upande wa Maalim Seif Sharif Hamad na Chaumma iliyojiunga hivi karibuni.

Uchaguzi huo unafanyika baada ya waliokuwa wabunge; Mollel (Siha- Chadema) na Maulid Mtulia (Kinondoni-CUF) kujivua uanachama wa vyama hivyo kwa maelezo kuwa wanamuunga mkono Rais John Magufuli na baadaye kujiunga CCM.

Chama hicho tawala kimewapitisha wawili hao kutetea majimbo hayo, huku Chadema ikimsimamisha naibu katibu mkuu (Zanzibar), Salum Mwalimu (Kinondoni) na Elvis Mosi (Siha).

Buswelu ‘alivyochafua hewa’

Juzi katika uzinduzi wa kampeni za Dk Mollel katika viwanja vya KKKT Karansi Jimbo la Siha, Buswelu alisema Serikali haijaribiwi hivyo ni vyema kila mmoja akahakikisha anadumisha amani na kufanya siasa za kistaarabu katika kipindi chote cha kampeni.

Alisema Dk Mollel ameleta heshima kwa wananchi wa Siha huku akiwataka wananchi wote kumuunga mkono na kuhakikisha anapata ushindi wa kishindo.

NEC ilivyomruka Buswelu

Akizungumza na Mwananchi, Kailima alikiri kitendo alichokifanya mkuu huyo wa wilaya kuwa hakikubaliki na kwamba ni kinyume cha kanuni za maadili, lakini haiwezi kumchukulia hatua.

“Wakuu wa mikoa na wilaya hawaruhusiwi kwenda katika kampeni na akifanya hivyo anakuwa amekiuka maadili ya uchaguzi,” alisema na kuongeza,

“Na kama amekiuka vyama vinavyoshiriki uchaguzi vinapaswa kuwasilisha malalamiko katika Kamati ya Maadili ndani ya saa 72.”

Alisisitiza, “Jambo hili tume hatuingii popote na vyama hivyo vya siasa vinalijua hili. Wanatakiwa kumpeleka kamati ya maadili ambayo wajumbe wake wanatoka katika vyama vinavyoshiriki uchaguzi, lakini iwe ndani ya saa 72 tangu kitendo hicho kilipotokea na wao watachukua hatua.”

Alivitaka vyama vya siasa kutokimbilia kulalamika bila kuchukua hatua kwani kama kuna uvunjifu wa maadili, kamati ina mamlaka ya kuwasilisha hilo katika ngazi nyingine ya kisheria kama polisi au kwa DPP (mkurugenzi wa mashtaka).

Kailima alibainisha kuwa NEC katika barua zao hawakuwazuia wakuu wa wilaya na mikoa kushiriki kampeni, bali waliwakumbusha kutojihusisha na kampeni kwani ni kinyume cha kanuni za maadili.

Vyama vyacharuka

Mkurugenzi wa itikadi, mawasiliano na mambo ya nje wa Chadema, John Mrema alisema, “Kama kweli NEC inasema iliwaandikia barua basi ituonyeshe hizo barua, lakini ichukue hatua kwa mkuu huyo wa wilaya ambaye amekiuka agizo hilo walilolitoa.”

Alisema waliposusia kushiriki uchaguzi wa Januari 13, moja ya sababu ni watendaji wa Serikali kuingilia chaguzi na endapo NEC haitachukua hatua wataeleza watakachokifanya kukomesha tabia hiyo.

“Sheria ya utumishi wa umma inazuia watumishi wa umma kujihusisha na siasa, huyu DC kavunja hiyo sheria na kama kuna usawa katika hili basi mamlaka zimchukulie hatua, anatumia nyenzo za Serikali katika mambo ya siasa, NEC ichukue hatua,” alisisitiza.

Mkurugenzi wa Habari wa CUF upande wa Profesa Ibrahim Lipumba, Abdul Kambaya alisema tatizo la wakuu wa mikoa na wilaya ni kubwa.

Alisema viongozi hao wamekuwa wakichangia uchaguzi kutokuwa huru na haki na kwamba jambo hilo linachangiwa na NEC kutokuwa na nguvu ya kuwashughulikia watendaji wa Serikali.

“NEC ina changamoto ya kusimamia uchaguzi na ina watendaji wachache ukilinganisha na wakurugenzi wanaosimamia uchaguzi na kutangaza matokeo. Kama akihakikishiwa ulinzi anamtangaza asiye mshindi na hii ni changamoto kubwa sana kwa tume yetu,” alisema Kambaya.

Kampeni Siha

Jana, katika kampeni za uchaguzi Siha zilizofanyika viwanja vya Ngarenairobi, katibu wa itikadi na uenezi wa CCM, Humphrey Polepole alimpigia debe Dk Mollel akitaka wananchi wamchague ili akashirikiane kwa karibu na Serikali kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili.

Alizitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni migogoro ya ardhi, miundombinu mibovu ya barabara, ukosefu wa kituo cha afya na ukosefu wa ajira.

“Mkitupa Dk Mollel, lazima turudi hapa kushughulikia tatizo la ardhi ambalo limewafanya kuishi kwa msongamano wakati mmezungukwa na maheka ya ardhi,” alisema Polepole na kuongeza,

“CCM hatubebi mizigo ya misumari, tunapokea watu ambao ni vichwa na wanaweza kushirikiana na Serikali kuwaletea wananchi maendeleo.”

Kwa upande wake, Dk Mollel aliwaambia wananchi wa Ngarenairobi kuwa anatambua mchango wao wa mwaka 2015, hivyo wamrudishe ulingoni ili akatatue changamoto zinazowakabili ambazo alishindwa kuzitatua akiwa upinzani.

Kinondoni pingamizi kibao

Katika Jimbo la Kinodnoni, wagombea watatu wa Chadema, CCM na Sau waliwekeana pingamizi.

Msimamizi msaidizi wa jimbo hilo, Latifa Almas aliwataja wagombea hao kuwa ni Mtulia, Mwalimu na Johnson Mwangosi (Sau).

Almas alisema pingamizi la kwanza ni lile la Mwalimu alilomuwekea Mtulia, la pili ni la Mtulia kumwekea Mwangosi na la mwisho ni la mgombea wa CUF, Rajab Salum Juma kumuwekea Mwalimu.

Almasi alisema wagombea hao wote wameshapewa taarifa za pingamizi hizo, tayari wameshachukua fomu za kutakiwa kujieleza wanazotakiwa kuzijaza na kuzirejesha haraka iwezekanavyo.

Alisema iwapo waliowasilisha mapingamizi hao hawataridhika, wanaweza kukata rufaa NEC.

Wakili wa Mwalimu, Fredirick Kihwelo alisema pingamizi dhidi ya mgombea wa CCM ni kutofanya mrejesho wa gharama za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Alisema nyingine ni Mtulia kushindwa kukidhi matakwa ya kisheria kwa kutojaza kwa usahihi fomu zake, kwa madai kuwa zimepigwa muhuri wa katibu wa CCM badala ya muhuri wa chama hicho tawala.

Alisema hoja ya mwisho ni Mtulia kujaza fomu akieleza kuwa anajishughulisha na kilimo cha mbogamboga, jambo ambalo Kihwelo amesema si kweli.

Hata hivyo, Mtulia alizijibu hoja hizo akisema ”Hili jambo jepesi sana na nimeandika ninachokijua na hakuna pingamizi hapo.”

Katika pingamizi la Mwalimu dhidi ya mgombea wa Sau, amesema Mwangosi amekosea kujaza fomu kwa maelezo kuwa jina lake linasomeka Mwangosi Johnson Joel badala Joel Johnson Mwangosi kama alivyoandika katika fomu ya kiapo.

Source: Mwananchi

TIRA, IIT yaanzisha mfumo wa Kimtandao wa huduma za bima



Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) kwa kushirikiana na Taasisi ya Bima Tanzania (IIT) imeanzisha mfumo wa kimtandao wa huduma za bima kwa wateja wanaoingiza bidhaa kutoka nje ya nchi.

Akizungumza Kamishna wa TIRA, Dk Baghayo Saqware amesema mfumo huo unazitaka kampuni kuweka taarifa kwenye mtandao kwa mizigo inayoingizwa kutoka nje ya nchi na bima wanazotoza.

Hatua hiyo imekuja baada ya marekebisho ya Sheria ya Bima inayowataka waagizaji wa mizigo kutoka nje ya nchi kutumia kampuni za ndani za bima.

Kabla ya marekebisho ya sheria hiyo, waagizaji wa mizigo nchini waliweza kutumia kampuni za bima za nje ili kupata kinga ya bidhaa zao.

Akifungua mafunzo ya wadau wa bima kuhusu namna ya kutumia mfumo wa kusimamia ulipaji wa bima kwa mizigo na bidhaa kutoka nje, Dk Saqware amesema utarahisisha upatikanaji wa taarifa kwa ajili ya mamlaka za serikali kama vile Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Ofisi ya Takwimu Taifa (NBS).

Amesema mfumo huo utasaidia kufahamu kama sekta ya bima inakua ukilinganisha na ukuaji wa uchumi.

Dk Saqware amesema mfumo huo utazirahisishia mamlaka za serikali kama Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Ofisi ya Takwimu ya Taifa (NBS) kupata taarifa za bima kwa urahisi.

Amesema kampuni za bima na mawakala wataoshindwa kutoa taarifa zao kwenye mfumo wa mtandao huo watakuwa wanavunja sheria za nchi na hatua zitachukuliwa dhidi yao.

Amesema utumiaji wa kampuni za ndani za bima utasaidia kampuni za bima, madalali na mawakala kukua kibiashara na kuongeza mapato.

Kwa upande wake, Rais wa Taasisi ya Bima Tanzania (IIT), Bosco Bugali alisema mtandao huo pia utawasaidia wanaodai fidia kulipwa kwa haraka na kwa ufanisi kwani hawatahangaika kuwasiliana na kampuni za bima za nje ya nchi.

BREAKING NEWS: Rais Magufuli amtumbua Mkurugenzi wa halmashauri ya Butiama


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo Januari 23, 2018 ametengua uteuzi wa Mkurugenzi wa halmashauri ya Butiama mkoani Mara Solomoni Ngiliule kuanzia leo kutokana na ubadhirifu wa fedha za Umma.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, Selemani Jafo ametangaza maamuzi hayo leo zikiwa zimepita siku tatu toka Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipotoa maagizo kwa Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara Bw. Raphael Nyanda kutuma timu ya wakaguzi kwenda kufanya ukaguzi maalumu katika ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Butiama.

Waziri Mkuu aliagiza kiongozi huyo kuchunguzwa kutokana na matumizi yasiyoeleweka ya fedha za miradi ya maendeleo zinazotolewa na Serikali zikiwemo sh. milioni 12 walizotumia kuandaa profile ya Halmashauri hiyo huku fedha zingine ni pamoja na sh. milioni 70 za elimu maalumu, sh. milioni 288 za mradi wa maji Butiama ambazo zote hazikujulikani zimetumikaje.

Nafasi za kazi leo Jan 23

Salum Mwalimu:Nipo tayari kuwa mwendawazimu


Mgombea Ubunge wa Jimbo la Kinondoni ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Zanzibar Salum Mwalimu amefunguka na kudai yupo tayari kuwa mwendawazimu kwa kuwapigania wananchi wa jimbo hilo akiwa Bungeni.

Salum Mwalim ameeleza hayo ikiwa imepita siku moja tokea Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuruhusu kuanza kwa kampeni rasmi za uchaguzi mdogo katika majimbo mawili ambayo ni Kinondoni na Siha.

"Nakwenda Bungeni kulia na kuwa mwendawazimu kwa ajili mahitaji ya watu wa Kinondoni, hakuna wa kunikataza kuongea jambo lolote ambalo litakuwa lina tija kwa watu wangu. Nitahakikisha narudisha heshima ya kinondoni", alisema Salum Mwalim.

Uchaguzi wa Jimbo la Kinondoni unatarajiwa kufanyika mwezi ujao (Februari 17, 2018) ili kuweza kuziba nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo kwa tiketi ya chama cha wananchi (CUF), Maulid Mtulia aliyejiuzulu kiti na uanachama kwa chama hicho na nafasi zote za uongozi alizokuwa nazo hapo awali.

Msigwa aachiwa baada ya kukamatwa kwa tuhuma za kuchomwa nyumba kiongozi wa CCM


Jeshi la Polisi mkoani hapa lilimshikilia na kumuachia kwa dhamana Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa kwa tuhuma za kuratibu matukio mawili ya kihalifu likiwamo la kuchoma nyumba aliyokuwa akiishi Katibu wa Jumuiya ya Vijana wa CCM Iringa Mjini, Alfonce Muyinga.

Kamanda wa polisi mkoani hapa, Julisu Mjengi amesema mbunge huyo alikuwa akitafutwa kwa muda akituhumiwa kuratibu utekelezwaji wa matukio mawili ya kihalifu likiwamo la Januari 17 la kuchomwa kwa nyumba aliyokuwa akiishi Muyinga.

Mjengi alitaja tukio la pili kuwa ni lile la Januari 15 la kubomolewa kwa nyumba ya aliyekuwa Diwani wa Kata ya Mwangata Chadema, Anjelus Mbogo aliyejizulu nafasi yake na kuhamia CCM.

"Mchungaji Msigwa tulikuwa tukimtafuta kutokana na kuhusika kwake katika kuratibu matukio mawili ya kihalifu, lile la Januari 15 la kubomoa nyumba ya aliyekuwa diwani aliyehama Chadema na kujiunga na CCM pamoja na tukio la kuchoma nyumba aliyokuwa akiishi Katibu wa Jumuiya ya Vijana wa CCM Alfonce," amesema Mjengi na kuongeza;

"Na jana (Jumatatu) amejisalimisha mwenyewe hivyo tumemhoji hadi majira ya saa tatu usiku tulipomuachia kwa dhamana, taratibu nyingine zinaendelea na tutawajulisha pindi tukapozikamilisha," amesema

Msigwa amekuwa mtuhumiwa wa nne kukamatwa akihusisha na matukio hayo baada ya wiki iliyopita jeshi hilo kueleza kuwa linawashikiliwa watuhumiwa watatu kwa mahojiano kutokana na kuhusika na tukio la kuchoma nyumba ya aliyokuwa akiishi Katibu wa UVCCM.

Mdee, Bulaya ‘wachomoka’ kifungoni


Kifungo walichokuwa wakitumikia wabunge wa Chadema, Ester Bulaya (Bunda Mjini) na Halima Mdee (Kawe) cha kutokuhudhuria shughuli za Bunge kimemalizika na wamesema wamerejea na kasi ileile.

Wabunge hao waliadhibiwa kwa azimio la Bunge Juni 5 mwaka jana kutohudhuria mikutano mitatu ya Bunge ambayo ni jumla ya siku 47, waliyokosa ukiondoa shughuli zote za mikutano ya kamati za Bunge.

Adhabu hiyo ilikwenda sanjari na kulipwa nusu mshahara na posho kwa kipindi chote walichotumikia adhabu hiyo wakituhumiwa kudharau kiti cha spika.

Mikutano mitatu waliyoikosa ni wa bajeti uliokuwa ukiendelea, wa saba uliofanyika kati ya Septemba 5 hadi 15 na mkutano wa tisa wa Novemba 7 hadi 17.

Makato ya mshahara na posho yamebainishwa katika Kanuni 75 ya Bunge inayosema: “Mbunge aliyesimamishwa kazi atatoka katika Bunge na hataingia tena katika sehemu yoyote ya ukumbi wa Bunge na maeneo ya Bunge kwa muda wote atakapokuwa amesimamishwa na atalipwa nusu mshahara na nusu posho zinazoambatana na mshahara huo.”

Jana, kwa nyakati tofauti Bulaya na Mdee walizungumza na gazeti hili juu ya kurejea kwao, huku wakisema hawajutii kwa adhabu hiyo na hawatorudi nyuma au kutetereka katika kusimamia wanachokiamini.

“Nitaendelea kuwa Mdee yuleyule wa siku zote, kama walidhani wakinifungia mwaka nitabadilika. Hapana! Sitaraji kubadilika. Nimetumwa na wananchi wangu kusema ukweli na nitausema, sijaja kumpigia magoti mtu,” alisema.

Mdee ambaye pia ni mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha), alisema wakati akitumikia adhabu hiyo amepata fursa ya kufanya shughuli kwa karibu za jimboni kwake na zile za Bawacha.

Naye Bulaya alisema: “Nimerudi bungeni tayari na leo (jana) nilihudhuria kamati yangu ya uwekezaji na mitaji.”

Alipoulizwa amejifunza nini kutokana na adhabu hiyo, alisema: “Bulaya wa kukosoa, Bulaya anayesimamia kile anachokiamini pasi na kuvunja sheria na taratibu hajabadilika, nitaendelea kuwakosoa.”

“Hata nilipokuwa natoka CCM kuja Chadema nilijua mambo kama haya ya kukamatana, kufungiana yatakuwapo kwa hiyo nilijipanga na wala hawanitetereshi, nimerudi na sitarudi nyuma,” aliongeza.

Mkhitaryan kusaidia matibabu kwa wenye Kansa


IKIWA ni saa chache baada tu ya kutua Arsenal akitokea Manchester United, Henrikh Mkhitaryan amesema atatumia jezi ya Man U ili kusaidia matibabu ya watoto wa Armenia walioathirika kwa saratani.
Mkhitaryan amekabidhiwa jezi ya Arsenal jana huku Sanchez akikabidhiwa jezi ya Man United United huku wakibadilishana miji kutoka London kwenda Manchester.

“Katika kuwashukuru wote waliochangia katika filamu ya simulizi yangu, nitatoa jezi la klabu ya Manchester United lililosainiwa na wachezaji ili kuwasaidia watoto wa Armenia walioathirika kwa saratani,”amesema Henrikh Mkhitaryan‏

Nyoso kupandishwa Kizimbani siku yoyote kuanzia Leo


Mlinzi wa timu ya Kagera Sugar Juma Said Nyosso anatarajiwa kupandishwa Mahakamani siku yeyote kutoka leo (Jumanne), kutokana na kutenda kosa la jinai wakati akitoka nje ya uwanja.

Hayo yamebainishwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, RPC Agustine Ollom na kusema bado wanamshikilia mchezaji huyo wa Kagera na endapo watakapomaliza mahojiano naye wanatarajia kumpeleka Mahamakani kwa ajili ya mashtaka yake.

"Bado mtuhumiwa yuko mahabusu anaendelea kuhojiwa na yule majeruhi yupo hospitali kwa hiyo tunategemea madaktari wakatakavyo kuwa wamepita hii 'round' ya asubuhi watatupa hali yake jinsi anavyoendelea. Juma Nyoso amefanya kosa la jinai hivyo sisi tutampeleka Mahakamani mapema itakavyowezekana na huko ndipo itakapojulikana kama alitenda kosa au laa na mwisho kutolewa adhabu juu yake", alisema RPC Agustine Ollom.

Juma Said Nyosso alikamatwa jioni ya jana (Jumatatu) baada ya mechi kumalizika dhidi ya Simba katika dimba la Kaitaba ambapo wachezaji wa Kagera Sugar walikuwa wanaelekea katika vyumba vya kubadilishia nguo kwa bahati mbaya mmoja ya mashabiki inasemekana alimpulizia vuvu zela Nyosso ndipo naye alipompiga shabiki huyo mpaka kupoteza fahamu.

Wafanyakazi walipwa mshahara wa matofali badala ya pesa


Wafanyakazi katika kiwanda cha matofali kusini mashariki mwa China wanaokidai kiwanda hicho mishahara yao yenye thamani ya $14,050, wamelipwa matofali, inaripotiwa.

Kwa mujibu wa shirika la habari Xinhua, takriban wafanyakazi 30 wa kiwanda hicho huko Nanchang, katika jimbo la Jiangxi , walikubali kulipwa matofali 290,000 badala ya mshahara wanaodai.

Gazeti la Jiangxi Daily linaripoti kuwa wafanyakazi hao , wote wakiwa ni wahamiaji , wametoka katika eneo la milima la jimbo la Yunnan kuini magharibi, na hawakuwa na namna ili kuishi kwa "kutumia mishumaa na kuwasha kuni moto ili kupunguza baridi ".

Baada ya chama chao cha wafanyakazi kuingilia kati na kwa usadizi wa mahakama, wafanyakazi hao walikubali kupokea matofali hayo kutoka wamiliki wa kiwanda badala ya mshahara wao ambao hawajalipwa.

Xinhua linasema kuwa waajiri wao, ambaye hakutajwa jina katika vyombo vya habari, bado anajaribu kutafakari namna ya kuwalipa, tofuati iliosalia ya Yuan 10,000 wanaodai wafanyakazi hao.

Taarifa hii imezusha mjadala mkubwa katika mitandao ya kijamii China, huku wengi wakielezea wasiwasi wao kuhusu ni kwanini mara kwa mara wafanyakazi wa vijijini wahamiaji ndio hulipwa kidogo kidogo?

Wengine wametania wakisema hali imekuwa mbaya kiasi cha matofali kuonekana kuwana thamani sawana fedha.

Je wewe ungekubali kulipwa mshahara wako kwa bidhaa nyingine yoyote kando na pesa taslimu?

Kamanda wa Polisi aweka bayana chanzo cha aliyegongwa na Ndege


KAMANDA wa Polisi wa Viwanja vya Ndege nchini, Matanga Mbushi, ameweka bayana chanzo cha mwanamke aliyegongwa na ndege ya Fastjet jijini Mwanza na kufariki dunia kuwa alikuwa na matatizo ya akili.

Akizungumza na Nipashe jana, Kamanda Mbushi alisema hadi sasa wameshindwa kubaini jina la mwanamke huyo ambaye alifariki dunia papo hapo baada ya kugongwa na ndege.

Ajali hiyo ilitokea katikati ya wiki iliyopita usiku kwenye Uwanja wa Ndege wa Mwanza, ulioko wilayani Ilemela.

Ndege hiyo ilimgonga mwanamke huyo akiwa anavuka kwenye njia ya kurukia ndege  wakati ndege hiyo yenye namba za usajili 58S-EJE190 ikiwa kwenye mwelekeo wa kuruka.

Alipoulizwa jana kama mwanamke huyo amefahamika na hatua gani zinachukuliwa ili tukio hilo lisitokee tena, Kamanda Mbushi alisema wanaopaswa kuzungumzia hilo ni Mamlaka ya Usalama wa Anga (TCAA).

“Yule mwanamke bado hatujapata jina lake, lakini inavyoonekana kuwa alikuwa na matatizo ya akili,” alisema.

Akizungumza na gazeti hili Ijumaa iliyopita, Kamanda huyo alisema wakati ndege hiyo ikiwa kwenye mwelekeo wa kuruka, mwanamke huyo alikuwa anakatiza kwenye njia ya ndege ndipo alipogongwa na kufa papo hapo.

“Ndege hii ilikuwa kwenye mruko wa futi 148 tokea pointi 12 kuelekea pointi 30 ikiwa na abiria 89 waliokuwa wakitoka Mwanza kwenda Dar es Salaam,” alisema.

Alisema pamoja na ajali hiyo, ndege hiyo iliruka na kusafiri salama hadi Dar es Salaam.

Matukio ya ndege kugonga mtu ni nadra kutokea duniani kwa mujibu wa utafiti wa Nipashe, lakini ajali inayokaribiana na ya Mwanza ni ile iliyotokea katika jimbo la California, Marekani Aprili 3, 2016.

Katika ajali hiyo, mtu mmoja alifariki baada ya ndege ndogo kuangukia gari lililokuwa barabarani.

Mashuhuda, kwa mujibu wa Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), walisema ndege hiyo ilionekana kama ilikuwa na matatizo ya injini na ikalazimika kutua kwa dharura kwenye barabara ya magari.

Rubani wa ndege hiyo aliyetajwa kuwa Dennis Hogge, alishindwa kuidhibiti na ikateleza na kugonga gari lililokuwa na watu wanne lililokuwa limeegeshwa kando ya barabara hiyo, ili dereva azungumze kwa simu.

Mtu mmoja alifariki dunia hapo hapo huku wengine watatu wakipelekwa hospitalini. Mtu aliyefariki dunia, Antoinette Isbelle (38), kutoka mji wa San Diego alikuwa ameketi nyuma katika gari hilo lililogongwa.

Katika hali ya kushangaza, haikuwa mara ya kwanza kwa ndege hiyo kutua kwenye barabara hiyo ya San Diego.

Mwaka 2000 mmiliki wa kwanza wa ndege hiyo alipatwa na hitilafu ya kimitambo na akalazimika kutua ndege aina ya Lancair 1V, kwenye barabara hiyo hiyo, BBC iliripoti.

Hata hivyo, tukio hilo halikusababisha maafa wala uharibifu wa ndege hiyo.