Sunday, 19 November 2017

Aliyezikwa akidaiwa mtu mzima abainika kuwa ni mwanafunzi aliyekuwa amepotea

Aliyezikwa akidaiwa mtu mzima abainika kuwa ni mwanafunzi aliyekuwa amepotea



Kama ni kuumbuka, basi walioidhinisha kuzikwa kwa maiti iliyodaiwa kuwa ni ya mtu mzima na mwenye ndevu, wameumbuka; maiti hiyo ni ya Humphrey Makundi, mwanafunzi wa kidato cha pili wa Shule ya Scolastica ya Himo wilayani Moshi.

Hayo yalibainika baada ya kutekelezwa kwa amri ya kufukua maiti hiyo iliyotolewa na Hakimu Idan Mwilapo wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi na baadaye kufanyiwa uchunguzi. Uchunguzi umebaini kuwa maiti hiyo ni ya mtoto na hakuwa na ndevu.

Amri ya kufukua maiti hiyo ilitolewa baada ya Jamhuri kuwasilisha maombi kupitia kwa Wakili wa Serikali, Ignas Mwinuka ukitaka mwili uliozikwa na Halmashauri ya Manispaa ya Moshi Novemba 12 kwa kukosa ndugu ufukuliwe.

Maombi hayo yaliwasilishwa mahakamani juzi yakiambatanishwa na kiapo cha Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Kilimanjaro (RCO), Doto Mdowe na Mahakama iliridhia ombi hilo.

Mwanafunzi huyo alitoweka shuleni katika mazingira ya kutatanisha Novemba 6 na baadaye mwili wake ukaokotwa Mto Ghona, umbali wa mita 300 kutoka shule hiyo.

Kutokana na mwili huo kuharibika, polisi na daktari waliufanyia uchunguzi wa awali na kueleza kuwa haukuwa wa mtoto huyo bali ni wa mtu mzima na kuruhusu halmashauri kuuzika.

Ingawa haielezwi katika shauri hilo ni nani aliyetoa hoja mwili huo ufukuliwe, lakini RCO katika kiapo chake alitaka ufukuliwe ili uchunguzwe kama ni wa Humphery aliyetoweka Novemba 6.

Watu 11 wakamatwa

Kamanda wa polisi mkoani Kilimanjaro, Hamis Issah alisema wanawashikilia watu 11, akiwemo mmiliki wa shule hiyo iliyopo mji mdogo wa Himo kwa ajili ya mahojiano.

Kwa mujibu wa Kamanda Issah, ingawa mtoto huyo aliondoka Novemba 6 kutoka shule hiyo iliyozungushiwa ukuta na walinzi na kwenda kusikojulikana, taarifa za kutoweka kwake zilitolewa polisi Novemba 11.

“Mtoto alitoweka shuleni tarehe 6.11.2017 wao wakaendelea na taratibu zao hadi tarehe 10.11.2017 ndio walizifikisha taarifa hizo polisi. Tulianzia uchunguzi papo hapo,” alisema.

“Katika hatua za awali za uchunguzi tulimkamata mmiliki wa shule kwa usalama wake kwa sababu wazazi tayari walikuwa wanamtuhumu kuhusika na kifo cha mtoto wao.”

Kamanda Issah alisema wakati wakiendelea na uchunguzi, walipata taarifa kuwa kuna mwili wa mtu uliokotwa Novemba 7 na ukahifadhiwa Hospitali ya Mawenzi hadi Novemba 12 ukazikwa.

“Baada ya kupata taarifa ndipo tukaomba kibali cha kufukua huo mwili na wakati unafukuliwa wazazi walikuwepo. Nawahakikishia haki ya huyu mtoto haitapotea,” alisema.

Kamanda Issah hakutaka kuzungumzia kwa undani kuhusu kile kilichobainika katika uchunguzi huo, lakini alisema umefikia asilimia 50.

“Tunataka kujua ilikuwaje mwanafunzi akatoka shuleni na shule ina geti na ina walinzi. Hapo nje kuna mama lishe,” alisema kamanda huyo.

“Niwaonye wamiliki wa shule, wasimamie vizuri maisha ya wanafunzi.”

Mwili ulivyotambuliwa

Watu walioshuhudia ufukuaji wa mwili huo katika makaburi ya Karanga mjini Moshi juzi saa 8:30 mchana, walilieleza gazeti hili kuwa baba mzazi wa mtoto huyo, Jackson Makundi aliishiwa nguvu na kuanguka.

Taarifa zinasema kabla ya ufukuaji kuanza, maofisa wa polisi walimuuliza mzazi huyo ataje alama zitakazomfanya amtambue kuwa huyo ni mwanaye naye alitoa alama mbili ambazo ni jino moja kukatika nusu na kidole kimoja cha mkononi kuwa na kucha iliyong’oka, alama ambazo zilionekana.

“Baada ya mwili kufukuliwa na baba na ndugu wengine kutambua alama alizozisema, yule baba aliishiwa nguvu na kukaa chini ikabidi aondolewe eneo lile,” alisema mmoja wa walioshuhudia tukio hilo.

Kwa mujibu wa mtu aliyeshuhudia uchunguzi huo, mwili wa mtoto huyo umekutwa na jeraha kwenye fuvu la kichwa ikiashiria alipigwa na kitu kizito kichwani.

Mwili wa mtoto huyo umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC.

Alichosema baba mzazi

Jackson Makundi, baba mzazi wa mtoto huyo amedai kuna mchezo uliofanywa baina ya uongozi wa shule na polisi wa Himo ili kuficha ukweli kuhusu ukatili aliofanyiwa mtoto wake.

Akizungumza na gazeti hili kwa simu jana, baba huyo alidai alipewa taarifa za kupotea mwanawe Novemba 8, ikiwa ni siku mbili baada ya kudaiwa ametoweka shuleni katika mazingira ya kutatanisha.

Makundi alidai taarifa ambazo baadhi ya walimu wanazitoa kuhusu kutoweka kwa mwanafunzi huyo zinatofautiana na taarifa za wanafunzi.

“Baada ya mwili kufukuliwa nilijiridhisha kwa asilimia 100 kuwa mtoto ni wangu kutokana na kwamba vichwa vyetu vinafanana na nyuso zetu,” alisema.

Alidai taarifa alizozipata kutoka kwa wanafunzi wenzake ni kwamba mtoto wake aliondoka shuleni akiwa amevaa bukta, fulana na soksi.

Makundi amehoji iweje mwanafunzi atoweke shule halafu apewe taarifa baada ya siku mbili, wakati shule hiyo ina ulinzi na utaratibu mkali wa kuingia na kutoka.

“Ninaamini na dhamira ya moyo wangu inanituma kuamini uongozi wa shule na polisi wa kituo cha Himo wana jambo wanalificha kuhusu kifo cha mtoto wangu,” alisema.

Hata hivyo, alimpongeza Kamanda Issah na wasaidizi wake kwa namna wanavyompa ushirikiano katika uchunguzi, akiamini kila kitu kitajulikana.

Maswali kuhusu uchunguzi

Tangu kufukuliwa kwa mwili huo na kubainika ni wa Humphrey, kumeibuka maswali kuhusu namna polisi na daktari wa Hospitali ya Mawenzi walivyoruhusu mwili uzikwe.

Taarifa kutoka eneo ambalo mwili huo uliokotwa zilidai polisi hawakupiga picha pande zote za mwili huo ili iwe rahisi kwa mtu yeyote kuutambua.

Imeelezwa polisi walitafuta picha na kupata kutoka kwa mwananchi aliyezipiga kwa kutumia simu zikionyesha mwili huo ukiwa umelala kifudifudi.

“Ndiyo maana ukitazama polisi siku mwili unaokotwa wana picha moja ya marehemu akiwa amelala kifudifudi. Huu ndio utaratibu wa kiuchunguzi?” Alihoji mmoja wa wajumbe wa Serikali ya Mji wa Himo.

Swali jingine ambalo baadhi ya watu wamekuwa wakihoji ni jinsi polisi na daktari wa Hospitali ya Mawenzi walivyoruhusu mwili huo uzikwe wakidai ni wa mtu mzima mwenye ndevu wakati ni wa mtoto.

Pia, wanahoji ilikuwaje mwanafunzi atoweke shuleni tangu Novemba 6, lakini taarifa za kutoweka kwake zikafikishwa polisi siku tano baadaye.

Swali jingine ni kwanini polisi waliofika mahali sehemu ulipookotwa mwili huo, hawakuchukua sampuli za vipimo vya vinasaba (DNA) ili atakapojitokeza ndugu, waweze kuoanisha.

Utaratibu unataka maiti isiyojulikana inapookotwa yatolewe matangazo katika maeneo yote ya jirani, lakini katika tukio hilo, mwili ulichukuliwa na kupelekwa hospitali na baadaye kuzikwa.

Mwananchi

Yanayojiri nchini Zimbabwe




Baada ya jeshi kuchukua utawala nchini Zimbabwe,mkutano wa pili untarajia kufanyika kwa ajili ya kumshauri rais Robert  Mugabe kuyaachia madaraka.

Kwa mujibu wa habari,katika mkutano ujao padri wa Katoliki Fidelis Mukonor,Waziri wa Ulinzi Aaron Nhepera na msemaji wa Mugabe George Charamba watahudhuria.

Ripoti zimeonyesha kuwa wananchi wamekuwa wakikusanyika barabarani wakimtaka rais Mugabe ajiuzulu.

Toka Jumatano jeshi kuu la Zimbabwe limechukua utawala wa nchi hiyo mpaka pale hatma itakapojulikana.

CCM walia kufanyiwa fujo na upinzani K'njaro

CCM walia kufanyiwa fujo na upinzani K'njaro


Wakati kampeni za udiwani zikiendelea katika maeneo mbalimbali nchini, Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoani Kilimanjaro kimedai kufanyiwa fujo na wafuasi wa upinzani pindi wafuasi wao wanapomaliza mikutano yao.

Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki na Katibu wa chama hicho mkoani hapa, Jonathan Mabihya katika mkutano wa kampeni za marudio ya uchaguzi wa udiwani Kata ya Bomambuzi.

Mabihya aliliomba Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua za kisheria wafuasi hao wa upinzani, huku akiwasisitiza wanachama wa CCM kutowajibu kwa fujo.

Katibu huyo aliwataka wanachama wote wanaoshiriki kwenye kampeni kufanya siasa safi na kunadi sera za chama hicho kwa kuzingatia sheria ikiwamo kufuata kanuni.

Pia, Mabihya aliwataka wananchi wa Kata ya Bomambuzi kutokubali kudanganywa kwa kilo moja ya nyama na sukari wanazopewa na wapinzani ili kuuza kura zao, badala yake wafanye uamuzi sahihi wa kuchagua kiongozi atakayewatumikia.

Pia, katibu huyo aliliomba jeshi la polisi mkoani Kilimanjaro kuingilia kati suala hilo akidai limekuwa likiwafifisha wafuasi wa chama hicho kushiriki katika mikutano yao kwa kuhofia kufanyiwa fujo.

Katibu msaidizi wa oganizesheni ya chama hicho, Steven Kazidi aliwataka wakazi wa Bomambuzi kutunza shahada zao za kupigia kura kwa ajili ya Novemba 26.

Aliwataka wananchi kutodanganyika na wapinzani kwa madai kwamba maendeleo yaliyopo wameyaleta.

“Wapo wanaopita majukwaani na kujitapa kuwa wao ndiyo wamewezesha maendeleo kwenye halmashauri zilizopo chini yao, ila si kweli, ukweli ni kwamba chama tawala ndicho kinachotoa fedha, kinatambua katika halmashauri kuna wananchi wao,” alisema Kazidi.

Aliwashauri wananchi kutokumchagua kiongozi kwa kuangalia fedha wala kabila bali wamchague mgombea wa CCM ili aweze kuwaletea maendeleo na kusimamia ilani ya uchaguzi inayoongoza dola.

Mgombea udiwani kupitia chama hicho, Juma Rahibu aliwataka vijana kutokubali kutumika na viongozi wa vyama vya siasa kwa lengo la kuhatarisha amani ya nchi.

Aliwashauri vijana kuungana ili kuhakikisha wanaleta maendeleo katika kata ya Bomambuzi.

Pia, aliwataka wakazi wa eneo hilo kuwa na msimamo katika shughuli za maendeleo huku akiahidi kuhakikisha anasimamia ilani ya uchaguzi pindi watakapompa ridhaa ya kuongoza.

“Mimi ni kijana mwenzenu, mkinichagua nitasimamia ilani ya chama changu pamoja na kuhakikisha asilimia tano zinazotengwa na halmashauri kwa ajili ya vijana zinawafikia vijana wote ndani ya kata hii,” alisema Rahibu.

Mwananchi.


Watu 19 wapoteza maisha kwenye ajali ya moto



Moto umeripotiwa kuteketeza jumba moja Pekin na kusababisha vifo vya watu 19.

Kwa mujibu wa habari,moto huo umetokea katika mji mkuu wa Pekin na kupelekea watu wengine nane kujeruhiwa.

Polisi wamekamata wale wote walioshtukiwa kuhusika na moto huo.

Majeruhi wamefikishwa hospitali haraka iwezekanavyo.

Uchunguzi zaidi wa chanzo hasa cha moto huo unafanyika.

Kumbe Dk Shika anajuana na Abromovich, ni shabiki wa Chelsea

Kumbe Dk Shika anajuana na Abromovich, ni shabiki wa Chelsea



Yule ' Bilionea wa nyumba za Lugumi'  Dk Louis Shika ambaye hivi karibuni alisema kuwa ni shabiki wa Chelsea kwa kuwa mmiliki wa klabu hiyo, Roman Abramovich ni rafiki yake, amefafanua zaidi.

Shika ambaye kitaaluma ni Daktari amesema kwamba, alikuwa akikutana na Abramovich mara kadhaa katika mikutano ya wadau.

Amesema kwa kuwa yeye ni mmiliki wa kampuni ya masuala ya kilimo, walikuwa wakikutana na Abramovich mara kwa mara katika mikutano ya viwanda.

“Mimi nilikuwa ninashughulika na masuala ya kilimo na yeye masuala ya mafuta. Sasa kule Urusi kuna kawaida ya makampuni kukutana.

“Kunakuwa na mikutano ya kuwakutanisha wamiliki kujadili mambo mbalimbali. Unajua kilimo pia kinahitaji mafuta na wauza mafuta wanawahitaji watu wa kilimo na makampuni mengine. Sasa pale nilikuwa ninakutana naye (Abramovich).

“Niliposikia kuwa yeye ndiye mmiliki wa Chelsea, basi nikaanza kuifuatilia na mwisho nikawa naipeda,” alifafanua



Yanga yasema mechi itakuwa ngumu lakini watapambana



Kocha mkuu wa Yanga George Lwandamina amesema mechi yao ya raundi ya 10 ligi kuu soka Tanzania bara dhidi ya Mbeya City itakuwa ngumu lakini watapambana washinde.

Lwandamiza amesema ni lazima wajitahidi washinde mchezo huo utakaopigwa kwenye uwanja wa Uhuru leo jioni ili wasiachwe mbali na mahasimu wao Simba katika mbio za ubingwa.

“Tunaingia kwenye mchezo mgumu, lakini tutapigana tushinde, Mbeya City ni timu nzuri na kwa sababu imefungwa mechi mbili mfululizo leo watakuwa wakali sana, lakini tutajitahidi tushinde,”amesema Lwandamina.

Kwa matokeo ya ushindi wa bao 1-0 iliyopata Simba jana dhidi ya Tanzania Prisons yanainyima Yanga nafasi ya kukaa kileleni hata ikishinda leo. Simba sasa ina alama 22 ambazo haziwezi kufikiwa na Yanga yenye alama 17. Ili kuipiku Simba, Azam FC yenye alama 19 inahitaji kushinda mabao 13-0 dhidi ya wenyeji Njombe Mji FC leo jioni.

Mechi nyingie ya kukamilisha mzunguko wa 10 leo itapigwa Uwanja wa Manungu, Turiani mkoani Morogoro, Mtibwa Sugar wakiwakaribisha ndugu zao Kagera Sugar.

Ufaransa: Chama tawala chachagua kiongozi mpya

Ufaransa: Chama tawala chachagua kiongozi mpya




Chama tawala cha rais wa sasa Emmanuel Macron kimemchagua kiongozi wake mpya.

Kwa mujibu wa habari,ni miezi 19 toka chama hicho cha LREM(La Republique En Marche) kiundwe.

Msemaji wa serikali Christophe Castaner ndie amechaguliwa kama kiongozi mpya wa chama hicho.

Chama hicho kimefanya mkutano wake wa kwanza mashariki mwa mji wa Lyon.

Mgombea pekee wa nafasi hio, Castaner, 51, amechaguliwa kama kiongozi wa chama hicho na viongozi waliochaguliwa, mawaziri, watendaji wa chama na wanachama 200 wa chama.

Christophe Castaner hakuchaguliwa moja kwa moja na wanachama  380,000 wa LREM.

Atatumikia nafasi yake kwa muda wa miaka mitatu

Zanzibar kujenga Jengo jipya la Uwanja wa Ndege



Waziri wa Fedha na  Mipango Dkt Khalid Salum Mohamed (pichani) amesema ujenzi wa jengo jipya la uwanja wa ndege unatarajiwa kuanza tena  Disemba Mwaka huu chini ya ufadhili wa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China  kupitia Exim Bank.

Alisema ujenzi wa  jengo jipya ni miongoni mwa miradi  mitatu mikubwa ya maendeleo katika kukiimarisha kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani Karume kiliopo Kisauni ambacho kinaumuhimu mkubwa kwa uchumi wa  Zanzibar.

Hayo aliyasema katika ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango Vuga wakati akitoa taarifa kwa waandishi wa habari kuhusu changamoto zilizojitokeza ambazo zilisababisha kushindwa kukamilika ujenzi huo .

Alisema kutokamilika kwa muda mrefu jengo jipya la kuhudumia abiria kulipelekea changamoto ya kumudu kuhudumia ndege kubwa aina ya Code E kulingana na mahitaji ya sasa na uwezo wake wa idadi ya abiria wataohudumiwa kwa mwaka .

Aidha alisema utengenezaji wa jengo kuligana na mahitaji mapya ya shirika la usafiri wa anga la duniani (ICAO) na mkabala wake wa maeneo ya kuegesha ndege yaliojengwa kwa ufadhili wa benki ya dunia .

Alieleza kutokana na kadhia hiyo Serikali ililazimika  kuajiri mshauri maalumu kutoka kampuni ADPi kutoka ufaransa ili kuweza kuishauri vizuri juu ya utatuzi wa changamoto zilizobainika  .

Hata hivyo alisema marekebisho yaliyopendekezwa na kukubaliwa na Serikali yalipelekea kuongezeka kwa gharama za mradi kutoka dola 70.4 millioni hadi 128.7 million .

Alieleza gharama hiyo ni kwa ajili ya ujenzi wa jengo lenyewe eneo Zaidi la maegesho ya ndege la mita za mraba 38,000 na eneo la kuegesha gari za watumiaji wa uwanja ,abiria pamoja na wapokeaji abiria .

Waziri wa fedha alisema tatizo hasa lililojitokeza ni upatikanaji wa fedha za ziada ambapo awali Benki ya Exim ilitaka atafutwe mfadhili mwengine kwa kiasi hichi lakini baada ya mashauriano ya muda mrefu baina ya  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali  ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja  na Serikali ya Watu wa China hatimae walikubaliana kudhamini kwa mkopo wa kibiashara .

Alifahamisha kuwa kutokana  na jitihada kubwa za  Serikali na Rais wa Zanzibar  Dkt Ali Mohamed Shein Benki ya Exim ilikubali kudhamini mkopo wote wa kugharamia ujenzi huo kwa utaratibu wa mkopo nafuu.

“Benki ya Exim kwa sasa imekubali kudhamini gharama zote za dola 128.7 million kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo na kwa masharti ya  mkopo nafuu .“alisema Waziri .

Alifafanua kuwa tayari wiki hii Benki hiyo imeshamlipa mkandarasi madai yake ya dola 17.6 millioni kwa kazi ambazo ameshazifanya awali na kuidhinishwa na mshauri dola nyengine 17.6 millioni kwa kazi kama hizo lakini zenye dhamana mpya ya mkandarasi na tayari mkandarasi amelipwa jumla ya dola 35.2 millioni .

Nae Waziri wa Ujenzi Mawasiliano na Usafirishaji  Balozi Ali  Karume (pichani) alisema mradi huo unatarajiwa kutekelezwa kwa ufanisi mkubwa na kufanikiwa kwa wakati uliopangwa kwa muda wa miezi 18 hadi 20.

Aidha alisema Wizara ya Ujenzi na Mawasiliano itahakikisha inasimamia vizuri ujenzi huo na kuhakikisha inatatua matatizo madogo madogo yatakayojitokeza ili  lengo la serikali la kuhakikisha jengo hilo jipya la abiria linauwezo wa kuchukua abiria 1,
200,000 mpaka 1,600,00 kwa mwaka .

Hata hivyo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweza kuwashukuru Wananchi wa eneo la Chukwani   kwa ustahamilivu wao na imani yao kwa muda wote wakati serikali ikilitafutia ufumbuzi suala la mradi huo

Mugabe kukutana na makamanda wa jeshi leo



 Washirika wa karibu wa Rais Robert Mugabe kwenye chama alichokianzisha wanamtaka ajiuzulu wakati shinikizo dhidi yake zikiongezeka kufuata hatua za jeshi kutwaa madaraka.
Maafisa wa vyeo vya juu chamani wameanza kuwasili kwenye mkutano wa Zanu PF, ambapo watajadili ikiwa watamtimua chamani Mugabe.

Kitengo cha vijana wa chama ambacho awali kilkuwa mtiifu kwake Mugabe sasa kimemgeuka.
Nao makamanda wa jeshi wanatarajiwa kukutana na Mugabe baadaye leo.

Mkuu wa chama chenye nguvu cha wale waliopigania uhuru Chris Mutsvangwa, aliiambia Reuters kuwa Bw Mugabe anawea kuondolewa kutoka uongozi wa chama mke wake kupokonywa wadhifa wa mku wa kitengo ya wanawake.

Bw Mugabe amekuwa akizuiliwa nyumbani tangu jeshli litwae madaraka siku ya Jumatano.
Jeshi lilingilia kati baad ya Mugabe 93, kumfuta makamu wa rais Emmerson Mnangagwa.

Maelfu ya watu wakiwemo kutoka chama tawala na upinzani waliingia mitaani siku ya Jumamosi kushrehekea hatua ya jeshi na kumtaka Mugabe ang'atuke


Wanajeshi walidhibiti kituo kikuu cha matangazo cha serikali siku ya Jumatano.
Afisa mmoja wa jeshi jenerali Sibusiso Moyo, kisha akasoma taarifa kwenye televisheni akiihakikishia nchi kuwa Mugabe na familia yake walikuwa salama.

Jeshi linasema kuwa likuwa likiwalenga waalifu wanaomzunguka Mugabe na kukana kuwa hayo sio mapinduzi ya kijeshi.
Ijumaa Mugabe alionekana hadharani kwa mara ya kwanza tangu aweke nchini ya kuzuizi cha nyumbani na jeshi, wakati alihudhuria sherehe za kufuza kwenye chuo cha Harare.

Hata hivyo Grace Mugabe hakuwa. Ilifikiriwa kuwa alikuwa ameondoka nchini humo lakini iliiibuka Alhamisi kuwa alikuwa nyumbani na Mugabe.


DC Handeni atoa onyo kwa wafugaji


Watendaji wa kata na vijiji wilayani Handeni mkoani Tanga, wameonywa na kutakiwa kuacha kuwaruhusu wafugaji kuingiza mifugo kwenye maeneo yao bila kufuata utaratibu. Atakaebainika kufanya hivyo atachukuliwa hatua za kisheria.

Onyo hilo limetolewa Novemba 18 na Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Godwin Gondwe, wakati akizindua zoezi la upigaji chapa mifugo (ng’ombe) wilayani humo katika kijiji cha Sua.

Gondwe amesema zipo taarifa kuwa kuna watendaji wa kata na vijiji bado wanapokea mifugo kinyemela.

Mkuu huyo wa wilaya alisema zoezi la kupiga chapa mifugo hiyo litasaidia kubaini mfugo katika kila eneo kutokana na alama zinazowekwa.

Alisema zipo taratibu za kupokea mifugo hivyo ni vizuri zifuatwe ili kuweza kuibaini mifugo ambayo inaweza kuingia na magonjwa na kusababisha maambukizi ya magonjwa.

Akielezea dhumuni ya zoezi hilo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Handeni, William Makufwe, alisema hikolo ni zoezi la kitaifa lililoagizwa kutoka ngazi za juu likiwa na nia ya kuondoa migogoro ya mara kwa mara, hivyo ni muhimu wafugaji wote kushiriki.

Alisema kwa halmashauri ya Handeni zaidi ya ng’ombe 30,000 wanatarajiwa kupigwa chapa ili iwe rahisi kutambuliwa, kuweza kusajiliwa na  kudhibiti mifugo iliyopo wilayani humo.

Aidha, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Handeni, Athumani Malunda, amewataka wafugaji kuepuka migogoro na wakulima kwa kulisha mifugo yao kwenye mashamba huku wakitoa lugha za maudhi  kwa wenzao.

Mmoja wa wafugaji mkazi wa Mkata, Omari Bigo, ameipongeza serikali  kwa kuendesha zoezi hilo na kusema kuwa litasaidia udhibiti wizi wa mifugo.

Serikali wilayani Handeni imetoa siku 45 hadi Disemba 31 kwa wafugaji wote kuhakikisha wamepeleka ng’ombe wao kupigwa chapa na atakayeshindwa kufanya hivyo atatozwa faini isiyozidi Sh1 milioni kwa kukiuka agizo.

Mwananchi.



Barnaba uzalendo umemshinda Mama Steve



Mwanamuziki anayefanya poa kwenye game ya Bongofleva Barnaba Classic ameshindwa kujizuia kwenye siku ya kuzaliwa mama wa mtoto wake Zuwena ambaye kwa sasa hawapo pamoja kwa kumshukuru kuwepo na kumpatia zawadi ya mtoto.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram Barnaba amesema kwamba upendo wake juu ya zawadi mwanadada huyo aliyempati ipo palepale na kusisitiza kwamba anamuheshimu huku akimsisitizia kwamba anapenda kumuona akiwa furaha.

"Wewe ni rafiki Yangu na ndugu yangu Uvungu wa moyo wangu unakushukuru kwa kuwa daraja kwenye maisha yangu na nashukuru nimevuka salama matatizo ni sehemu ya kila mwanadamu upendo wangu juu ya zawadi uliyonipatia Iko pale pale/STEVE Na Kitu kizuri ninakuheshimu Sana mbali Na mambo Yote Na Kitu kingine Furaha Yangu kuona unaendela Kutabasamu Hata kama ilo Tabasamu Silitengenezi Mimi," Barnaba

Aidha Barnaba ameongeza kwamba anamtakia kila la kheri mwanadada huyo ambaye tayari amekwishaingia kwenye mahusiano na kumwambia anapenda yeye awe shuhuda wa maisha ya mzazi mwenzake huyo kwa kila jambo.

"Nakutakia maisha mema yenye baraka, nawaombea heri Katika Familia yako, nakuombea heri na uwahi uwe shuhuda wangu nami niwe shuhuda wako wa kila jambo heri ya siku yako ya kuzaliwa mzazi mwenzangu mama yake Steve, Zuunamela mama watoto ! Damu Ya yesu ikuangazie Amina,"  Barnaba

Mtanzania mwingine afuzu majaribio timu ya AFC ya Sweden

Mtanzania mwingine afuzu majaribio timu ya AFC ya Sweden



Kiungo mshambuliaji Rashid Chambo ,17, amefuzu kucheza kuitumikia timu ya AFC ya Sweden.

AFC ndiyo timu anayofanya majaribio Mtanzania, Said Hamis Ndemla.

Chambo kutoka JKT Ruvu alikwenda kufanya majaribio katika timu hiyo mwezi uliopita na sasa amefuzu.

Pamoja na kufuzu timu ya vijana, kocha amependekeza awe anapewa nafasi katika timu ya wakubwa.

“Kocha kaona ana kipaji, hivyo atakuwa akitumiwa pia na timu ya wakubwa. Lakini timu ya vijana inapokuwa na mechi, basi anakwenda kucheza,” kilieleza chanzo kutoka Sweden

Mbowe kumnadi mgombea aliye mahabusu

Mbowe kumnadi mgombea aliye mahabusu



Wakati Mwenyekiti wa Chadema,  Freeman Mbowe akitarajiwa kuwahutubia wakazi wa Kata ya Mhandu katika kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani, mgombea wa chama hicho, Godfrey Misana yupo mahabusu kutokana na kukabiliwa na shitaka la kujeruhi.

Katibu wa Chadema Mkoa wa Mwanza, Boniphace Nkobe  amesema Mbowe ameambatana na aliyekuwa mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu.

Amesema mkutano huo pia utahudhuriwa na aliyekuwa mbuge wa Nyamagana, Ezekia Wenje na utafanyika saa kumi jioni.

Misana (46), mgombea udiwani wa Chadema katika uchaguzi mdogo utakaofanyika Novemba 26,2017 na kampeni meneja wake, Charles Chinjibela (37) Ijumaa Novemba 17,2017 walipandishwa kizimbani wakidaiwa kumjeruhi meneja wa kampeni za CCM katika kata hiyo, Thomas Warioba.

Katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza, mbele ya hakimu Ainawe Moshi wanadaiwa kutenda kosa hilo Novemba 14,2017.

Akisoma mashtaka katika shauri hilo namba 540/2017, mwendesha mashtaka wa Jamhuri, Elizaberth Barabara alidai washtakiwa walitumia visu na mawe kumjeruhi Warioba.

Upande wa Jamhuri uliomba Mahakama kuzuia dhamana ya washtakiwa kwa kile ilichoeleza ni kwa usalama wao.

Ombi hilo la Jamhuri limepingwa na wakili wa utetezi, Gasper Mwanaliela.

Wakili Mwanaliela alisema dhamana ni haki ya wateja wake na kwamba, kuwanyima kutawazuia kushiriki kikamilifu katika kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani unaotarajiwa kufanyika Novemba 26,2017.

Baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili, Hakimu Moshi alisema Mahakama itatoa uamuzi kuhusu dhamana Novemba 21,2017. Washtakiwa walipelekwa mahabusu