Tuesday, 26 December 2017

Amana yaongoza kwa idadi kubwa ya watoto waliozaliwa krismas



Dar es Salaam. Watoto 102 wameripotiwa kuzaliwa katika hospitali mbalimbali nchini wakati wa mkesha wa sikukuu ya Krismasi. Dar es Salaam wamezaliwa 50, Kanda ya Ziwa 29, Arusha 18, na Handeni mkoani Tanga watano.
Hospitali ya Amana ndiyo iliyokuwa na idadi kubwa ya watoto waliozaliwa na Ofisa Muuguzi wa zamu, Agnes Simon alisema kati ya watoto 32, watano waliozaliwa kwa upasuaji.
Alisema afya za watoto hao ni njema na baadhi yao huenda wakaruhusiwa kurudi nyumbani.
“Hakuna mtoto mwenye tatizo, wote wana afya nzuri, hata wazazi wao wanaendelea vizuri pia, hivyo tunatarajia kuwaruhusu wakasherehekee sikukuu nyumbani,” alisema Agnes.
Kaimu Mkuu wa Jengo la Wazazi Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Mariam Mlawa alisema jana kwamba watoto waliozaliwa hospitalini hapo wana afya njema na wanaendelea vizuri na idadi hiyo haijapishana na waliozaliwa katika mkesha wa Krismasi mwaka jana.
Alisema kina mama sita walijifungua na kati yao, wawili kwa upasuaji na wengine kwa njia ya kawaida. Pia kati yao, wawili wamejifungua watoto pacha.
“Tunashukuru watoto wote wapo vizuri, mama zao pia wapo vizuri na kwa hawa waliojifungua kwa njia ya kawaida huenda wakaruhusiwa muda wowote,” alisema Mlawa.
Ofisa Muuguzi Kiongozi katika Hospitali ya Temeke Rashidi Nyombiage alisema watoto 12 walizaliwa kwa njia ya kawaida na kwamba hakuna aliyejifungua kwa njia ya upasuaji.
“Hatukupata pacha, watoto wote walizaliwa mmojammoja na hakuna mtoto mwenye tatizo lolote wote wanaendelea vizuri na afya zao pamoja na mama zao zinazidi kuimarika,” alisema Nyombiage.
Katika Kanda ya Ziwa, watoto 16 walizaliwa katika Hospitali ya Mkoa ya Sekou Toure. Muuguzi msimamizi wa zamu, Rhoda Lissu alisema kati ya hao wa kike ni 10 na wakiume sita.
“Watoto wawili kati ya hao wamezaliwa kwa njia ya upasuaji, lakini tunamshukuru Mungu wapo salama na afya za mama zao zipo vizuri, “ alisema Rhoda.
Wilayani Serengeti, muuguzi mkuu wa Hospitali ya Teule ya Nyerere, Neema Machara alisema watoto watatu wa kiume walizaliwa kwa njia ya kawaida.
Arusha, watoto 18, walizaliwa katika Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru.
Mganga mfawidhi wa hospitali hiyo, Jackline Urio alisema kati yao 12 ni wa kiume.
Akizungumza jana, Mwamvua Barua mkazi wa Mtoni Kijichi aliyejifungua Muhimbili alisema hakutarajia maishani mwake kujifungua katika siku hiyo akisema atamlea mtoto wake huyo aliyempa jina la Emmanuel katika maadili.
“Huyu ni mtoto wa pili na wote nimewazaa mwezi wa 12, ila uzao huu umeangukia kwenye mkesha wa sikukuu,” alisema.

Miradi Mikubwa itakayo kumbukwa mwaka 2017



Dar es Salaam. Mwaka 2017 ukielekea ukingoni, miradi mikubwa saba itaendelea kuutaja kila itakapikuwa ikizungumziwa.
Miradi hiyo ni ujenzi wa bomba la mafuta, uboreshaji Bandari Dar es Salaam, upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), ujenzi wa reli ya kisasa (Standard Gauge) na ujenzi wa Daraja la Furahisa, Mwanza, bandari mpya ya Bagamoyo na mradi wa kuzalisha megawati 2,100 za umeme wa Stiegler’s Gorge.
Ikiwa imetangaza kuzikaribisha taasisi zinazoweza kufanya utafiti wa namna ya kufanikisha azma ya uchumi wa viwanda, Serikali inatekeleza miradi hiyo mikubwa na kati yake ipo iliyofikia hatua za mwisho.
Bomba la mafuta
Agosti 5, Rais John Magufuli pamoja na mwenzake, Yoweri Museveni wa Uganda walizindua ujenzi wa bomba la mafuta ghafi kutoka Hoima hadi Bandari ya Tanga. Ajira zaidi ya 1,000 zinatarajiwa kupatikana katika mradi huo.
Bomba hilo lenye urefu wa kilomita 1,450 litapita katika mikoa minane ya Kagera, Geita, Shinyanga, Tabora, Singida, Dodoma, Manyara na Tanga. Ndani ya mikoa hiyo, bomba hilo litakalogharimu Sh8 trilioni, litapita katika vijiji 184 vilivyomo katika wilaya 24.
Mbali na ajira kwenye mradi huo, kutakuwa na fursa za kibiashara kwa wauzaji na wasambazaji wa vyakula na vifaa vya ujenzi.
Bomba hilo litajengwa na kuendeshwa na kampuni za Total ya Ufaransa, CNOOC ya China na Tullow ya Uingereza kwa ubia na Kampuni ya Taifa ya Mafuta ya Uganda (Unoc) na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).
Bandari ya Dar
Julai 2, ulifanyika uzinduzi wa kuboresha Bandari ya Dar es Salaam ambao unatekelezwa na Kampuni ya China Harbour Engineering Company (CHEC) utakaogharimu Sh336 bilioni ambazo ni mkopo kutoka Benki ya Dunia. Kazi hiyo inatarajiwa kukamilika baada ya miezi 36.
Uboreshaji huo unahusisha ujenzi wa gati jipya la kuhudumia magari pekee, uboreshaji wa gati namba moja hadi saba na kuongeza kina cha maegesho ya meli kutoka mita 8.2 hadi 15 na kina cha mlango wa bahari ili meli kubwa na za kisasa ziweze kufika katika bandari hiyo.
Upanuzi huo unatarajiwa kuongeza ufanisi wa Bandari ya Dar es Salaam hivyo kuiwezesha kuhudumia kiasi kikubwa cha mizigo hivyo kukuza uchumi.
Licha ya kuboreshwa kwa miundombinu, huduma nazo zinatarajiwa kurahisishwa. Mamlaka zote zinazohusika na uondoshaji au usafirishaji wa mzigo zimetakiwa kuwa na ofisi bandarini hapo. Hizo ni pamoja na benki zote zinazopokea fedha za Serikali ambazo ni na tozo za aina tofauti zinazopaswa kulipwa.
Taasisi zote muhimu zimewekwa chini ya dirisha moja ili kupunguza muda wa kukamilisha mchakato huo na kuharakisha biashara kwa waagizaji wa ndani na nchi jirani zinazoitumia bandari hiyo.
Upanuzi JNIA
Katika kuimarisha usafiri wa anga kwa wasafiri wa ndani na kimataifa, Serikali inapanua uwezo wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), mradi huo unaotekelezwa na Kampuni ya Bam International ya Uholanzi, kwa gharama ya Sh560 bilioni.
Wakati upanuzi huo ukitarajiwa kukamlika mapema mwakani na kuongeza idadi ya abiria kutoka milioni 2.5 hadi milioni 6.4 kwa mwaka, Serikali pia inaimarisha Shirika la Ndege Tanzania (ATCL).
Ndege mbili zikiwa zimeanza kutoa huduma, nyingine nne zipo kwenye mpango wa kuwasili. Mpaka mwakani, Serikali imesema ndege zote zitakuwa zimewasili nchini ili kuimarisha usafiri wa anga na sekta ya utalii kwa ujumla.
Bandari mpya Bagamoyo
Baada ya kusuasua kwa muda mrefu, mwaka huu Serikali imekamilisha taratibu za ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo pamoja na eneo maalumu la uwekezaji (SEPZ). Tangu Oktoba 15, 2015 Rais mstaafu Jakaya Kikwete alipoweka jiwe la msingi la utekelezaji wa mradi huu, hapakuwa na uendelezaji.
Lakini Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage amesema taratibu zimekamilika na ujenzi utaanza Januari 2018. Utekelezaji wa mradi huo utaifanya Bagamoyo kuwa bandari kubwa zaidi Afrika Mashariki na Kati.
Utekelezaji wake utagharimu Dola 10 bilioni za Marekani (zaidi ya Sh22.3 trilioni), na waziri Mwijage alisema utafanywa kwa ushirikiano wa Kampuni ya China Merchants Holdings International (CMHI) ya China na State General Reserve Fund ya Oman. Eka 3,000 zimetengwa na viwanda 190 vinatarajiwa kujengwa kabla ya mwaka 2020.
Utakapokamilika, mradi huo utakuwa na viwanda 700 na kuufanya kuwa eneo la kimkakati kwa uwekezaji katika ukanda wa Afrika Mashariki na kuchangia kuinua uchumi wa Taifa.
Kwa mujibu wa taarifa za ujenzi huo, awamu ya kwanza itahusu meli kubwa zinazobeba hadi makontena 8,000 ya futi 20 hivyo kupunguza foleni ya meli za mzigo katika Bandari ya Dar es Salaam huku kukiwa na uwezekano wa kuitanua zaidi.
Stiegler’s Gorge
Mipango iliyomshinda Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na awamu tatu zilizofuata baada yake imewezekana hivi sasa. Agosti 30 Serikali ilitangaza zabuni ya ujenzi wa mradi mkubwa wa kuzalisha megawati 2,100 za umeme katika maporomoko ya maji ya Mto Rufiji (Stiegler’s Gorge).
Zaidi ya kampuni 80 zimejitokeza kuomba kutekeleza mradi huo unaoelezwa kwamba utapunguza uhaba wa nishati hiyo nchini na kuweka mazingira rafiki ya ujenzi wa viwanda. Utakapokamilika, utaifanya Tanzania kuwa na jumla ya megawati 5,000 ifikapo mwaka 2021.
Mradi huo unatekelezwa huku Wakala wa Nishati Vijijini (Rea) ukiwa unaendelea kusambaza umeme nchini. Mwaka jana, jumla ya vijiji 4,000 viliunganishwa. Pamoja na hiyo, mradi wa Kinyerezi I na II ipo kwenye hatua tofauti. Upanuzi wa Kinyerezi I uliokamilika kwa zaidi ya asilimia 50 unatarajiwa kuzalisha megawati 185 utakapokamilika wakati Kinyerezi II uliokamilika kwa zaidi ya asilimia 86 ukitegemewa kuzalisha megawati 250.
Ujenzi reli ya kisasa (SGR)
Ujenzi wa reli ya kisasa (Standard Gauge Railway) kutoka Dar es Salaam kwenda Kigoma na Mwanza tangu utekelezaji wake ulipoanza mwaka huu, unatarajiwa kuanza kufanyakazi baada ya miezi 36.
Ujenzi wa awamu ya kwanza kutoka Dar es Salaam mpaka Morogoro utakaogharimu Sh2.7 trilioni wa reli hiyo ya mwendo wa kasi ya kilomita 160 kwa saa, umeanza na utaifanya Tanzania kuwa ya pili kwa kasi hiyo baada ya Morocco.
Kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli Tanzania (Rahco) imetiliana saini mkataba wa ujenzi wa awamu ya kwanza ya reli hiyo na Kampuni ya Yapi Merkenzi Instant Ve Sanayi A.S ya Uturuki na Mota-Engil, Engenharia E and Construcao S.A ya Ureno kujenga kilomita 205 za njia kuu na kilomita 95 za kupishania.
SGR itakuwa na uwezo wa kusafirisha tani milioni 17 za mzigo ambalo ni ongezeko karibu mara mbili na nusu ya uzani uliopo.
Daraja la furahisha
Licha ya kujenga barabara zenye urefu wa kilomita 1,500 kwa kutumia Sh1.2 trilioni nchini kote mwaka huu, Serikali imekamilisha ujenzi wa Daraja Furahisha lililopo jijini Mwanza kwa kutumia Sh4.7 bilioni. Rais Magufuli alilizindua Oktoba 30.
Daraja hilo lina urefu wa mita 46, upana mita 3.6 na kimo cha mita 5.8 na njia za kuingia na kutoka zenye jumla ya meta 700. Fedha zilizotengwa kwa ajili ya sherehe za Muungano mwaka 2016 zilijenga daraja hilo baada ya kuzibadilishia matumizi.
Kujengwa kwa daraja hilo kumeokoa kwa kiasi kikubwa maisha ya wapita katika eneo hilo kwani lilikuwa na matukio mengi ya ajali.

Matukio ya Mauwaji yaliyotikisa Mwanza 2017



Mwanza. Tukiwa tunaelekea kuhitimisha mwaka 2017, mkoa wa Mwanza na viunga vyake vilitikiswa na matukio mbalimbali.
Miongoni mwa matukio yaliyobamba na kutikisa nyoyo za wakazi mkoani hapa ni vifo vya watu mbalimbali pamoja na mamilioni ya fedha ambayo idadi yake haikujulikana kuteketea ndani ya nyumba.
Juni 10 mwaka huu wakazi wa Mwanza waligubikwa na simanzi ya kifo cha milionea mmoja mkazi wa jiji la Mwanza, Maduhu Masunga (76) maarufu kwa jina la Mzee Shinyanga kuteketea kwa moto ndani ya nyumba aliyokuwa anaishi pamoja na mamilioni yake.
Mzee huyo inadaiwa alifariki dunia wakati anajaribu kuokoa mamilioni hayo ya fedha aliyokuwa ameyaficha ndani ya nyumba hiyo.
Taarifa iliyotolewa na Kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi ilisema thamani ya mali na fedha zilizoteketea katika ajali hiyo haijafahamika na kwamba jeshi la polisi lilikuwa linaendelea na uchunguzi kubaini kiasi cha fedha hizo.
Pamoja na kiasi cha fedha kilichokutwa ndani hakijaweza kujulikana, Meneja wa Idara ya Uchumi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Kanda ya Ziwa, James Machemba alisema kisheria fedha zote zinapaswa kuhifadhiwa kwenye taasisi za fedha ili zirejee kwenye mzunguko na hivyo kusisimua uchumi.
“Hata kama ni fedha zinazomilikiwa kihalali, ni kosa kisheria kuhifadhi kiasi kikubwa nyumbani; fedha zinatakiwa kuwa kwenye mzunguko na anayezihifadhi ndani anakwamisha maendeleo na uchumi wa Taifa,” alisema Machemba.
Akizungumza na gazeti hili akiwa nyumbani kwake mtaa wa Kirumba wilayani Ilemela, mke wa marehemu, Mariam Masanja (68) alisema pamoja na kuwa mzee huyo alikuwa akimiliki mali nyingi yakiwamo maghorofa na magari lakini hakuna hata mmoja aliyekuwa anajua kiasi cha fedha alichokuwa nacho na mahala alipoweka fedha zake.
Mke wa marehemu pamoja na baadhi ya watoto waliozungumza na gazeti hili kila mmoja alidai kuwa hafahamu ni kiasi gani cha fedha alichokuwa anamiliki.
“Mzee Shinyanga alikuwa anatoa mahitaji yote muhimu kwenye familia, ikiwamo kusomesha watoto lakini hatukuwahi kujua kama fedha zote zinakaa ndani tena kwenye ndoo, hadi pale siku ya tukio zilipobainika zimeteketea kwa moto,” alisema Mariam.
Majambazi wauawa Mwanza
Tukio jingine lililoibua hisia kwa wakazi wa Mwanza ni baada ya jeshi la polisi mkoani Mwanza kufanikiwa kuwaua majambazi sita katika mtaa wa Fumagila, kata ya Igoma jijini Mwanza.
Tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia Julai 8 mwaka huu baada ya majambazi hao kurushiana risasi na askari waliokuwa doria, hivyo kufanikiwa kuyaua huku wawili wakifanikiwa kutoroka.
Kutokana na tukio hilo, wakazi wa mtaa huo waliingiwa na hofu hivyo kusababisha shughuli zao za kila siku kusuasua.
Mauaji ya wanandoa
Mauaji ya wanandoa nayo yalileta taswira mbaya kwa wakazi wa mkoani Mwanza baada watu wawili wakazi wa mtaa wa Kanyerere, kata ya Butimba kuuana kwa risasi.
Tukio hilo lilitokea Mei 25, mwaka huu baada ya Maximilian Tula (40) kumuua kwa kumpiga risasi mkewe Teddy Malulu kabla ya yeye kujimaliza.
Chanzo cha mauaji hayo ni ugomvi kati yao.
Mbali na tukio hilo, matukio ya wanandoa kuuana yaliendelea baada ya wakazi wa kijiji cha Mwagiligili wilayani Sengerema, Kwilokeja Boniphace (35) kumuua mkewe Shija Luchagula (30) kwa kumpiga na kumnyonga kisha naye kujinyonga kwa kile kinachosemekana kuwa ni wivu wa mapenzi.
Matukio mengine yanayofanana na hayo zaidi ya saba yaliendelea kutokea katika maeneo mbalimbali mkoani humo.
Hiace yatumbukia ziwani
Oktoba 9 mwaka huu, wakazi wa mkoa wa Mwanza pia waliingiwa na simanzi kutokana na vifo vya watu 12 waliofariki dunia baada gari dogo la abiria maarufu kama daladala aina ya Toyota Hiace kutumbukia Ziwa Victoria katika Kivuko cha Kigongo wilayani Misungwi.
Baadhi ya majeruhi walitoka salama na kulazwa katika Kituo cha Afya Bukumbi.
Majeruhi Yohana Ngabula alisema ajali hiyo ilisababishwa na dereva kuwa kwenye mwendo mkali.
“Tulimshauri dereva asiendeshe kwa kasi lakini hakutusikiliza hali iliyosababisha gari kufeli breki na kusababisha vifo hivyo,” alisema Ngabula.
Mganga mfawidhi wa hospitali ya Bukumbi, Dk Robert Shija alithibitisha kupokea miili ya watoto watatu na watu wazima tisa.
Miezi mitatu baadaye watu watano walifariki dunia na wengine 13 kujeruhiwa katika ajali iliyotokea jijini Mwanza ikihusisha gari aina ya Coaster na lori eneo la Buhongwa.
Kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi alisema ajali hiyo ilitokea Desemba 16, saa 3:30 usiku katika barabara ya Mwanza-Shinyanga kata ya Buhongwa wilayani Nyamagana.
Wanawake wavishana pete
Tunaweza kusema kuwa ni tukio la funga mwaka baada ya jeshi la polisi mkoani hapa kuwatia nguvuni wanawake wawili waliodaiwa kuvishana pete za uchumba kinyume cha sheria.
Washtakiwa hao ambao ni, Milembe Suleiman (35) na Janeth Shonza (25) Mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino walifikishwa mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Gway Sumaye na kusomewa shtaka la kufanya vitendo vinavyoashiria mapenzi ya jinsia moja.
Wakili wa Serikali, Emmanuel Luvinga alidai kuwa washtakiwa hao walitenda kosa hilo Agosti 31 wakiwa katika Hoteli ya Pentagon jijini Mwanza, kinyume cha kifungu cha 138 A cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai sura ya 16 kama na marekebisho yake ya mwaka 2002.
Katika shauri hilo namba 548/2017, Wakili Luvinga alidai kuwa washtakiwa hao waligusanisha ndimi zao ikiwa ni shara ya kuwa na uhusiano wa kimapenzi kinyume cha sheria.
Aneth Mkuki (24) mkazi wa jijini Mwanza, naye alifikishwa mahakamani kwa shtaka hilo hilo na kifungu hicho hicho cha sheria baada ya kudaiwa kuwa mshereheshaji siku ya tukio hilo.
Mshtakiwa mwingine katika kesi hiyo ni Richard Fabian (28) Mkazi wa Buzuruga Mwanza yeye ameshtakiwa kwa kosa la kusambaza picha ya video za tukio hilo la kuvishana pete, kinyume na Sheria ya Mtandao Kifungu cha 20 Kifungu Kidogo cha (1) (a) cha Sheria ya Mitandao namba 14 ya mwaka 2015.
Wakili Jebra Kambole anayewatetea washtakiwa hao aliiomba mahakama iwape dhamana kwa sababu mashtaka yanayowakabili yana dhamana.
Ombi hilo lilikubaliwa na Hakimu Sumaye lakini akasema kwamba hawezi kutoa masharti ya dhamana kwa sababu shauri hilo lilipangwa kusikilizwa mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Wilbert Chuma ambaye hakuwapo.

TEHAMA yawanufaisha watoto




Maadhimisho ya tamasha la kufunga mwaka la TEHAMA yanayohusu kuwafundisha watoto elimu ya kompyuta kwa vitendo yamefanyika jijini Da es salaam yakiwa na lengo la kuonyesha kwamba watoto wakifundishwa kwa kufuata silabasi sahihi iliyowekwa na serikali inamafanikio kwa asilimia 100.
Akizungumza katika maadhimisho hayo Mkurugenzi Kiongozi wa mpango huo wa Tehama class, Rajab Mustafa amewataka wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao katika vituo vilivyo sehemu mbalimbali jijini Dar es salaam ili wapate elimu hiyo kwani watoto kuanzia darasa la kwanza hadi la tatu ni bure kwa siku ya jumamosi na juma pili inapotelewa elimu hiyo kulingana na ratiba za nasomo.
Aidha katika mpango huo watoto watapata elimu ya kompyuta kwa vitendo ikiwa ni dhamira ya kufanya watoto waelewe kuhusu Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.
''Tunawafundisha Ngamizi ili baadae watakapojiendeleza na elimu zao wapate kuelewa kuhusu teknolojia pia waweze kujiajili'' Alisema Mustafa

Barnaba Kufanya Kolabo Na Ben Pol



MKALI wa Bongo Fleva, Elias Barnaba amefunguka kuhusu kufanya kolabo la maana na msanii mwenzake Ben Pol, mwakani 2018. Akizungumza na Full Shangwe, Barnaba alisema kuwa, Mungu akibariki, watafanya kolabo moja ya ukweli mwakani.
“Kikubwa ni kumshukuru Mungu na kumuomba atufikishe salama lakini naamini kolabo langu na Ben Pol litakuwa ni la hatari sana, maana mafundi wanakutana, unadhani nini kitatokea kama siyo nyasi kuwaka moto,” alisema Barnaba.

Ali Choki afunguka Sababu ya mashabiki kupungua kwenye maonyesho ya Muziki



MWANAMUZIKI nguli wa muziki wa dansi nchini, Ally Choky amesema kuwa kukaza kwa vyuma kumesababisha mashabiki wengi kutohudhuria kwenye maonyesho mbalimbali ya muziki.
Choky ambaye ni Mwanamuziki wa Bendi ya The African Stars ‘Twanga Pepeta’, amesema kwa sasa hali ni mbaya katika bendi karibu zote.
“Ukitaka kujua kuwa vyuma vimekaza, wewe angalia shoo nyingi hazina mashabiki kama zamani. Sisi kama Twanga Pepeta tunaendelea kupambana na hali yetu hadi kieleweke maana lazima maisha yaendelee na tuna imani mambo yatabadilika,” alisema Choky.

Aina Ya Virutubisha Vya Vyakula Kwa Mjamzito



Moja kati ya changamoto kubwa ambayo huwakumbuwa wajawazito wengi hata kupelekea watu hao kuweza kujifungua kwa operation ni pamoja na kutokuzingatia lishe ya mama mjamzito, hata hivyo kutokana na changamoto hiyo wengi wa wajawazito wamekuwa wakichagua vyakula vya kula huku wakisahau vile vyakula walivyoviacha ndivyo vinavyosababisha kukosa lishe kamili ifaayo kwa mama mjamzito.
Zifuatavyo na aina ya vyakula na virutubisho vifaavyo kwa mama mjamzito;
Protini
Protini katika chakula cha mama mjamzito inasaidia ukuaji wa tishu za mtoto, hiyo ni pamoja na ubongo pia hata ogani nyingine za mwili. Pia inasaidia matiti na tishu za tumbo la uzazi kukua wakati wa mimba, na pia inachangia usambazaji mzuri wa damu.
Mama anahitajika kula milo 2 hadi 3 kwa siku yenye vyakula vya protini kama vifuatavyo:-
Nyama ya ng’ombe ya steki.
Samaki wa maji baridi au maji chumvi.
Maini.
Nyama ya kondoo
Karanga
Jamii ya mikunde kama maharage.
Kalshamu (Calcium)
Mama mjamzito anahitaji madini ya kalshamu kama miligramu 1000 kwa siku. Madini ya kalshamu yanasaidia kurekebisha viwango vya majimaji mwilini, kujenga mifupa na meno ya mtoto aliye tumboni.
Vyakula vyenye madini haya ni kama:-
Mayai.
Maziwa
Jibini
Maharage meupe
Maharage ya soya
Samaki
Kabichi
Madini ya chuma
Madini ya chuma husaidia kuongeza kiwango cha damu mwilini na kukukinga na upungufu wa damu mwilini (Anemia).
Vyakula vyenye madini ya chuma ni kama vifuatavyo:-
Spinachi
Mchicha
Kabichi
Nyama
Maini
Nafaka zisizokobolewa
Samaki
Mayai
Folic acid
Folic acid acid hupatikana katika vyakula tunavyokula, hii husaidia kujengeka vizuri kwa ogani za mtoto na kumuepusha na ulemavu pamoja na tatizo linalojulikana kitaalam kama mgongo wazi au neural tube defect (NTD). Katika nchi zinazoendelea mara nyingi wajawazito huwa hawapati virutubisho hivi kwa kiasi cha kutosha katika vyakula, kwa hiyo kinamama wajawazito huongezewa virutubisho hivi kama vidonge vya folic acid wanapohudhuria kliniki.
Folic acid hupatikana katika vyakula kama:-
Kabichi
Spinachi
Machungwa
Papai
Limao
Embe
Nyanya
Zabibu
Tikiti
Nafaka
Mkate
Jamii za mikunde kama maharage
Vitamini C
Matunda na mbogamboga huwa na vitamini C kwa wingi. Vitamini C husaidia uponaji wa majeraha kwa haraka, husaidia meno na fizi na kujengeka kwa mifupa, pia husaidia mmeng’enyo.
Vyakula vyenye vitamini C ni kama:-
Machungwa
Limao
Nyanya
Zabibu
Pilipili
Embe
Mboga za majani
Tahadhari
Mama mjamzito anatakiwa kuhakikisha kuwa vyakula vyote hivi, lazima viandaliwe katika mazingira safi kuepuka athari kwa mama na mtoto. Vyakula vingine visipopikwa vizuri vyaweza kuwa na vimelea hatari vya magonjwa kama Salmonella na E coli pia aina nyinginezo za vimelea ambavyo vyaweza kuwa hatari kwa afya.
Mpango wa mazoezi
Mpango wa mazoezi ni muhimu kwa mama mjamzito kwa kuwa mazoezi husaidia maendeleo ya kiafya ya mama na mtoto aliye tumboni.Pia mazoezi humsaidia mama kuwa mwenye nguvu wakati wa kujifungua. Mazoezi ya kutembea huwafaa sana kina mama walio wajawazito. Lakini ni vyema kushauriana na daktari wako kabla ya kujihusisha na aina yeyote ya mazoez

Fahamu Madhara Ya Usukaji Wa Nywele Bandia Na Uvaaji Wa Mawigi



Katika karne ya sasa , uvaaji wa wigi umekuwa fasheni katika sekta ya urembo na hutumika hususan na wanawake. Ingawa uvaaji wa wigi huwafanya wanawake hao kuonekana ni walimbwende zaidi.
Wigi huvaliwa zaidi na kinamama wenye asili ya Afrika au Wamarekani wa asili ya Afrika. Lakini tukiangalia moja ya chimbuko hasa la uvaaji wigi ni ubaguzi uliokuwepo wakati wa utumwa ambapo wale wenye ngozi nyeupe na nywele shombeshombe walipewa kazi za ndani na wale wasio na ngozi nyeupe na nywele zisizo shombeshombe walifanyishwa kazi ngumu za mashambani.
Watumwa waliopelekwa barani Amerika hawakuweza kuzihudumia nywele zao kutokana na hali ngumu, na mabwenyenye waliwashusha hadhi na kuwavunja moyo kwa kuwaambia hawakuwa na nywele bali ni "manyoya".
Lakini sababu nyingine inayodhaniwa kuwaathiri wanawake wa asili ya Afrika ni fikra kuwa mwanamke mwenye nywele ndefu pengine hadi mgongoni ni mrembo zaidi. Pia siku hizi warembo na wanaoshiriki katika mashindano ya urembo hujaribu kurefusha nywele zao ili kuwa na viwango na aina za mitindo ya ughaibuni.
Pamoja na kuwa wanawake wanajaribu kuwa warembo kwa uvaaji wa wigi, zifuatazo ni baadhi ya hasara au madhara kiafya ya uvaaji wigi na usukaji wa nywele za bandia.
1. Uvaaji wa wigi au nywele za bandia waweza kukusababishia mzio(allergy), endapo malighafi au kemikali zilizotumika kutengeneza wigi hiyo zitasisimua mfumo wa kinga ya mwili wa mvaaji.
2. Kupata mba ni tatizo jingine kutokana na uvaaji wigi, hii hutokana na kukosekana kwa hewa ya kutosha ya Oksijeni katika ngozi ya kichwa(scalp hypoxia) na katika tishu za shina la nywele. Kwa hiyo kama utaamua kuvaa wigi uhakikishe imetengenezwa kwa viwango vya ubora unaotakiwa na inapitisha hewa ya kutosha ya Oksijeni.
3. Pia waweza kunyonyoka nywele hata kama una nywele nzuri zenye afya, na kama utachagua kuvaa wigi na unataka kuepuka madhara hakikisha kuwa nywele zako ni safi, usilazimishe kuvaa wigi iliyo ndogo na yenye kubana sana, hakikisha unapata muda wa kupata hewa na nywele zako zinapakwa mafuta kuepuka ukavu wa ngozi ya kichwa na nywele kukatika .
4. Maumivu ya kichwa ni tatizo ambalo laweza kusababishwa na uvaaji wigi au usukaji wa nywele bandia. Wigi iliyo ndogo husababisha mkandamizo kichwani na kusababisha maumivu ya kichwa ya mara kwa mara.
5. Upotevu wa muda na fedha ni dhahiri kwa kuwa ufumaji wa nywele za bandia waweza kuchukua muda mrefu, itamlazimu mvaaji wigi kubadili kwa kununua mpya kila baada ya muda fulani au kuwa na wigi nyingi kwa ajili kubadili kulingana na fasheni.
6. Harufu mbaya huweza kujitokeza endapo mba na jasho vitachanganyikana na hupelekea uwepo wa bakteria au fangasi na kusababisha muwasho mkali, hii yaweza kumkosesha raha mvaaji wigi na mwenye kufuma nywele za bandia hasa pale anapokuwa katika majumuiko ya kijamii.Kama utachagua kuvaa wigi hakikisha nywele zako zinasafishwa na shampoo au sabuni, zinakaushwa vizuri na kupakwa mafuta.
Endapo mwanamama atachagua kuvaa wigi,asisahau kuwa nywele zake za asili zinahitaji matunzo,na azingatie wakati wa kununua wigi au nywele za bandia, ahakikishe ananunua yenye ubora unaotakiwa ili kuepuka madhara ya kiafya anayoweza pata kutokana na uvaaji wigi au anapofuma nywele za bandia.

Kilimo Cha Maharage ya Njano



Kilimo cha maharage ni rahisi na kinalipa sana kikifanyika kwa utaalamu. Gharama nafuu na ushindani wa soko sio mkubwa sana. Huhitaji kusafiri, kinachofanyika ni kuwaita wateja waje shambani kwako na kuchukua mzigo.
Ekari moja ya maharage ya njano kwa maeneo mengi unaweza pata gunia kati ya 8 – 12 au zaidi ila inategemea na eneo unalolimia.
Shamba la maharage kama unalima kwa kumwagilia unaweza lima mara tatu kwa mwaka . Hii ina maana ukilima ekari moja tu utakua na uhakika wa kipato cha uhakika na kikubwa kila baada ya miezi minne.
 Upandaji wa Maharage
1.Mbegu.
Upandaji wa maharage unatakiwa ufanyike katika muda muafaka kutokana na eneo ili kuweza kupata maji ya kutosha (mvua) na wakati wa mavuno kunatakiwa kuwe na ukavu ili maharage yasiharibikie shambani.
Maji mengi yaliyotuama na ukame siyo nzuri kwa maharage na husababishia mmea magonjwa na kuoza au kukauka.
Kuna aina nyingi za maharage ambazo zinaweza kupandwa kwa mfano (Rojo, Mshindi, Pesa, SUA 90 na Canadian wonder) ambazo ni mbegu zilizoboreshwa, lakini pia kuna mbegu za kawaida zilizopo kwa wakulima ambazo huhimili
baadhi ya magonjwa na wadudu.
Inashauriwa kupanda maharage katika umbali wa (50×20) sentimita 50 (mstari kwa mstari) na sentimita 20 (mmea kwa mmea), panda mbegu mbili za maharage katika shimo moja, mbegu zinaweza kupandwa katika umbali wa sentimita 3-6 kwenda chini.
Kama mbegu moja moja katika kila shimo, nafasi itapungua. Kwa maharage yaliyokuwa vizuri kunatakiwa kuwe na idadi ya mimea 150,000-200,000 kwa hekta (maharage mafupi), maharage yatambaayo idadi yake ni nusu ya maharage mafupi kwa hecta. Hekta 1 = ekari 2.471.
2. Mbolea.
Mimea huhitaji virutubisho kutoka kwenye udongo ili kuweza kukua na kuzalisha matunda yenye afya. Maharage huhitaji madini ya ‘phosphorous’ na ‘potassium’ ambayo hupatikana kutoka kwenye mbolea hai kama vile samadi, mboji, majivu, mkojo wa mifugo na mabaki ya mimea.
Ni muhimu kufahamu udongo ambao unatarajia kupanda mimea yako ili kutathmini viwango vya madini yaliyopungua ili kufanya juhudi za kuongeza.
Zaidi ya yote ni vizuri kutumia mbolea hai ambazo zinasaidia viumbe hai huweza kukua na kuendeleza kurutubisha udongo, kwa mfano mizizi ya maharage husaidiana na viumbe hai (nitrogen fixing bacteria) waishio kwenye udongo kutengeneza nitrogen. Mbolea za chumvichumvi huharibu na kufukuza viumbe hai kutoka kwenye udongo.
3.Magugu.
Inashauriwa kupalilia mimea kabla haijatoa maua. Shughuli hii inatakiwa ifanywe kwa uangalifu ili kukinga mimea isiharibike kwenye mizizi kwani uharibifu wa aina yoyote huweza kusababisha magonjwa kwa mmea.
Inashauriwa kupanda mimea kwa kuzunguka (crop rotation) ili kupunguza uwezekano wa magugu na maradhi kuweza kushambulia
mimea.
4.Wadudu na magonjwa.
Maharage hushambuliwa na wadudu na magonjwa. Miongoni mwa njia za kuzuia, kukinga na kufukuza wadudu ni kuhakikisha kuwa mimea ipo katika hali nzuri (imepaliliwa, nafasi ya kutosha na haijaharibika).
Pia kubadilisha aina ya mimea inayopandwa kwenye shamba moja mara kwa mara husaidia kupunguza uwezekano wa wadudu kuongezeka. Kwa baadhi ya wadudu kama vile viwavi (African Ballworm) huweza kufukuzwa kwa kutumia muarobaini au vitunguu saumu.
Maji ya muarobaini ni dawa nzuri sana kwaajili ya kufukuzia wadudu na haina madhara yoyote kwa binadamu.
5.Kukomaa na Kuvuna.
Maharage ya kijani yanatakiwa yavunwe kabla punje za maharage hazijakuwa sana. Hii ni kati ya wiki 7-8 baada ya kupanda. Maharage makavu huvunwa mara tu kiasi cha kuridhisha cha kukomaa na kukauka kinapokuwa kimefikiwa.
Kwa mfano asilimia 80 ya maharage yakishakomaa na kuanza kubadilika rangi (kukauka) au kwa aina nyingine kusinyaa yanakuwa tayari kwa mavuno.
Kwa kawaida mmea wote hung’olewa na kuwekwa juani ili uendelee kukauka kisha maharage hutolewa kutoka kwenye mmea na kuendelea kukaushwa ili kupunguza matatizo wakati wa kuhifadhi.
Baada ya kukauka hadi kufikia angalaua asilimia 12 ya unyevu, maharage yanatakiwa yahifadhiwe kwenye chombo chenye mfuniko kama vile ndoo ya plastiki au pipa na kuendelea kuyaangalia mara kwa mara ili kuhakikisha kuwa wadudu hawajaingia na kisha kuyafunika tena.
6. Kilimo mchanganyiko.
Ni vizuri sana na inashauriwa kupanda maharage pamoja na mimea ya jamii nyingine kama vile mahindi kwani husaidia katika kusambaza madini ya nitrogen na kwa maharage yenye kutambaa, hupata sehemu ya kujishikilia au kutambalia.
Maharage yanaweza yakapandwa katikati ya mistari ya mahindi. Pia viazi huweza kupandwa pamoja na maharage. Inashauriwa kutokupanda maharage pamoja na mimea mingine ya jamii ya maharage (leguminous) kwani husababisha mimea isiweze kukua vizuri kwasababu ya kutokupata virutubisho vya kutosha na huweza kusababisha matatizo kama ya wadudu kama nzi weupe.

Tabia ya kuzoeana. inavyoweza kuathiri maisha yako ya kimahusiano



kuzoeana baina ya wanandoa ni jambo zuri, kwa maana ya kila mmoja kumfahamu mwenzake, lakini kuzoeana huku kunaweza kuzalisha dharau hususani kwa upande wa mwanamke kwa kutojali usafi wake, mavazi anayovaa, chakula anchopika, nidhamu ya nyumba na mpangilio kwa ujumla.
Matatizo mengi ndani ya nyumba yanaweza kusababishwa na moja au baadhi ya tabia hizo, ambazo huenda ikawa hazitokani na dharau, bali kuzoeana, kwa mfano, siku za mwanzo wa ndoa mwanamke huwa anajali sana usafi wa mwili wake, umaridadi wa nguo anazovaa, usafi wa nyumba na nidhamu ya hali ya juu, upishi wa chakula unaozingatia vionjo na ubunifu, mapokezi yenye bashasha na wakati mwingine hata kumkumbatia mumewe arudipo kutoka kazini.
Lakini baada ya kuzoeana yote hayo hubadilika, mwanamke huhisi kuwa hana jipya la kumuonyesha mumewe, hujiona wameishakuwa watu wazima sasa, na mara nyingi utakuta mwanamke huyu anashinda na sare (uniform) moja kuanzia asubuhi hadi anapopanda kitandani usiku, mambo ya Hinna, nguo za fashion, salon, manukato, kujipamba na dhahabu huyafanya pale anapotoka kwenda harusini na sio nyumbani. Huku ndio kuzoena, na tafsiri sahihi ni kudharau.
Hivyo ili kulinda kibarua cha chako cha mahusiano ni vyema ukajifunza kila wakati kutofanya vitu ambavyo vimekuwa havijayajengi mahusiano yako.

Monday, 25 December 2017

Lukuvi, Ummy Mwalimu watajwa tena



Siku 6 kabla ya kufunga mwaka 2017, wasomaji na wafuatiliaji wa habari kupitia mitandao ya kijamii ya Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), wametoa maoni wakiwataja mawaziri watano wa Serikali waliofanya vizuri katika maeneo wanayoyasimamia.
Wametoa maoni hayo takriban wiki moja baada ya gazeti hili kufanya tathmini ya utendaji wa mawaziri watano. Katika orodha hiyo, mawaziri wawili wameingia katika makundi yote mawili ambao ni William Lukuvi wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Ummy Mwalimu anayeisimamia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto.
Wananchi wametoa maoni hayo kupitia swali lililoulizwa kwenye akaunti za MCL za mitandao ya kijamii za Instagram, Facebook na Twitter.
Swali hilo lililoambatana na picha ya Rais John Magufuli akiongoza kikao cha Baraza la Mawaziri lililisema, “Ni waziri gani katika Serikali ya Rais Magufuli ambaye amekuvutia kwa utendaji wake mwaka huu? Kwa nini? Toa maoni yako.”
Mbali ya Lukuvi na Ummy, mawaziri wengine waliotajwa kufanya vizuri kwa maoni ya wasomaji hao ni; Selemani Jafo (Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa); Dk Hamisi Kigwangalla (Maliasili na Utalii) na Profesa Makame Mbarawa (Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano).
Kwa maoni yao, Lukuvi ndiye anayeongoza akifuatiwa na Jafo, Dk Kigwangalla, Ummy na Profesa Makame.
Hadi jana jioni, Lukuvi alikuwa akiongoza katika mitandao yote ya Instagram, Facebook na Twitter akimwagiwa sifa na wasomaji zaidi ya 100.
Katika gazeti hili toleo la Desemba 16, mawaziri waliotajwa mbali ya Lukuvi na Ummy walikuwa, Angellah Kairuki wakati huo akiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora na Utumishi), Profesa Palamagamba Kabudi (Katiba na Sheria) na Profesa Joyce Ndalichako (Elimu, Sayansi na Teknolojia).
Ingawa waliotoa maoni kupitia mitandao ya kijamii ya MCL waliwataja mawaziri hao watano, wapo ambao walisema hawakufanya vyema.
Wengine waliwataja mawaziri vivuli kutoka kambi ya upinzani akiwamo Tundu Lissu wa Katiba na Sheria huku baadhi wakimtaja aliyekuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye aliyeng’olewa katika wadhifa huo Machi 23.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa pia ametajwa kama kiongozi anayemudu nafasi yake vyema kwa kuwasimamia watendaji walio chini yake, wakiwamo mawaziri akielezewa kuwa mwaka huu ametimiza majukumu yake vyema.
Akichangia swali hilo, angwisa137 alisema, “Kuanzia mwakani tunatarajia makubwa mno kutoka kwa mawaziri. Watakuwa wamezijua wizara zao vizuri. Ila Lukuvi yuko vizuri mno. Hamisi Kigwangalla namkubali. Ila mawaziri waache kufanya kazi kwa mazoea tunahitaji mabadiliko ya kweli.”
Mwingine alikuwa maseleizengo ambaye alisema, “Waziri Lukuvi ni pekee amefanya kazi ya wanyonge... ameokoa viwanja vingi sana vya wanyonge vilivyokuwa vimeibwa na wenye fedha. utapeli wa ardhi umepungua sana.”
Mtoa maoni mwingine, mikeuswege alisema, “Lukuvi na Jafo ni wahalisia wengine walio wengi wanafanya kwa pressure.’’
Kwa maoni yake, Isaya Wa Yesu alisema, “Majaliwa ni Waziri Mkuu ambaye anajua kuyatumia mamlaka yake vizuri, Lukuvi amerudisha nidhamu kwa maofisa ardhi pia amewapa watu uhuru na amani ya kumiliki ardhi.”
Kareemgriff alisema, “Majaliwa, kubwa kabisa alivyotenganisha utendaji wake na masuala ya kichama, amekuwa si mwongeaji bali mtendaji.”
Katika maoni yake Julius S. Bugarika alisema, “Sauti ya watu wengi ni sauti ya Mungu. Lukuvi comment (maoni) nyingi zinaukubali utendaji wake. Waziri aliyefanya vizuri kiutendaji mwaka 2017 ni William Lukuvi.”
Mtoa maoni mwingine, witnessselestin alisema, “Mh. Lukuvi sababu ametafuna mifupa mingi na migumu iliyowashinda watangulizi wake na waheshimiwa wengine waige kutoka kwake huku edo_de__best akisema ‘’Makame Mbarawa naona anasimamia vizuri taaluma yake.”
Mwingine alikuwa meshackkwila ambaye alisema, “Mh Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu ni mtu mwenye busara anaongea kwa kufikiri sana naweza kusema ni kiongozi bora wa kuigwa.”
France Kavishe alisema, “Dah kwangu waziri aliyefanya vizuri na anayefanya vizuri awamu hii kwangu ni Mh. Dr @HKigwangalla.”
Mchangiaji mwingine, festosimkwayi_sr alisema, “Mheshimiwa Ummy Mwalimu anafanya mambo yake katika kulitumikia Taifa kwa uhakika bila papara wala mbwembwe. Hakika ni waziri wa afya anayetumia elimu na dhamana aliyopewa vyema.”
Akizungumzia maoni hayo ya wasomaji wa MCL, Lukuvi alisema, “Nimefurahi kuona wameridhika na utendaji wa Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Wizara ya Ardhi, tutaendeleza ushirikiano huo.”
Waziri Lukuvi alisema moja ya jukumu alilopewa na Rais John Magufuli ni kuhakikisha anamaliza migogoro ya ardhi.
Alisema anafanikiwa kutokana na juhudi zake na ushirikiano anaoupata kutoka kwa watendaji wa wizara.
“Tuliacha watendaji wa Serikali huko nyuma wakatengeneza migogoro, hakuna mgogoro wa ardhi ambao hauhusiki na watendaji au viongozi wa Serikali. Nimeambiwa na Rais ndani ya miaka mitano hii jukumu kubwa liwe ni kutatua migogoro ya ardhi,” alisema Lukuvi.
Akizungumzia hilo, Waziri Ummy alianza kwa pongezi akisema, “Nashukuru kwa ‘feedback’ kutoka kwenu na kutoka kwa wananchi, nawashukuru sana! Hakika mnanitia moyo katika utendaji wangu.”
Alisema sekta ya afya bado inakabiliwa na changamoto nyingi lakini anachopenda kuwaahidi Watanzania ni kuendelea kupambana usiku na mchana ili kutatua changamoto kadhaa.
Waziri Ummy alizitaja changamoto hizo kuwa ni kuendelea kuboresha huduma za mama na mtoto ili kupunguza vifo vya wajawazito na uzazi na kuimarisha upatikanaji wa dawa muhimu katika ngazi zote za kutoa huduma na hasa ngazi ya msingi yaani zahanati na vituo vya afya.
Alitaja mikakati mingine kuwa ni pamoja na kuimarisha hospitali za rufaa za mikoa ili kuziwezesha kutoa huduma za matibabu ya kibingwa kwa kuzipatia madaktari bingwa, vifaa na vifaa tiba lengo likiwa ni kusogeza huduma za kibingwa karibu na wananchi na kupunguza mrundikano wa wagonjwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Jambo lingine ambalo alisema wizara yake itahakikisha inalifanya ni, “Kuongeza idadi ya Watanzania wanaojiunga katika mifuko ya bima ya afya ili kupata huduma za matibabu bila kikwazo cha fedha pindi wakiugua. Hivi sasa ni asilimia 32 tu ya Watanzania wamejiunga na mifuko ya bima ya afya. Ninaamini kwa mwaka 2018, sekta ya afya tutapata mafanikio makubwa,” alisema waziri Ummy.
Waziri Mbarawa akichangia swali hilo kwenye ukurasa wetu wa Twitter alindika ‘’Shukrani kwa wote tuendelee kushirikiana kwa maendeleo ya wananchi wote.”
Juhudi za kuwapata mawaziri wengine waliotajwa na wasomaji ambao ni Dk Kigwangalla na Jafo ziligonga mwamba kwa kuwa simu zao za mikononi ziliita pasipo kupokewa na wengine hazikupatika kabisa.

Hussein Bashe Aomba Radhi





Mbunge wa Nzega Mjini, kwa tiketi ya (CCM) Hussein Bashe amefunguka na kuwaomba radhi baadhi ya wananchi wa Nzega na Watanzania mbalimbali ambao kwa namna moja au nyingine amewakwaza mwaka huu katika utekelezaji wa majukumu yake.
Bashe amesema hayo kupitia mitandao yake ya kijamii ambapo anatuma salamu za heri ya sikukuu kwa wananchi na watanzania na kudai kuwa wamsamehe pale ambapo amewakosea katika utekelezaji wa majukumu yake ya kibunge.

DK. Shein atoa onyo Kali



Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, amewaonya wale waonadhani kuwa yeyeni mpole na kwamba hawezi kuwachukulia hatua viongozi wa serikali na chama wanaovunja nidhamu na kukiuka taratibu za utendaji.
Dk. Shein ambaye pia ni Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, ametoa kauli hiyo mjini Zanzibar katika sherehe za kumpongeza baada ya kuchaguliwa tena kushika wadhifa wa Makamu Mwenyekiti wa CCM katika Mkutano Mkuu wa Tisa wa CCM uliofanyika mjini Dodoma hivi karibuni.
Amesema, kiongozi wa nchi anapaswa kutumia taratibu za uongozi na si kukurupuka kwa kuwaadhibu watu bila ya utaratibu.
Amesema yupo madhubuti na imara kwa kuwashughulikia wanaovunja nidhamu ya chama hicho na hatomuonea wala kumuadhibu mtu bila kufuata utaratibu wa maadili ya CCM .